Hubiri Njia ya Mungu ya Kuleta Amani na Usalama
1 Wanadamu wamefanya mipango mingi ya kuleta amani na usalama, lakini hakuna mojayapo mipango hiyo inayotimiza mahitaji halisi ya watu ulimwenguni pote. Ingawa chuki za kidini, za kirangi, na za kitaifa, pamoja na kujitakia makuu katika siasa na pupa, vyaonekana kuwa vizuizi vikubwa vya ulimwengu wenye usalama na amani, Wakristo wa kweli wanajua kwamba vizuizi halisi ni Shetani Ibilisi na kukataa kwa mwanadamu kujinyenyekeza kwa Yehova Mungu.—Zab. 127:1; Yer. 8:9; 1 Yoh. 5:19.
2 Katika Januari, tutajitahidi kuwasaidia majirani wetu waone kwamba njia ya Mungu ya kuleta amani na usalama ndiyo njia pekee na kwamba Yehova ana suluhisho kamili kwa matatizo yote ya ainabinadamu.
3 Tumia Trakti Mpya: Twaweza kushiriki ujumbe huo wenye kujenga kwa kutumia zile trakti mpya zilizotolewa kwenye “Wachukuaji Nuru” Mkusanyiko wa Wilaya. Wonyesho sahili ulionyesha namna ya kutumia Trakti Na. 19, Je! Ulimwengu Huu Utaokoka?, ili kuanzisha mazungumzo na kuelekeza kwenye funzo la Biblia. Utimizo wenye kutokeza wa unabii wa Yesu juu ya mwisho wa ulimwengu huu wapasa kukamata uangalifu wa wengi.
4 Mamilioni ya watu leo wameshuka moyo, nao wanatamani wakati wa maponyo na wa amani, usalama, na utulivu wa kweli. Faraja kwa Walioshuka Moyo (Trakti Na. 20) yaweza kuwa chanzo halisi cha kitia-moyo kwa wengi.
5 Trakti Na. 21, Furahia Maisha ya Familia, inaandaa shauri lenye kutumika juu ya yale yanayoweza kufanywa ili kufanyia maendeleo maisha ya familia hata sasa huku tukingojea wakati ujao mzuri ajabu katika ulimwengu mpya wa Mungu.
6 Trakti Na. 22 inatoa jibu la moja kwa moja kwa swali Ni Nani Hasa Anayeutawala Ulimwengu? Inaeleza kwa nini wanadamu wametumia njia zenye kuchukiza sana za kutesana na kuchinjana ijapokuwa tamaa ya watu wengi ya kuwa na maisha yenye amani na usalama. Kuna majeshi maovu ya roho katika mahali pa kimbingu, na udanganyifu wa Shetani wenye hila zaidi umekuwa kuwashawishi wengi waamini kwamba yeye na mashetani wake hawako kikweli.
7 Anzisha Mafunzo ya Biblia: Funzo la Biblia laweza kuanzishwa kwa trakti, broshua, gazeti, au kitabu. Ukipata kujua kwamba mwenye nyumba tayari ana kimojapo vichapo vyetu, mwombe kwa busara kumwonyesha jinsi kinavyoweza kutumiwa katika funzo la Biblia. Zile trakti mpya na ile broshua Je! Kweli Mungu Anatujali? ni vyombo bora kabisa vya kutumiwa katika kuamua kadiri ya kupendezwa kwa mwenye nyumba katika kuanzisha mafunzo ya Biblia. Kwa kuongezea, vichapo vyovyote vilivyochapishwa na Sosaiti katika 1980 au kabla ya hapo vyaweza kutolewa katika utumishi wa shambani wakati watu wanapoonyesha kwa kweli kupendezwa na kweli. Ikiwa kundi lako lina vitabu Maisha ya Jamaa, “Ufalme Wako Uje,” Kweli, au Vijana akibani, panga kuvitumia vizuri katika huduma.
8 Usalama wa kweli waweza kuja tu kutoka Muumba, Yehova Mungu. Tunataka kuwasaidia wengi iwezekanavyo wafungue mioyo na akili zao kwa ile kweli ya Neno la Mungu na kukubali lile tumaini inayowatolea. Na tutumie vizuri ile misaada ya kufundisha tuliyonayo ili kuhubiri njia ya Mungu ya kuleta amani na usalama.—Isa. 2:3, 4.