Sanduku La Swali
◼ Kutumikia kama painia msaidizi kwapasa kuonwaje?
Upainia msaidizi wapasa kuonwa kuwa pendeleo na daraka zito pia. Makumi ya maelfu ya wahubiri kila mwezi huwekwa kutumikia wakiwa mapainia wasaidizi, na wengine hufanya hivyo kwa kuendelea. Twawapongeza wahubiri hao wenye bidii ambao hali zao huwaruhusu kutimiza takwa la saa 60 katika utumishi wa shambani kila mwezi wanapotumikia wakiwa mapainia wasaidizi. Wazee na wengine pia wapaswa kuwatia moyo wahubiri wanaotoa ombi la utumishi wa upainia msaidizi wachukue ahadi yao kwa uzito na waepuke mbetuko wowote wa kuwa na mwelekeo wa kizembe.
Kama vile painia wa kawaida, wale wanaojitolea kuwa mapainia wasaidizi kwa mwezi mmoja au zaidi wanapaswa kwanza kuhesabu gharama. (Lk. 14:28) Hili hutia ndani kuchunguza kimbele ikiwa wanaweza kutazamia ifaavyo kutimiza takwa la saa katika huduma ya shambani bila kupuuza madaraka mengine ya Kikristo. Uamuzi wa mtu wa kujiandikisha awe painia msaidizi wapaswa kufanywa baada ya ufikirio wa sala wa hali zake binafsi. Haupaswi kusukumwa na uchocheo wa hisia-moyo zinazochochewa kwa sababu wengine wanajiandikisha. Unapaswa uwe uamuzi uliofikiriwa vizuri, ukiandamana na ratiba iliyoandikwa ya kutimiza matakwa. Ni jambo la maana kusoma ombi kwa uangalifu na kuamua moyoni mwa mtu mwenyewe kwamba anaweza kuyakubali matakwa kwa moyo mweupe.
Bila shaka, kujitahidi kwahusika. Miezi fulani mwakani hutoa fursa ya ‘kusongwa sana’ na kuhubiri habari njema. (Mdo. 18:5) Hii yatia ndani kipindi cha Ukumbusho cha Machi na Aprili na miezi ambayo mwangalizi wa mzunguko huzuru kundi. Wahubiri wengi hujitia nidhamu kwa moyo kufuata ratiba yenye mkazo ili washiriki zaidi katika kazi ya kuhubiri katika pindi hizi za utendaji wa pekee, wakijua kwamba baraka tele hutokea mara nyingi. (2 Kor. 9:6) Wahubiri wengi hufanya jitihada za pekee ili wafanye upainia wakati wa miezi ya likizo na mwezi wowote ulio na miisho-juma mitano kamili. Lakini wanapojiandikisha, wanajua uhitaji wa kufuata ile kanuni ya ‘Ndiyo yako iwe Ndiyo’ kwa kufanya yote wawezayo kuripoti saa 60 au zaidi kila mwezi watumikiapo wakiwa mapainia wasaidizi.—Mt. 5:37.
Wahubiri ambao huenda wasiweze kufanya upainia wanaweza kusaidia kwa kujitoa wenyewe kufanya kazi pamoja na mapainia wasaidizi, wakifanya mipango hususa pamoja nao. Ni jambo la msaada kubaki kwa muda mrefu zaidi shambani pamoja na mapainia inapowezekana. Huenda mapainia wakathamini hasa kuungwa mkono asubuhi mapema, baadaye alasiri, au saa za mapema za jioni. Mapainia wasaidizi wanapendezwa kualikwa kufanya kazi na wengine katika kufanya ziara za kurudia na kuanzisha mafunzo ya Biblia nyumbani. Wale wanaoweza kuwaunga mkono mapainia wasaidizi bila shaka watavuna furaha nyingi zaidi inayotokana na kutoa.—Mdo. 20:35.
Jitihada kwa upande wa mapainia wengi wasaidizi inathaminiwa sana. Wale wanaoweza kujiunga nao wanaweza kutazamia baraka tele. (Mit. 10:4) Unaweza kushiriki wakati gani mwingine katika shangwe za utendaji ulioongezwa ukiwa painia msaidizi?