Sanduku La Swali
◼ Twaweza kutoaje maelezo kwa njia yenye matokeo zaidi mikutanoni?
Sisi hutazamia kwa hamu nyingi kukusanyika pamoja kwenye mikutano ya kutaniko ya kila juma. Huko sisi huwa na fursa ya kuonyesha imani yetu na kutia wengine moyo kwa kutoa kwetu maelezo. (Mit. 20:15; Ebr. 10:23, 24) Twapaswa kuona kutoa maelezo kukiwa pendeleo na tujitahidi kushiriki kwa ukawaida. Twaweza kufanyaje hivi kwa matokeo zaidi?
Utayarishaji ni hatua ya kwanza. Kusoma na kutafakari habari hiyo mapema ni kwa maana. Jaribu kupata maana halisi ya lile linalosemwa. Ingawa huenda mada ilizungumziwa wakati uliopita, tafuta mambo yoyote yaliyotiliwa mkazo au yaliyoongezwa yanayosemwa. Weka akilini kichwa cha habari yote. Unapotayarisha maelezo kutoka kichapo kinachokazia funzo lenye kina kirefu la kitabu cha Biblia, kama vile kitabu Ufunuo Upeo, jaribu kuona jinsi mstari hususa unavyohusiana na mistari inayouzunguka. Kufuata madokezo haya kutachochea uwezo wako wa kufikiri. Kutakusaidia utayarishe maelezo mazuri na upate shangwe katika kushiriki kwako.
Maelezo bora zaidi ni mafupi, yenye kuelezwa kwa usahili, na yanategemea kichapo cha funzo. Mtoa-maelezo wa kwanza apaswa kujibu swali moja kwa moja, akiacha mambo mengine kwa maelezo ya ziada. Epuka maelezo marefu, yasiyo na lengo yanayochukua wakati mwingi zaidi na kuzuia wengine kushiriki. Jieleze kwa maneno yako mwenyewe, badala ya kusoma elezo lako neno kwa neno kutoka kichapo. Maelezo ya ziada yanaweza kutia ndani mambo yaliyo kwenye Maandiko yaliyowekwa bila manukuu. Sikiliza kwa uangalifu yale wanayosema wengine ili kwamba uepuke kurudia-rudia kusiko kwa lazima.
Ni vema kunyoosha mkono wako mara kadhaa lakini si kwa kila fungu. Twakaribisha wachanga washiriki kutoa maelezo. Ikiwa unasitasita kutoa maelezo, unaweza kumjulisha kiongozi ajue mapema fungu utakalopenda kutoa maelezo, na yaelekea ataweza kukupatia fursa ya kufanya hivyo.
Sisi sote twapaswa kuwa na jitihada nyingi za kuwa na jambo la kushiriki kwenye mikutano ya kutaniko linalohusisha ushiriki wa wasikilizaji. Kumbuka, mafanikio ya mikutano kama hiyo hutegemea kwa kadiri kubwa nia yetu na kuwa na matokeo katika kutoa maelezo.—Zab. 26:12.