Mnara wa Mlinzi na Amkeni! —Majarida Yenye Kweli
1 Toleo la Mnara wa Mlinzi la Januari 1, 1994, ukurasa 22, lilitukumbusha kwamba magazeti yetu huchapisha “makala za wakati ufaao ambazo zimeshughulikia mahitaji halisi ya watu.” Twataka kuyagawa majarida haya kotekote. Katika miezi ya Aprili na Mei, Mnara wa Mlinzi na Amkeni! ndiyo yatakayotolewa.
2 Kazi ya nyumba kwa nyumba hutupa sisi fursa nzuri kabisa ya kuangusha magazeti haya. Ushahidi wa vivi-hivi na ziara za kurudia zenye matokeo hutokeza pia kuangushwa kwa magazeti haya kwa kawaida. Vilevile kufanya ushahidi wa barabarani na kutembelea majengo ya biashara katika eneo letu ni njia zenye matokeo za kuongeza ugawaji wa magazeti.
3 Habari za Kuzungumzia: Toleo la Mnara wa Mlinzi la Aprili 1 lazungumzia habari “Ulimwengu Bora Zaidi—Je! Ni Ndoto Tu?” na “Ulimwengu Bora Zaidi—U Karibu!” Hilo kwa hakika lapatana na kusudi la gazeti hilo la kutangaza Ufalme wa Mungu. Makala ya pili yamalizia kwa kuonyesha jinsi paradiso ya milele itakavyokuwa jambo halisi chini ya utawala wa Kristo Yesu.—Lk. 23:43.
4 “Waweza Kupata Wapi Mwongozo Wenye Kutumainika?” ndilo swali linalozungumziwa katika toleo la Aprili 15. Matoleo ya Mei yatazungumzia habari hiyo zaidi katika makala “Je! Dini Inatosheleza Mahitaji Yako?” na “Kwa Nini Uisome Biblia?” Twapaswa kuweza kuanzisha mazungumzo kwa urahisi pamoja na watu juu ya habari hizi za wakati ufaao.
5 Kuangusha Mengi Zaidi: Mnara wa Mlinzi la Januari 1 lilitoa madokezo manne juu ya jinsi ya kuangusha magazeti mengi zaidi. Tulitiwa moyo (1) kuwa wenye utambuzi juu ya magazeti. Tunapoyasoma, twapaswa kufikiria ni makala zipi ziwezazo kuwavutia zaidi watu katika eneo letu. Pia, tukibeba nakala kadhaa kwa kawaida, huenda tukaweza kuziangusha kwa wafanyakazi wenzetu, majirani, walimu, wanafunzi wenzetu, au wale wanaonunua vitu dukani.
6 Tulikumbushwa (2) kufanya utoaji wetu uwe sahili. Chagua jambo moja lenye kupendeza, na ulieleze kwa maneno machache. Ikiwa huwezi kumsadikisha mwenye nyumba akubali gazeti, hilo laweza “kusema” na mtu uliyekutana naye au na wengine nyumbani.
7 Uhitaji mwingine ni (3) kuwa mwenye kunyumbulika. Ni vizuri kufikiria makala tofauti-tofauti za kuzungumzia—moja kwa ajili ya vijana, nyingine kwa ajili ya wanaume, na jambo jingine kwa ajili ya wanawake.
8 La mwisho, twahitaji (4) kuweka mradi wa kibinafsi wa kuangusha magazeti. Ingawa kutaniko haliwezi kuweka idadi ya magazeti yapaswayo kuangushwa na kila mtu, sisi mmoja-mmoja twaweza kujiwekea mradi. Hilo laweza kutupa sisi kichocheo zaidi cha kuwa wenye idili katika kutoa magazeti. Tukitoa agizo la kupata idadi fulani ya magazeti sikuzote, huenda tukachochewa kuangusha mengi zaidi.
9 Twataka wengine wajue juu ya Ufalme wa Mungu. Acheni tupate faida kamili kutokana na ule msaada mzuri ambao magazeti huandaa katika kueneza ujumbe wa Ufalme.—Mt. 10:7.