Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • km 10/96 kur. 7-10
  • “Wajumbe wa Amani ya Kimungu” Mkusanyiko wa Wilaya wa 1996

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Wajumbe wa Amani ya Kimungu” Mkusanyiko wa Wilaya wa 1996
  • Huduma Yetu ya Ufalme—1996
  • Habari Zinazolingana
  • “Imani Katika Neno la Mungu” Mkusanyiko wa Wilaya wa 1997
    Huduma Yetu ya Ufalme—1997
  • “Wasifaji Wenye Shangwe” Mkusanyiko wa Wilaya wa 1995
    Huduma Yetu ya Ufalme—1995
  • “Njia ya Mungu ya Maisha” Mkusanyiko wa Wilaya na wa Kimataifa wa 1998
    Huduma Yetu ya Ufalme—1998
  • “Hofu ya Kimungu” Mkusanyiko wa Wilaya wa 1994
    Huduma Yetu ya Ufalme—1994
Pata Habari Zaidi
Huduma Yetu ya Ufalme—1996
km 10/96 kur. 7-10

“Wajumbe wa Amani ya Kimungu” Mkusanyiko wa Wilaya wa 1996

1 Programu ya mkusanyiko wa wilaya mwaka huu kwa kweli itatusaidia kudumisha amani yetu ya kimungu, na itaeleza daraka letu katika kusaidia wengine wapate amani hiyo. Kama ilivyotangazwa, kichwa kitakuwa “Wajumbe wa Amani ya Kimungu.” Je, umefanya mipango ili usikose sehemu yoyote ya programu?

2 Programu ya Siku Tatu: Twajua mtafurahia sana mkusanyiko wa mwaka huu na mtarudi nyumbani mkiwa na nguvu iliyofanywa upya. (2 Nya. 7:10) Mwaka huu tena tutakuwa na programu ya siku tatu. Je, tayari umefanya mipango upate ruhusa kutoka kazi ya kuajiriwa ili uweze kuhudhuria kipindi chote? Baadhi ya mikusanyiko huenda itafanywa kabla shule hazijafungwa. Ikiwa una watoto wa umri wa kwenda shule, je, umejulisha walimu wao kwa heshima kwamba hawatakuwako Ijumaa kwa sababu ya sehemu hii muhimu ya mafundisho yao ya kidini?

3 Huduma ya Ufalme Yetu ya Mei 1996, yaorodhesha tarehe na mahali pa mikusanyiko yote ya Afrika Mashariki na Rwanda. Kufikia sasa mwandishi wa kutaniko lenu amewajulisha lile ambalo mmegawiwa. Zaidi ya Kiingereza, kutakuwa na mikusanyiko katika Kiganda, Kinyarwanda, na Kiswahili, na lugha ya Ishara ya Kimarekani.

4 Programu itaanza saa 3:30 asubuhi sikuzote na kumalizika Jumapili saa 10:00 hivi alasiri. Milango itafunguliwa saa 2:00 asubuhi. Wale watakaoruhusiwa kuingia kabla ya wakati huo ni wale walio na migawo ya kazi, nao hawataruhusiwa kuhifadhi viti hadi jengo lifunguliwe kila mtu. Je, tutaonyesha fadhili kwa ndugu zetu wazee-wazee na wagonjwa kwa kuacha wazi viti vinavyofaa na vyenye starehe? Kumbuka: “upendo . . . hautafuti mambo yake.”—1 Kor. 13:4, 5; Flp. 2:4.

5 Je, Utanolewa?: Baada ya kunukuu Mithali 27:17, “Chuma hunoa chuma,” Mnara wa Mlinzi la Agosti 15, 1993, lilisema: “Sisi ni kama vyombo vinavyohitaji kunolewa kwa ukawaida. Kwa kuwa kuonyesha upendo kwa Yehova na kufanya maamuzi yenye msingi wa imani yetu kunamaanisha kuwa tofauti na ulimwengu, tunahitaji daima kufuata mwendo ulio tofauti na ule unaofuatwa na wengi.” Twaweza kutumiaje shauri hilo?

6 Sisi ni tofauti na ulimwengu na lazima tudumu tukiwa tofauti nao. Jitihada ya daima ya kutimiza hili yapaswa kudumishwa ikiwa tutakuwa wenye bidii katika matendo mema. (Tito 2:14) Hiyo ndiyo sababu makala ya Mnara wa Mlinzi iliyonukuliwa hapo juu iliendelea kusema: “Tunapokuwa na wengine wanaompenda Yehova, tunanoana—tunahimizana katika upendo na kazi nzuri.” Mkusanyiko wa Wilaya ni mojapo maandalizi kutoka kwa Yehova ya kutusaidia tudumu tukiwa makini kiroho. Hatuwezi kukosa sehemu yoyote ya programu.

7 Mtu Mwenye Hekima Atasikiliza: Kusikiliza ni ufundi ambao ni lazima usitawishwe. Imesemwa kwamba mtu wa kawaida hukumbuka karibu nusu tu ya yale ambayo amesikia—hata iwe anafikiri amesikiliza kwa uangalifu kadiri gani. Kwa kuwa twaishi katika kizazi cha vikengeusha-fikira, wakati mwingine huenda tukapata ugumu wa kukaza fikira kwa vipindi virefu. Je, twaweza kujaribu kuongeza urefu wetu wa kukazia uangalifu, hasa tunapoketi miongoni mwa wahudhuriaji wengi tukisikiliza mtu anayesema? Ikiwa ungeulizwa utoe muhtasari wa programu ya kila siku baada ya kurudi nyumbani kutoka mkusanyikoni, je, ungeweza kufanya hivyo? Sisi sote twawezaje kuongeza uwezo wetu wa kusikiliza na kukazia uangalifu sana kila sehemu inayotolewa kwenye programu ya mkusanyiko?

8 Kupendezwa sana ni muhimu, kwa kuwa zawadi ya kimungu ya kumbukumbu haiwezi kutumika vizuri bila kupendezwa huko. Kwa kielelezo, kadiri mtu aonyeshavyo kupendezwa sana katika habari fulani, ndivyo iwavyo rahisi kukumbuka mambo makuu ya hotuba au sehemu ya mkusanyiko. Hata hivyo, mengi hutegemea kukazia uangalifu zaidi kuliko ilivyo kawaida mambo tuliyo na pendeleo la kuyasikia kwenye mikusanyiko ya wilaya. Kupendezwa kwetu sana na kusikiliza kwa makini kila sehemu ya programu ya mkusanyiko kunatimiza fungu katika hali yetu ya sasa ya kiroho na vilevile katika matazamio yetu ya wakati ujao. Kwenye mikusanyiko twafundishwa njia za Yehova na twapewa maagizo ya kutimiza kazi ya kuokoa uhai. (1 Tim. 4:16) Jiwazie ukiwa meli inayoelea kwenye bahari yenye dhoruba. Ahadi za Yehova ni nanga imara ya tumaini. Mtu asiposikiliza kwa makini kwenye programu za Kikristo na aruhusu akili yake iyumbeyumbe, huenda akakosa mambo muhimu ya shauri na fundisho ambalo lingemzuia kuvunjikiwa merikebu kiroho.—Ebr. 2:1; 6:19.

9 Katika sehemu nyingi za ulimwengu, ndugu zetu hufanya jitihada nyingi sana kuhudhuria mikutano. Inapendeza sana kuona wakikazia uangalifu mwingi kwenye mikusanyiko. Ingawa hivyo, mahali pengine, watu mmoja-mmoja wamekengeusha wengine kwa kuzunguka-zunguka mahali pa mkusanyiko programu inapoendelea. Wengine huchelewa. Kwenye mikusanyiko mingine iliyopita, ilikuwa vigumu kusikiliza dakika chache za kwanza za programu kwa sababu ya watu wengi waliokuwa wakizunguka katika vijia na nyuma ya sehemu za viti. Hawa kwa kawaida si akina ndugu walio na migawo ya kazi au akina mama wanaoshughulikia mahitaji ya watoto wao wadogo. Usumbufu mwingi hutoka kwa watu wanaopiga gumzo tu. Mwaka huu Idara ya Ukaribishaji itatoa uangalifu zaidi kwa tatizo hilo, na yatumainiwa kwamba, wote watakuwa wameketi wakati mwenyekiti atukaribishapo sote kufanya hivyo. Ushirikiano wako upande huu utathaminiwa sana.

10 Ni madokezo gani yenye kutumika yatakayotusaidia tuwe wasikivu zaidi kwa programu ya mkusanyiko na kukumbuka mengi yanayotolewa? Yaliyosemwa miaka iliyopita ni ya muhimu kurudia: (a) Kazia fikira sababu kuu ya kwenda kwenye jiji la mkusanyiko. Si kujiingiza katika tafrija, bali ni kusikiliza na kujifunza. (Kum. 31:12) Jaribu kupata usingizi wa kutosha kila usiku. Ukija mkusanyikoni ukiwa umechoka sana, kukaza fikira kutakuwa kugumu. (b) Jipe wakati wa kutosha wa kuegesha gari lako na kuketi kabla programu haijaanza. Kukimbilia viti dakika ya mwisho mara nyingi kutatokeza kukosa sehemu fulani ya kufungua. (c) Andika maandishi mafupi ya mambo makuu. Kuandika maandishi mengi kwaweza kuzuia kusikiliza kuzuri. Unapoandika, hakikisha kwamba hukosi mambo mengine kwa sababu ya kukazia fikira maandishi yako. (d) Sehemu ya mkusanyiko inapotolewa utangulizi, uitazamie sana. Jiulize, ‘Naweza kujifunza nini kutokana na sehemu hii ambacho kitaongeza uthamini wangu na upendo wangu kwa Yehova? Habari hiyo yaweza kunisaidiaje kuonyesha utu mpya zaidi? Jambo hili litanisaidiaje kufanya maendeleo katika huduma yangu?’

11 Mwenendo Unaopamba Huduma Yetu: Paulo alimtia moyo Tito ajionyeshe kuwa “kielelezo cha matendo mema.” Kwa kutokuwa mfisadi katika mafundisho yake, Tito angesaidia wengine “wayapambe mafundisho ya Mwokozi wetu Mungu katika mambo yote.” (Tito 2:7, 10) Kila mwaka, sisi hupokea vikumbusha vyenye fadhili juu ya sababu mwenendo wa kimungu ni wa maana tunaposafiri kwenda na kutoka mkusanyikoni, pia tunapokuwa kwenye hoteli na mikahawa na kwenye mkusanyiko wenyewe. Mwaka uliopita tulisikia tena maelezo yenye kuchangamsha ambayo humtukuza Mungu.

12 Ijapokuwa utumishi wa chakula umeondolewa kwenye mikusanyiko yetu, bado kuna gharama kubwa zinazohusika katika kukodisha majengo, kuandaa maegesho, na kutunza mambo mbalimbali. Upaji wetu wa hiari hutunza gharama hizi. Dada mmoja mwenye watoto wake matineja alikuja kwenye mkusanyiko na fedha chache. Hata hivyo, yeye na watoto walisaidia kutoa mchango kidogo. Kile ambacho mtu anaamua kufanya kuhusu hili ni jambo la kibinafsi, lakini twajua mnathamini vikumbusha hivyo.—Mdo. 20:35; 2 Kor. 9:7.

13 Twatambuliwa kwa Jinsi Tunavyovalia: Jinsi tunavyovalia huonyesha mengi zaidi kutuhusu na juu ya hisia zetu kuelekea wengine. Matineja walio wengi na watu wazima wanazungukwa na mitindo ya mavazi ya kiholelaholela shuleni au kazini mwao. Kila mwaka mitindo ya mavazi huzidi kupita kiasi, hata huwa yenye kushtua. Tusipokuwa waangalifu, huenda tukashawishiwa kwa urahisi na marika wa kilimwengu kuvalia kama wao. Mitindo mingi haifai kuvaliwa kwenye mikutano ya ibada. Barua iliyopokewa baada ya mojapo mikusanyiko ya mwaka jana ilionyesha uthamini kwa programu lakini ikaongezea: “Nilishangaa kwa nini kulikuwa na wasichana wengi wachanga waliovalia nguo fupi hivyo, blauzi zenye mikato ya chini sana, na skati zenye mipasuo mirefu.” Kwa hakika sisi sote twataka kuvaa kwa njia inayofaa wahudumu Wakristo kwenye mkusanyiko na tunaposhirikiana baada ya programu. Nyakati zote inafaa kufikiria shauri la mtume Paulo kwa Wakristo la kujipamba “kwa mavazi ya kujisitiri, pamoja na adabu nzuri, na moyo wa kiasi.”—1 Tim. 2:9.

14 Ni nani apaswaye kuamua mavazi ya kiasi, “ya kujisitiri”? Kuwa mwenye kiasi humaanisha kutokuwa “wagumu au wenye kujidai.” Pia kamusi hufafanua kiasi kuwa “kutojivuna.” Wala Sosaiti wala wazee hawapaswi kuweka sheria juu ya mavazi au kujipamba. Hata hivyo, je, haipasi kuwa wazi kwa Mkristo ni mitindo gani ya mavazi isiyo yenye kiasi au isiyofaa? (Linganisha Wafilipi 1:10.) Kujipamba kwetu na kuvalia kwetu hakupaswi kuvutia uangalifu usiofaa. Lazima tupendeze katika sura yetu, si kuwa wa kilimwengu au wenye kuudhi. Tukiwa wahudumu wa habari njema, kuvalia na kujipamba kwetu vizuri tunapokuwa katika jiji la mkusanyiko humletea Yehova heshima na huletea tengenezo lake sifa nzuri. Hivyo, wazazi wataweka kielelezo na kuhakikisha watoto wao wanavalia vizuri kwa pindi hiyo. Wazee watataka kuweka kielelezo chema na kuwa tayari kutoa shauri la fadhili ikiwa lazima.

15 Kamera, Vidiokamera, na Virekodio vya Kaseti: Inaruhusiwa kutumia kamera na vifaa vinginevyo vya kurekodi, mradi tu tuonyeshe ufikirio kwa wengine katika hudhurio. Tukizunguka-zunguka tukipiga picha wakati wa vipindi, tutawakengeusha fikira wengine wanaojaribu kusikiliza na pia tutakosa sehemu ya programu hiyo sisi wenyewe. Kwa kawaida sisi hunufaika na mkusanyiko zaidi tunaposikiliza wasemaji kwa makini na kuandika maandishi machache. Huenda ikawa tunamrekodia ndugu au dada ambaye ni mgonjwa; hata hivyo, kwa manufaa yetu wenyewe, huenda tukapata kwamba tunaporudi nyumbani baada ya kurekodi saa nyingi za programu hiyo, hakutakuwa na wakati wa kupitia mengi ya yale tuliyorekodi. Vifaa vya aina yoyote vya kurekodi havipaswi kuunganishwa kwenye mifumo ya umeme au ya sauti, wala vifaa havipaswi kufunga vijia vya kupitia, au kuzuia wengine kuona.

16 Viti: Twaendelea kuona maendeleo katika habari ya kuhifadhi viti. Mwaka jana, wengi wenu mlifuata mielekezo hii: VITI VYAWEZA KUHIFADHIWA TU KWA WASHIRIKI WA KARIBU WA FAMILIA YAKO NA WOWOTE AMBAO HUENDA WAKAWA WANASAFIRI PAMOJA NAWE KATIKA GARI LAKO. Labda mliona kwamba halitokezi mkazo sana kwa sababu mlifuata mielekezo hii iliyo wazi. Hata la maana zaidi, kukubali kwenu kulimpendeza Yehova na ‘mtumwa mwaminifu,’ ambaye hutoa chakula cha kiroho.—Mt. 24:45.

17 Kuna idadi yenye kuongezeka ya ndugu zetu walio na mahitaji ya pekee. Wengine huja kwa viti vya magurudumu nao wanahitaji utunzi wa washiriki wa familia. Wengine wanapata matibabu mbalimbali kwa magonjwa ya kudumu kama vile matatizo ya moyo au kifafa. Kwa kweli huchangamsha mioyo yetu kuona ndugu na dada zetu wapendwa kwenye mkusanyiko, wakiwa wameazimia kutokosa chakula chochote cha kiroho. Hata hivyo, nyakati nyingine, kumekuwa na tatizo la watu fulani kuwa wagonjwa wakati wa mkusanyiko, wakiwa bila washiriki wa familia au kutaniko wa kuwapa msaada. Katika visa fulani wasimamizi wa mkusanyiko walihitajika kuita utumishi wa dharura wa kitiba kusafirisha ndugu au dada hospitalini. Daraka la utunzi wa wale walio na magonjwa ya kudumu lapaswa kuwa la washiriki wa familia na watu wa ukoo wa karibu. Idara ya Mkusanyiko ya Msaada wa Kwanza haiwezi kuandaa utunzi kwa wale walio na magonjwa hayo ya kudumu. Ikiwa mshiriki wa familia yako anahitaji utunzi wa pekee, tafadhali hakikisha kwamba haachwi peke yake dharura itokeapo. Kwa kuongezea, hakutakuwa na mipango kwenye mikusanyiko ya mahali pa kulala pa pekee kwa wale walio na mizio inayowazuia kuketi sehemu za kawaida za kukaa. Wazee watataka kuwa chonjo kwa wowote katika kutaniko lao walio na mahitaji ya pekee ya kiafya na kuhakikisha mipango imefanywa kabla ya mkusanyiko kwa ajili ya utunzi wao.

18 Mahitaji ya Chakula ya Mkusanyiko: Maelezo mengi yanayofaa yametolewa kuhusu manufaa za kuleta chakula chetu wenyewe. Ndugu mmoja aliandika hivi: “Naweza kuona waziwazi faida kubwa ya kiroho. Wakati huo wote na nishati zaweza kutumiwa sasa kwa mambo ya kiroho. Sijasikia elezo hata moja lisilofaa.” Dada mmoja aliandika hivi: “Kwa kielelezo mnachotoa, nyinyi ndugu wapendwa hututia moyo tukiwa Wakristo mmoja-mmoja tujichunguze wenyewe na kutafuta njia za kurahisisha maisha zetu na kuongeza utendaji wetu wa kitheokrasi.” Mwangalizi mmoja wa mzunguko aliandika kuhusu maandalizi ya zamani ya utumishi wa chakula: “Mpango wa zamani ulifanya ndugu wengi wakose programu nzima ya kusanyiko.” Kuhusu chakula ambacho akina ndugu walileta, akaandika mzee mmoja: “Walikuwa na kile walichotaka tu, na hawakulazimika kukisubiri kwenye foleni.” Mwishowe, dada mwingine aliandika: “Baada ya programu kulikuwa na amani na kimya na kulikuwa na uchangamfu.” Naam, kila mtu angeleta cha kutosha kujishibisha hadi kipindi cha alasiri. Wengi walieleza kwamba walikuwa na wakati mwingi zaidi wa kutembelea marafiki.

19 Mwaka huu tena hakutakuwa na utumishi wa chakula. Unaweza kuchukua dakika chache kupitia nyongeza ya Huduma ya Ufalme Yetu ya Mei 1995, mafungu 12, 13, kwa madokezo juu ya chakula kiwezacho kubebwa mkusanyikoni. Tafadhali kumbuka, vyombo vya bilauri au vileo havipaswi kuletwa kwenye majengo ya mkusanyiko. Ikiwa vyombo vya kuhifadhi baridi vidogo ni vya lazima, lazima vitoshee chini ya kiti chako. Kumbuka kwamba kuna wakati wa kutosha wakati wa mapumziko ya mchana wa kula na kunywa unacholeta. Kama ilivyo kwenye Majumba ya Ufalme yetu wakati wa mikutano, sikuzote sisi hujizuia kula wakati wa vipindi vya mkusanyiko. Hivyo twaonyesha staha kwa mpango wa ibada na chakula cha kiroho kinachoandaliwa.

20 Tahadhari ya ziada ni kwamba hakuna upishi unaopaswa kufanywa katika mahali pa mkusanyiko au katika vyumba vya hoteli isipokuwa kama kuna nafasi ndogo kwa kusudi la kupika. Ni vema kufikiri kwa uzito uhakika wa kwamba wakati ulioruhusiwa kwa ajili ya pumziko la mchana umepangwa ili tuweze kushiriki kiburudisho chepesi na kufurahia ushirika wa kitheokrasi wa ndugu na dada zetu. Tukiwa watu wa Yehova, twatambua kwamba chakula cha kiroho kwenye mikusanyiko ni chenye umuhimu zaidi kikilinganishwa na vitu vya kimwili, na twapaswa kufanya mipango ifaavyo.

21 Hivi karibuni wa kwanza kati ya Mikusanyiko ya Wilaya ya “Wajumbe wa Amani ya Kimungu” utaanza. Je, umekamilisha matayarisho yako ya kuhudhuria, na sasa uko tayari kufurahia siku tatu za ushirika wenye furaha na mambo mazuri ya kiroho? Ni sala yetu nyoofu kwamba Yehova atabariki jitihada zenu za kuhudhuria mkusanyiko mwaka huu.

[Sanduku katika ukurasa wa 10]

Vikumbusha vya Mkusanyiko wa Wilaya

Ubatizo: Wataka kubatizwa wapaswa kuwa vitini mwao katika mahali palipoteuliwa kabla ya programu kuanza Jumamosi asubuhi. Imeonekana kwamba wengine huvaa mavazi ambayo hayana heshima na yasiyofaa hiyo pindi. Vazi la kuogelea lenye kiasi na taulo vyapasa kuletwa na kila mmoja anayepanga kubatizwa. Wazee wa kutaniko wanaopitia maswali katika kitabu Huduma Yetu pamoja na wataka kubatizwa wangependa kuhakikisha kwamba kila mtu anaelewa mambo haya. Baada ya hotuba ya ubatizo na sala itakayotolewa na msemaji, mwenyekiti wa kipindi atatoa maagizo mafupi na kisha atataja wimbo. Baada ya ubeti wa mwisho, wakaribishaji watawaongoza wataka kubatizwa hadi kwenye mahali pa uzamisho. Kwa kuwa ubatizo katika mfano wa wakfu wa mtu ni jambo la uhusiano wa karibu na la kibinafsi kati ya mtu huyo na Yehova, hakuna uandalizi wa ule uitwao eti ubatizo wa kishirika ambapo wataka kubatizwa wawili au zaidi hukumbatiana au kushikana mikono wanapobatizwa.

Kadi za Beji: Tafadhali vaa kadi ya beji ya 1996 kwenye mkusanyiko unaposafiri kwenda na kutoka mahali pa mkusanyiko. Mara nyingi hili hufanya iwezekane kwetu kutoa ushahidi mzuri tunaposafiri. Kadi na vifuko vya beji vyapasa kupatikana kupitia kutaniko, kwa kuwa havitapatikana mkusanyikoni. Usingoje hadi siku chache kabla ya mkusanyiko kuuliza juu ya kadi zako na za familia yako. Kumbuka kubeba kadi yako ya wakati huu ya Mwelekezo wa Mapema Kuhusu Tiba/Ondoleo la Hatia. Washiriki wa familia ya Betheli na mapainia wanapaswa kuwa na vitambulisho vyao.

Nyimbo: Nyimbo zifuatazo zimeteuliwa kwa ajili ya programu ya mwaka huu: 8, 15, 16, 26, 38, 42, 59, 111, 123, 127, 159, 170, 174, 187, 207, 211, 212, na 215. Watu mmoja-mmoja na vikundi vya familia huenda wakataka kupanga vipindi vya mazoezi ili waweze kushiriki kikamili katika kuimba nyimbo zote wakati wa programu ya mkusanyiko.

Utumishi wa Kujitolea: Kukiwa hakuna tena utumishi wa chakula wengi waliokuwa wakifanya kazi katika idara hiyo sasa kwamba wanaweza kujitolea kufanya kazi mahali kwingine. Je, waweza kutenga kando wakati kwenye mkusanyiko ili usaidie katika idara mojapo? Kutumikia ndugu zetu, japo kwa saa chache tu, kwaweza kusaidia sana na kuleta kiasi kizuri cha uradhi. Ikiwa waweza kusaidia, tafadhali ripoti kwenye Idara ya Utumishi wa Kujitolea kwenye mkusanyiko. Watoto walio chini ya umri wa miaka 16 wanaweza kuchangia vizuri kwa kufanya kazi chini ya mwelekezo wa mzazi au mtu mzima mwingine mwenye kuchukua mambo kwa uzito.

Maneno ya Tahadhari: Angalia matatizo yawezayo kutokea ili kuepuka magumu yasiyo ya lazima. Mara nyingi wezi na watu wengine walaghai huibia watu ambao wako mbali na mazingira ya kwao. Hakikisha gari lako limefungwa nyakati zote, na usiache kamwe garini chochote chenye kuonekana kiwezacho kumfanya mtu alivunje ili kuiba. Wezi na wenye kuibia watu mifukoni hukazia fikira vikusanyiko vikubwa. Halingekuwa jambo la hekima kuacha vitu vyovyote vyenye thamani kitini mwako. Huwezi kuwa na hakika kwamba kila mtu anayekuzunguka ni Mkristo. Kwa nini utokeze ushawishi? Ripoti zimepatikana za majaribio yaliyofanywa na watu fulani wa nje ili kudanganya watoto na kuwatorosha. JUA MAHALI WATOTO WAKO WALIPO NYAKATI ZOTE.

Uangalifu wapaswa kutolewa pia ili kuepuka kujaza kupita kiasi magari yaliyokodiwa na kutaniko kwa ajili ya safari ya mkusanyiko. Ni afadhali kutumia fedha zaidi kwa gharama za usafiri kuliko kuvunja sheria za Kaisari au vibaya hata zaidi kuweka akina ndugu katika hatari za aksidenti na upotezo uwezekanao wa uhai kwa sababu ya kujaza gari kupita kiasi au kumtia moyo dereva aendeshe kasi zaidi ili mfike mwisho wa safari mapema. (Rum. 13:1-7; Kum. 21:1-9) Akina ndugu wenye daraka wanaosafiri kwenye magari hayo wanapaswa kujihisi huru kutoa shauri lenye upendo kuhusiana na jambo hili ikihitajika.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki