Endelea Kuwa Mwenye Nguvu Kiroho, Baki Ukiwa Safi kwa Ajili ya Utumishi wa Yehova
1 Kwenye Isaya 60:22, Yehova alifanya ahadi inayotimizwa mbele ya macho yetu yenyewe: “Mdogo atakuwa elfu, na mnyonge atakuwa taifa hodari; Mimi, BWANA, [Yehova, NW] nitayahimiza hayo wakati wake.” Tunapofikiria taifa, tunawazia kikundi kikubwa cha watu wanaofungamanishwa pamoja kwa mapendezi yale yale na ambao wanatenda wakiwa chini ya mamlaka ya serikali iliyofanyizwa.
2 Ripoti ya utumishi wa shambani ya 1991 ilionyesha kilele cha ulimwenguni pote cha wahubiri wa habari njema 4,278,820, ongezeko la asilimia 6.5 zaidi ya mwaka uliotangulia. Kwa kweli Yehova amekusanya halaiki kubwa ya watu wanyofu wanaotaka kujitenga wenyewe na mfumo huu wenye uonevu na kuwa raia waaminifu-washikamanifu wa serikali ya Ufalme wa Kimesiya wa Mwana wake, Yesu Kristo. Mwaka baada ya mwaka idadi ya wanaokusanywa inaendelea kuongezeka. Sisi tunaonea shangwe kuwa sehemu ya taifa hilo linaloweza kuelezwa kihalisi kuwa jamii ya ulimwengu mpya. Kwenye mwadhimisho wa Ukumbusho katika 1991, jumla ya hudhurio ilikuwa 10,650,158, ongezeko la asilimia 7 zaidi ya 1990. Hilo lawakilisha uwezekano mkubwa ajabu wa wengi zaidi kuungana nasi wakiwa raia wa Ufalme.
3 Bila shaka, tunang’amua kwamba si watu wote wakiwa mtu mmoja mmoja waliotiwa ndani ya hesabu iliyo juu ya waliohudhuria Ukumbusho wamejitenga wenyewe na ulimwengu huu kwa kadiri inayohitajiwa wakubalike kabisa kuwa watu wa Yehova. Watu kutoka kwa mataifa yote ‘wanaendea nyumba ya BWANA, [Yehova, NW] makundi makundi,’ lakini wanahitaji ‘kufundishwa kikamili juu ya njia zake’ ili waweze ‘kutembea katika mapito yake.’ (Isa. 2:2-4) Watu zaidi ya milioni nne waliohudhuria Ukumbusho wamekubali maagizo ya Mungu, wakipata nguvu ya kiroho ambayo imewachochea kudumisha mwenendo safi na kustahili kushiriki katika kazi ya kuhubiri Ufalme inayotimizwa sasa. (Mt. 24:14) Watu kama hao wana msimamo mzuri machoni pa Yehova na huonea shangwe faida za maandalizi yote ya ajabu anayowatolea. Ni lazima idadi ya watu zaidi ya milioni sita wanaobaki wafanye nini ikiwa wao pia watakuwa wenye nguvu kiroho na safi kwa ajili ya utumishi wa Yehova?
4 Ni lazima wao ‘waishindanie imani.’ (Yuda 3) Wanapochagua kutembea katika njia ya Yehova, wanapatwa na msongo kutoka kwa Ibilisi kupitia majaribu, vishawishi, na uvutano mbaya. Kama Paulo, ni lazima wamtegemee Yehova awape nguvu ya kuvumilia. (Flp. 4:13) Yehova hutia nguvu watu kama hao kupitia wale ambao tayari ni wenye nguvu katika imani. Paulo alihimiza kwamba ‘sisi tulio na nguvu tuuchukue udhaifu wao wasio na nguvu.’ (Rum. 15:1, 2) Wakati wenye nguvu na wasio na nguvu wanapoungana, kunakuwako nguvu ya kusimama imara. “Afadhali kuwa wawili kuliko mmoja. . . . Hata ikiwa mtu aweza kumshinda yule aliye peke yake, wawili watampinga.”—Mhu. 4:9, 12.
5 Hilo lamaanisha kwamba kwa kufaa, wapya hututegemea sisi kuwa ndiyo njia ambayo kwayo wanaweza kupata nguvu kutoka kwa Yehova. Wale miongoni mwetu ambao ni Wakristo walio wakfu ni lazima tuendelee kuwa wenye nguvu kiroho ikiwa tutawasaidia wapya. Wakristo wenye nguvu huweza ‘kugawa zawadi za kiroho,’ tokeo likiwa ni ‘kuimarishana.’ (Rum. 1:11, 12, HNWW) Hiyo ni njia moja ya msingi ambayo Yehova hutumia kutuunganisha na kutufanya sote kuwa ‘thabiti na wenye nguvu.’—1 Pet. 5:9-11.
6 Tunapaswa kulifanya liwe lengo letu kusaidia wapya hao hali wakati huo huo tukiendelea kutambua mahitaji yetu wenyewe ya kiroho. (Mt. 5:3) Kuwa watu wa kiroho ndio ufunguo wa nguvu yetu. Hiyo ni sifa inayopasa kukuzwa na kuimarishwa kwa kula chakula cha kiroho kwa ukawaida. Kupitia tengenezo lake, Yehova huandaa mipango iliyosawazika kwa ajili ya funzo la Neno lake. Mikutano mitano ya kila juma huwa na sehemu ya maana katika kutufanya tuwe wenye nguvu, ‘ikituhimiza katika upendo na kazi nzuri.’—Ebr. 10:24.
7 Faida za mikutano hiyo zinaongezwa zinapounganishwa na mazoea mazuri ya funzo la kibinafsi na la familia. Sisi sote twapaswa kusoma na kutafakari juu ya andiko la siku, kuenda sambamba na mpango wa usomaji wa Biblia kama unavyoonyeshwa katika Ratiba ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, na kutayarishia Funzo la Kitabu la Kundi na Funzo la Mnara wa Mlinzi, hiyo ikiwa miradi yetu midogo. Kila familia itaamua jinsi hilo litakavyopangwa, ikihakikisha kwamba hayo yanafanywa kwa ukawaida. Pia, kichwa cha familia ahakikishe kwamba programu ya funzo inafanyizwa iweze kuridhisha mahitaji ya kiroho ya familia. Kwa njia hiyo ‘nyumba itajengwa na kuthibitika.’ (Mit. 24:3) Tukiwa wenye kudhamiria katika mazoea yetu ya kujifunza tukiwa mtu mmoja mmoja na tukiwa familia, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatubariki na roho yake itatusaidia kuvumilia majaribu mbalimbali kwa mafanikio.—Yak. 1:2, 3; 1 Pet. 4:11.
8 Kuendelea Kuwa Safi na Bila Lawama: Ingawa Yehova hutualika kwa uchangamfu tumkaribie yeye, wakati ule ule, anafanya iwe wazi kwamba hilo hufanywa kwa msingi wa kujizoeza kwetu imani katika damu ya Yesu iliyomwagwa, ambayo “yatusafisha dhambi yote.” (1 Yoh. 1:7; ona pia Waebrania 9:14.) Tunaweza kuendelea kuimarisha imani yetu kwa funzo la kibinafsi la Neno la Mungu na kwa kutumia yale tunayojifunza. Wengine hukosa kufanikiwa baadaye kwa sababu ama wanashindwa kula chakula cha kiroho ama hawajitahidi kukitumia maishani mwao. Hilo huwafanya wakose ulinzi kwa mashambulio ya Shetani. Wengine wamekuwa dhaifu kiroho, tokeo likiwa ni kutotenda. Kwa kusikitisha, wengine wamejiruhusu washindwe kwa kufanya makosa mazito, ikiwafanya watengwe na ushirika. Paulo alionya: “Anayejidhania kuwa amesimama na aangalie asianguke.” (1 Kor. 10:12) Tukipuuza kwa makusudi funzo, hudhurio la mikutano, na utumishi, tunaweza kunaswa kwa urahisi na uvutano usio mtakatifu na vishawishi.—Ebr. 2:1; 2 Pet. 2:20-22.
9 Ni jambo la maana kwamba tujiweke safi katika kila njia: kimwili, kiakili, kiroho, na kiadili. (2 Kor. 7:1) Ulimwengu unaotuzunguka unaendelea kuwa mpotovu na wenye kushusha tabia zaidi kila siku. Ibilisi anaendelea kupata njia zenye udanganyifu zaidi ili kutunasa. Kuendelea kwetu kuwa wenye nguvu kiroho kunahakikisha kwamba ‘hatukosi kuzijua fikira zake.’ (2 Kor. 2:11) Maagizo na shauri tunalopokea kutoka kwa tengenezo la Yehova hutuwezesha tutambue na kupinga uvutano mbaya.
10 Wale wanaoongoza kundini wana daraka la kuweka mfano unaofaa kwa wengine kwa kuendelea kuwa wenye nguvu na kubaki wakiwa safi. Paulo alikazia daraka hilo aliposema: “Wakumbukeni wale waliokuwa wakiwaongoza. . . . Kwa kuuchunguza sana mwisho wa mwenendo wao, iigeni imani yao.” (Ebr. 13:7) Ni jambo la maana kwamba wazee na watumishi wa huduma waliowekwa wawe mifano katika mwenendo wao wa kibinafsi na pia katika kushughulikia madaraka yao wakiwa vichwa vya familia. Wanapaswa wajitahidi kuwa kama kijana Timotheo, aliyehimizwa ‘awe kielelezo katika usemi na mwenendo, na katika upendo na imani na usafi.’ (1 Tim. 4:12; 1 Pet. 5:3) Sisi wengine wote hushiriki daraka hilo la kuwa mifano mizuri kwa kudumisha mwenendo wenye kuheshimika. Mara nyingi, wapya hupambanua kweli, pamoja na tengenezo la Yehova, kwa yale waonayo ndani yetu. Tunataka tuhakikishe kwamba yale waonayo yanawatia moyo kuchukua nafasi yao katika tengenezo safi la Yehova.
11 Kukusanywa kwa watu kwa ajili ya wokovu kupita “dhiki iliyo kuu” kunaendelea kuongeza mwendo. (Ufu. 7:14) Ni wale tu wanaokuwa wenye nguvu kiroho na kujiweka safi ndio watakaookoka hatimaye. Mengi yanategemea mambo haya: (1) kudumisha mazoea mazuri ya funzo la kibinafsi na kutafakari juu ya Neno la Mungu; (2) kuonyesha kupendezwa kibinafsi kwa moyo mweupe na mmoja na mwenzake tukitamani kutoa kitia-moyo; na (3) kufanya kazi pamoja kwa umoja ili kudumisha mwenendo safi utakaoheshimu jina la Yehova. Kufanya mambo hayo kutatuhakikishia mibaraka na ulinzi wa Yehova wakati ulimwengu huu unapofikia mwisho wao. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba tutakuwa miongoni mwa wale ‘waaminifu wanaohifadhiwa na Yehova.’—Zab. 31:23.