Sanduku La Swali
◼ Je! tupigie Sosaiti simu ili kupata majibu kwa maswali ya Biblia au kupata shauri la kibinafsi?
Watu wengi hutumia simu ili kufanya mambo kwa haraka, lakini mara nyingi mengi kuliko upesi huhusika. Ulimwenguni ni kawaida kutanguliza ustarehe wa kibinafsi; watu huepuka kujikakamua wenyewe.
Ni kinyume kama nini na shauri la Mungu! Yeye hutuhimiza tutafute-tafute maarifa kama vile hazina iliyofichwa, jambo linalodokeza kuwa kwetu na nia ya kujikakamua wenyewe. Ujuzi huthibitisha kwamba kufanya kwetu hivyo kunatokeza uradhi zaidi wenye kudumu.—Mit. 2:1-4.
Jitihada ya jinsi hiyo inafaa ikiwa swali linatokea tunapojitayarisha ili kushiriki katika mikutano au ikiwa tunakabili tatizo la kibinafsi. Badala tu ya kupigia Sosaiti simu, tutanufaika kwa kufanya utafiti kibinafsi katika Biblia na vichapo vyetu, hasa Watch Tower Publications Index, pamoja na faharisi zayo zenye thamani za Maandiko na habari.
Baada ya sisi ‘kuzitafuta-tafuta hazina zilizofichwa,’ tunaweza kumwendea mmoja wa wazee wa kwetu ikiwa tungali twahitaji msaada. Wazee wana maarifa mengi ya Biblia na ujuzi mwingi wa kutafuta-tafuta habari. Msaada wao uliosawazika ungefaa hasa ikiwa tunahitaji shauri juu ya tatizo au uamuzi wa kibinafsi, kwani wako karibu nasi na hali yetu.—Linganisha Matendo 8:30, 31.
Ikiwa bado inaonekana kwamba habari zaidi inahitajiwa moja kwa moja kutoka kwa Sosaiti, kwa kawaida ni afadhali kupeleka barua. Wazee wanaweza kusaidia pia katika kuitayarisha. Barua hiyo itaruhusu kuwe na wakati ili jibu litegemee utafiti au uangalifu wa kutosha, ambao kwa kawaida hauwezekani kwa simu.