Wasaidie Wachukue Hatua ya Kutenda Kulingana na Ujumbe
1 Kazi yetu ya kuhubiri huwapa watu fursa ya ‘kusikia maneno ya unabii wa Ufunuo.’ (Ufu. 1:3) Lakini ikiwa wataokoka “dhiki ile iliyo kuu,” ni lazima wachukue hatua ya kutenda kulingana nayo. (Ufu. 7:14) Maisha yanahusika! Kwa hiyo hakikisha umerudia wale walioonyesha kupendezwa mara ya kwanza katika mojawapo utoaji uliotumia mwezi huu.
2 Ikiwa uliacha kitabu “Upeo wa Ufunuo,” unaweza kusema:
◼ “Nimefurahi kukuona tena. Tulipoongea wakati uliopita, tulizungumza juu ya mojawapo unabii wa kitabu cha Ufunuo, nami nilikuachia kichapo kinachoueleza. Labda uligundua kwamba ingawa kitabu cha Ufunuo kina mambo ya ndani sana, chaweza kueleweka kwa kufikiria matukio ya ki-siku-hizi kwa kutumia baadhi ya kweli za msingi za Biblia. Ningependa kutumia dakika chache kukuonyesha mambo machache ambayo Biblia hutuambia juu ya nyakati zetu.” Kisha geukia kichapo kinachofaa ambacho unaweza kutumia kuanzisha funzo la Biblia nyumbani.
3 Ikiwa uliacha trakti “Je! Ulimwengu Huu Utaokoka?” wakati wa ziara ya kwanza, unaweza kusema hivi:
◼ “Nimefurahi kukupata nyumbani leo. Nilipokutembelea hivi karibuni, tulizungumza juu ya matukio yanayofanyiza ishara ambayo ingetokea mara kabla ya mwisho wa ulimwengu. [Pitia sehemu zifaazo za ile ishara ya Mathayo 24:3-14.] Je! umeona tukio lolote ambalo limetokea ulimwenguni au katika jumuiya yetu hivi karibuni ambalo wafikiri laweza kuwa utimizo wa sehemu ya ishara hiyo?” Ukitumia vielezi katika sura ya 16 ya kitabu Upeo wa Ufunuo, eleza juu ya utimizo wa baadhi ya unabii huo mbalimbali wa Biblia. Mwishoni mwa ziara, taja kichwa cha hotuba ya watu wote ya juma hilo, na umkaribishe aende nawe kwenye Jumba la Ufalme.
4 Ikiwa ulimkaribisha mwenye nyumba kwenye Ukumbusho, sema:
◼ “Nilipokutembelea wakati uliopita, tulizungumza juu ya jinsi kifo cha Yesu ni cha maana kwa wanadamu. Pia nilikualika uhudhurie Ukumbusho wa kifo chake, utakaoadhimishwa na Wakristo ulimwenguni pote mnamo Machi 26. Leo nimekuja kukukumbusha kwamba unakaribishwa kwenye tukio hilo la maana. [Mwambie wakati na mahali pa mwadhimisho.] Huenda ikakusaidia kuthamini umaana wa pindi hiyo tukipitia baadhi ya baraka ambazo twafurahia sasa kutokana na yale ambayo Yesu alifanyia wanadamu, pamoja na baraka zitakazokuja bado.” Kisha jitahidi kuzungumzia mambo yafaayo kutoka mojayapo magazeti ya karibuni au kutoka sura ya 41 ya kitabu Upeo wa Ufunuo. Pia waweza kuonyesha vielezi vilivyo kwenye kurasa 294, 299, na 308. Ikiwezekana, fanya mipango ya kusaidia mwenye kupendezwa ahudhurie Ukumbusho.
5 Ikiwa mtu alikuwa msikilizaji mzuri tu, jambo hili laweza kuwa na matokeo:
◼ “Nilifurahia sana mazungumzo yetu ya karibuni juu ya Biblia. Nimerudi kwa sababu ningependa kuona ukifurahia yale ambayo Mungu ameahidi kwa wale wanaotaka kujifunza zaidi kuhusu yeye.” Soma Yohana 17:3, kisha rejezea trakti Uzima Katika Ulimwengu Mpya Wenye Amani.
6 Kupenda kwako uhai na kuthamini kwako fidia na kukusukume ufanye ziara za kurudia kwa wenye kupendezwa. Wasaidie wachukue hatua ya kutenda kulingana na ujumbe wenye kusisimua uliomo katika Ufunuo. Kumbuka kwamba, “wakati u karibu”!—Ufu. 1:3.