Ni Nini Tutakalotimiza Wakati wa Mwaka Huu wa Utumishi?
1 Kwa kuwa mwaka wa utumishi wa 1994 umeanza katika Septemba 1, sasa ni wakati unaofaa kwetu sote tukiwa watu wa Yehova kuweka mradi ili kusitawisha yale tunayotamani kutimiza tukiwa watu mmoja-mmoja na tukiwa tengenezo wakati wa mwaka huu mpya wa utumishi.
2 Endeleeni Kukua Kiroho: Ikiwa tumeshirikiana na kweli hivi majuzi, twapaswa kutamani kuwa wenye nguvu katika imani. (Ebr. 6:1-3) Ikiwa tayari tu wenye nguvu kiroho, twapaswa kusaidia si wapya na wengine wanaohitaji msaada tu bali pia twapaswa kutoa uangalifu kwa hali yetu wenyewe ya kiroho, tusifikiri kamwe kwamba tuna ujuzi wote wa Biblia na maarifa yenye kuhitajiwa katika maisha ya Kikristo. Je! sisi huchunguza andiko la siku, kuendelea na programu ya usomaji-Biblia iliyowekwa kwenye Ratiba ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, na kutayarisha Funzo la Kitabu la Kutaniko na Funzo la Mnara wa Mlinzi? Huo wapaswa kuwa mradi wa kuanzia kwetu sote. Ni lazima tuendelee kukua kiroho ikiwa tutaokoka uharibifu wa mfumo huu mbovu wa mambo na kuhifadhiwa kuingia katika ulimwengu mpya wa Mungu.—Linganisha Wafilipi 3:12-16.
3 Baki Ukiwa Safi Kiroho: Ili tukubaliwe kabisa na Yehova, ni lazima tusafishwe kutoka kwenye “uchafu wote wa mwili na roho.” (2 Kor. 7:1) Tunapokuwa safi, kwa nini tutake kurudi tena ‘kugaa-gaa katika matope’ ya ulimwengu huu mbovu wa kale? (Linganisha 2 Petro 2:22.) Twapaswa kuazimia kubaki tukiwa wenye nguvu na safi kiroho. Kisha hatutakosa kujua hila mbaya za Shetani na kushindwa, tutumbukie kwenye dhambi na kukosa kibali cha Yehova.—2 Kor. 2:11.
4 Tii Shauri Lenye Hekima: Mithali 15:22 hueleza hivi: “Pasipo mashauri makusudi hubatilika; bali kwa wingi wa washauri huthibitika.” Hata hivyo, kumbuka kwamba, mwanamume aliyezungumza maneno hayo, Sulemani, baadaye aliruhusu ‘wake zake wamgeuze moyo wake, afuate miungu mingine’ kwa sababu alikosa kutii shauri la Mungu la kutochukua wake wa kigeni. (1 Fal. 11:1-4) Kwa hiyo, tusipofuata kibinafsi shauri lenye hekima, twaweza kutazamiaje kuwa wenye matokeo katika utumishi wa Yehova au kuweka kielelezo kinachostahili kuigwa? (1 Tim. 4:15) Shauri la Biblia litatusaidia tulinde moyo wetu. (Mit. 4:23) Kupenda yale ambayo Yehova hupenda, kuchukia anayochukia, kutafuta mwongozo wake daima na kufanya yanayompendeza ni ulinzi wa hakika.—Mit. 8:13; Yn. 8:29; Ebr. 1:9.
5 Ibada yetu kwa Yehova si jambo la kidesturi tu, si namna ya ujitoaji kimungu kama ile ya wanaodai kuwa Wakristo katika ulimwengu, bali ni yenye moyo mwepesi, yenye kutenda, na iliyo hai kulingana na ile kweli inayopatikana katika Neno la Mungu.—Yn. 4:23, 24.
6 Azimio letu la kufanya mapenzi ya Mungu laweza kujaribiwa kila siku. Twapaswa kutiwa nguvu kwa kujua kwamba “ndugu zetu walioko duniani” hupatwa na majaribu yaleyale na kwamba ni Yehova atakayetutia nguvu. (1 Pet. 5:9, 10) Hivyo tutaweza kutimiza huduma yetu kikamili wakati wa mwaka wa utumishi wa 1994.—2 Tim. 4:5.