Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!
1 “Mwenye furaha ni yeye anayesoma kwa sauti na wale wanaosikia maneno ya unabii huu, na wanaoshika mambo yaliyoandikwa humo; kwa maana wakati uliowekwa uko karibu.” (Ufu. 1:3) Maneno hayo hukazia umuhimu wa kitabu cha Ufunuo, hasa kwa sababu tunaishi katika wakati uliowekwa wa kutimizwa kwa unabii wake mwingi. Basi inafaa kwamba tutaanza kujifunza kitabu Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu! katika Funzo la Kitabu la Kutaniko kuanzia juma la Januari 8, 2007.
2 Tangu tuliposoma kitabu Upeo wa Ufunuo katika Funzo la Kitabu la Kutaniko, tamasha ya ulimwengu imebadilika katika njia nyingi sana. (1 Kor. 7:31) Isitoshe, wengi ambao wamejiunga katika kuhubiri habari njema za Ufalme hawajawahi kunufaika na uchunguzi wa mstari kwa mstari wa kitabu cha Ufunuo. Kujifunza kitabu Upeo wa Ufunuo kunapaswa kutusaidia kudumu tukiwa macho kuhusu mambo ya wakati ujao.—Ufu. 16:15.
3 Azimia kuhudhuria Funzo la Kitabu kila juma. Habari hiyo itatusaidia kuwa macho, nao ujumbe wa Yesu kwa makutaniko saba utatusaidia kuepuka mambo yanayoweza kuathiri sana hali yetu ya kiroho na kushiriki kwetu katika huduma.—Ufu. 1:11, 19.
4 Jitayarishe Vizuri: Kabla ya kila funzo la kitabu, soma mistari ya kitabu cha Ufunuo ambayo itazungumziwa. Fikiria maelezo ya Kimaandiko yanayofafanua mistari hiyo. Jaribu kuelewa mambo muhimu ili moyo wako uchochewe. (Neh. 8:8, 12) Tumia muda fulani utafakari na kujiuliza: ‘Jambo hili linanionyesha nini kuhusu Yehova na kutekelezwa kwa kusudi lake? Ninaweza kutendaje kupatana na kusudi lake na kuwasaidia wengine?’
5 Miaka 92 imepita tangu “siku ya Bwana” ianze katika mwaka wa 1914. (Ufu. 1:10) Matukio yenye kusisimua yaliyotabiriwa katika kitabu cha Ufunuo yatatukia hivi karibuni. Kujifunza kitabu Upeo wa Ufunuo kutaburudisha mioyo na akili zetu na kuimarisha imani yetu kwamba “vita vya ile siku kuu ya Mungu Mweza-Yote” na ulimwengu mpya umekaribia.—Ufu. 16:14; 21:4, 5.