Mikutano ya Utumishi wa Shambani
1. Kwa nini tunapaswa kuwa wenye utaratibu tunapoenda katika utumishi wa shambani?
1 Yesu alishughulikia kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme kwa njia nzuri na kwa utaratibu. Leo pia, wale walio na jukumu la kuhubiri kuhusu Ufalme wanataka sana kuona kazi hiyo ikifanywa kwa utaratibu. Kupatana na hilo, makutaniko duniani kote hutumia mikutano ya utumishi wa shambani kupanga vikundi vya wahubiri wa Ufalme kwa ajili ya kazi ya kuhubiri.— Mt. 24:45-47; 25:21; Luka 10:1-7.
2. Ni mambo gani yatakayoshughulikiwa katika mikutano ya utumishi wa shambani?
2 Mpango Mzuri: Mikutano ya utumishi wa shambani inakusudiwa kutoa mwongozo na maelekezo yanayofaa na kuwatia moyo wale walio tayari kwenda katika utumishi wa shambani. Andiko la siku linaweza kuzungumziwa kifupi ikiwa linahusu utumishi wa shambani. Mara kwa mara, habari katika Huduma Yetu ya Ufalme, kitabu Kutoa Sababu, au labda kitabu Shule ya Huduma, zinaweza kuzungumziwa ili wote waliofika watayarishwe kwa ajili ya utumishi wa shambani siku hiyo. Onyesho fupi kuhusu jinsi ya kutoa toleo la mwezi linaweza kupangwa. Kabla ya sala ya kumalizia, wote wanapaswa kujua ni nani watakaoandamana nao na pia eneo ambako watahubiri. Punde baada ya mkutano usiozidi dakika 15, wote wanapaswa kwenda kwenye eneo.
3. Ni nani walio na jukumu la kupanga mikutano ya utumishi wa shambani?
3 Jinsi Inavyopangwa: Mwangalizi wa utumishi ana jukumu la kusimamia mipango ya mikutano ya utumishi wa shambani. Nao waangalizi wa vikundi au wasaidizi wao, wana jukumu la kufanya mipango kwa ajili ya utumishi wa shambani na kuandamana na vikundi vyao katika huduma ya shambani mwishoni mwa juma. Baadhi ya waangalizi au watumishi wa huduma wanaweza kuandamana na vikundi vya utumishi katikati ya juma. Waangalizi wa vikundi wanapaswa kushirikiana kwa ukaribu na mwangalizi wa utumishi na kuhakikisha vikundi vyao vina eneo la kutosha ili kuhubiri nyumba kwa nyumba mwishoni mwa juma. Mwangalizi wa utumishi atafanya mipango ili kuwe na ndugu ambao wataongoza vikundi katikati ya juma.
4-6. (a) Mikutano ya utumishi wa shambani inakusudiwa kutimiza nini kuhusiana na eneo la kutaniko? (b) Ni mambo gani yanayopaswa kuzingatiwa ili kuamua kuhusu uhitaji wa mikutano ya utumishi wa shambani?
4 Mikutano ya Utumishi wa Shambani Ifanywe Wakati Gani na Wapi? Badala ya kutaniko zima kukutana mahali pamoja, ni heri mikutano ya utumishi ifanywe mahali panapofaa kotekote katika eneo, hasa kwenye nyumba za akina ndugu, ili kuhakikisha kwamba eneo la kutaniko linahubiriwa kikamili. Majumba ya Ufalme yanaweza pia kutumiwa kwa ajili ya mikutano hiyo. Makutaniko mengi hutumia Jumba la Ufalme kufanya mikutano ya utumishi wa shambani punde baada ya hotuba ya watu wote na Funzo la Mnara wa Mlinzi siku ya Jumapili. Jitihada zinapaswa kufanywa ili wahubiri wasitumie wakati mwingi kusafiri kwenda kwenye eneo. Kwa hiyo, mipango inaweza kuchunguzwa mara kwa mara ili kuhakikisha kwamba mahali ambapo mikutano ya utumishi wa shambani inafanywa, bado panafaa ili eneo lihubiriwe vizuri na kikamili.
5 Kwa kutegemea eneo, inaweza kuamulia ni wakati gani unaofaa wa kufanya mikutano ya utumishi wa shambani, na ni mara ngapi mikutano hiyo inapaswa kufanywa katika juma. Maswali yafuatayo yanaweza kuwasaidia kuamua mahali na wakati unaofaa wa kufanya mikutano ya utumishi wa shambani.
6 Ni eneo gani linalohitaji kuzingatiwa zaidi? Ni wakati gani unaofaa hasa kuhubiri nyumba kwa nyumba? Je, mpango unaweza kufanywa ili kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba au ya kufanya ziara za kurudia ifanywe jioni? Mipango yote kuhusu utumishi wa shambani inapaswa kuwekwa kwenye ubao wa matangazo ya kutaniko. Ni tamaa yetu sote tukiwa wahubiri wa Ufalme kuhubiri kikamili katika eneo lote tulilogawiwa hivi kwamba tunaweza kusema kama mtume Paulo alivyosema: “Sina tena eneo lisiloguswa.”—Rom. 15:23.
7. Ndugu anayepewa mgawo wa kuongoza kikundi cha utumishi wa shambani ana jukumu gani?
7 Kuongoza Mikutano ya Utumishi wa Shambani: Ndugu anayepewa mgawo wa kuongoza mkutano wa utumishi wa shambani anaonyesha kwamba anauheshimu sana mpango huu wa kiroho kwa kujitayarisha vizuri. Mikutano hii inapaswa kuanza kwa wakati na inapaswa kuwa yenye kuelimisha na mifupi—kati ya dakika 10 na 15. Anayeongoza anapaswa kuwa na eneo litakalohubiriwa kabla ya mkutano kuanza. Baada ya mkutano wa utumishi wa shambani kuisha, si lazima kuwangoja wale ambao wamechelewa, lakini linaweza kuwa jambo linalofaa kuacha ujumbe ili wapate kujua mahali ambapo kikundi kinahubiri. Mara tu mkutano unapoisha, wote wanapaswa kuondoka na kuelekea kwenye eneo ambako watahubiri. Mkutano wa utumishi wa shambani uliopangwa vizuri na ambao ni wenye kuelimisha, unatoa mwongozo unaohitajika ili wote waliofika waweze kutimiza huduma yao siku hiyo.—Met. 11:14.
8. Ni katika njia zipi ambazo wale wanaohudhuria mikutano ya utumishi wa shambani wanaweza kushirikiana na wale wanaoiongoza?
8 Kuhudhuria Mkutano wa Utumishi wa Shambani: Ushirikiano ni muhimu. (Ebr. 13:17) Inapowezekana, ndugu anayeongoza kikundi atamsaidia mhubiri yeyote anayehitaji mwenzi wa kuhubiri naye. Inafaa wahubiri walio na uzoefu wahudhurie mkutano wa utumishi wa shambani ili kuwasaidia wahubiri wapya na wasio na uzoefu. Wale walio tayari kuhubiri na mtu tofauti mara kwa mara, wanaweza kutimiza mambo mengi mazuri. (Met. 27:17; Rom. 15:1, 2) Wote wanapaswa kujitahidi sana kufika kwa wakati. Ikiwa tunaheshimu mpango huu wa kiroho na tunawafikiria ndugu na dada zetu, tutachochewa kufanya marekebisho yanayohitajika kuhusiana na mkutano wa utumishi wa shambani.—2 Kor. 6:3, 4; Flp. 2:4.
9. Ni katika njia gani muhimu ambayo mapainia wanaweza kuunga mkono mikutano ya utumishi wa shambani?
9 Mapainia Wanavyoiunga Mkono: Mapainia wanafanya jambo muhimu na wanawatia wote moyo wanapounga mkono mikutano ya utumishi wa shambani. Mapainia wana shughuli nyingi sana. Mbali na kuongoza mafunzo ya Biblia na kufanya ziara za kurudia, huenda pia wakahitaji kutunza familia na kufanya kazi ya kuajiriwa. Kwa hiyo, hawahitaji kuhisi wanawajibika kuhudhuria kila mkutano wa utumishi wa shambani uliopangwa na kutaniko, hasa ikiwa mikutano hiyo inafanywa kila siku. Hata hivyo, yamkini inawezekana kwa mapainia kuhudhuria angalau mikutano fulani kila juma. Kwa kadiri fulani, wahubiri wa kutaniko huzoezwa kwenye mikutano ya utumishi wa shambani, na ujuzi na uzoefu wa mapainia unaweza kuwasaidia sana. Mapainia wamepata uzoefu katika huduma kwa sababu wanashiriki katika utumishi wa shambani mara nyingi, nao wanaweza kutumia uzoefu huo kuwasaidia wengine. Wamekuwa mifano ya kuigwa kwa kuwa wanashiriki kwa bidii katika huduma na kwenye mikutano ya utumishi wa shambani. Maelezo yao kwenye mikutano hiyo yanathaminiwa sana.
10. Kwa nini inafaa wahubiri wote wa Ufalme waunge mkono kwa moyo wote mikutano ya utumishi wa shambani?
10 Kama Yesu na mitume wake walivyofanya, sehemu kubwa ya kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme inatimizwa kwa kuhubiri nyumba kwa nyumba. Mikutano ya utumishi wa shambani inafanywa ili kutiana moyo na kuwa na matokeo katika huduma. Wahubiri wote wa habari njema wanapaswa kuunga mkono kadiri wawezavyo mipango yote inayohusu kazi ya kuhubiri. (Mdo. 5:42; 20:20) Sote na tuunge mkono kwa moyo wote mikutano ya utumishi wa shambani. Kwa kufanya hivyo, tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atatubariki sana na tunaweza kufanya moyo wa Kiongozi wetu, Yesu Kristo, ushangilie tunapohubiri habari njema kuhusu Ufalme wa Mungu.—Mt. 25:34-40; 28:19, 20.