Kuhudhuria Mikutano kwa Ukawaida—Muhimu kwa Kusimama Kwetu Imara
1 Mtume Paulo alituhimiza tuendelee tukiwa “wazima katika imani.” (Tito 1:9, 13) Kwenye mikutano ya kutaniko sisi huzungumza juu ya mawazo yenye kujenga na tunaagizwa juu ya jinsi ya kuendelea tukiwa tumevaa kikamili silaha za kiroho ili tuweze “kusimama imara dhidi ya mbinu za Ibilisi.”—Efe. 6:11, NW; Flp. 4:8.
2 Mikutano Huandaa Kile Tunachohitaji: Kuhudhuria mikutano ya kutaniko kwa ukawaida ni muhimu kwa kusimama kwetu imara. (1 Kor. 16:13) Kwenye mikutano sala zinatolewa kumshukuru na kumsifu Mungu, na pia kumwomba dua kwa niaba ya kutaniko na mahitaji yalo. (Flp. 4:6, 7) Kujiunga katika nyimbo za Ufalme hutuimarisha na kutuwezesha kueleza maoni na hisia zetu tunapomwabudu Yehova. (Efe. 5:19, 20) Ushirika wetu pamoja kwenye Jumba la Ufalme kabla na baada ya mikutano hututia moyo, hutujenga, na kutuburudisha.—1 The. 5:11.
3 Aprili uliopita hotuba ya pekee, “Mwisho wa Dini Bandia U Karibu,” ilikazia sana akilini mwa wapendao kweli uharaka wa kuchukua hatua ya mara moja ya kutoka katika Babiloni Mkubwa. (Ufu. 18:4) Ilisisimua kama nini kuzungumza zile makala tatu za funzo za Mnara wa Mlinzi juu ya mimweko ya nuru ambayo imetia nuru kijia cha waadilifu! (Mit. 4:18) Fikiria kile ambacho tungalikosa ikiwa tungalipuuza kuhudhuria mikutano hiyo.
4 “Wasifaji Wenye Shangwe” Mkusanyiko wa Wilaya wetu, utakazia uhitaji wa elimu inayoongezea ubora wa huduma yetu. Kama vile kitabu chetu Tumefanywa Tengenezo Tutimize Huduma Yetu kionyeshavyo kwenye ukurasa 72, Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ni uandalizi kwa ajili ya elimu yenye kuendelea ya kutaniko zima. Kwa sasa, sehemu moja ya programu hiyo ya Kiingereza hutusaidia tufahamu vizuri zaidi historia ya tengenezo ya siku ya kisasa kwa kutumia kitabu Proclaimers. Hatuwezi kukubali kukosa fursa ya kupokea elimu hiyo.
5 Mkutano wa Utumishi wetu hututayarisha kuwa wenye matokeo zaidi katika huduma. Jambo hili lilitolewa kielezi na mkutano ambao katika huo tulipokea maagizo ya kushiriki katika ugawaji mpana wa trakti Habari za Ufalme Na. 34. Baraka za Yehova juu ya kazi hiyo zilikuwa nyingi, kama vile ilivyoonwa katika matokeo yasiyo na kifani ulimwenguni pote. (Linganisha 2 Wakorintho 9:6, 7.) Wale ambao huhudhuria mikutano kwa ukawaida walitiwa moyo, nao wakasaidia kutokeza ule utegemezo uliopewa kampeni hiyo.
6 Kwenye Funzo la Kitabu la Kutaniko, hisi yetu ya uharaka inazidishwa na mambo tunayojifunza kutoka katika Neno la Mungu kwa msaada wa kitabu Upeo wa Ufunuo. Mambo yakiwa yanasonga kasi katika mandhari ya ulimwengu, sisi twahitaji kuelewa utimizo wa unabii mbalimbali wenye kina zaidi wa Ufunuo.
7 Weka Kuhudhuria Mikutano kwa Ukawaida Katika Mahali pa Kwanza: Katika nchi nyingi ambamo ndugu zetu wanapatwa na majaribu, wao bado hutambua jinsi ilivyo muhimu kwao kukutana kila juma. Kwa kielelezo, katika Burundi, Rwanda, Liberia, na Bosnia na Herzegovina, watu wapya wengi sana wanahudhuria mikutano hivi kwamba wale wanaohudhuria huzidi idadi ya wahubiri mara mbili au tatu. Katika njia hii Yehova husaidia akina ndugu waendelee wakiwa imara katika roho moja.—Flp. 1:27; Ebr. 10:23-25.
8 Wowote ambao huenda wakawa wamepuuza kuhudhuria mikutano kwa ukawaida wapaswa kuchukua hatua sasa ili kurekebisha mwelekeo huu. (Mhu. 4:9-12) Ili tusimame imara, twahitaji kule kutiana moyo pamoja na watu wakomavu, kunavyoandaliwa kwa kuhudhuria mikutano kwa ukawaida.—Rum. 1:11.