Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • km 6/96 kur. 3-6
  • Jinsi ya Kufanya Wanafunzi kwa Kutumia Kitabu Ujuzi

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jinsi ya Kufanya Wanafunzi kwa Kutumia Kitabu Ujuzi
  • Huduma Yetu ya Ufalme—1996
  • Habari Zinazolingana
  • Jinsi ya Kumsaidia Mwanafunzi wa Biblia Afikie Hatua ya Ubatizo—Sehemu ya Kwanza
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2020
  • Jinsi ya Kumsaidia Mwanafunzi wa Biblia Afikie Hatua ya Ubatizo—Sehemu ya Pili
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2020
  • Wasaidie Wanafunzi Wako wa Biblia Wafikie Ubatizo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2021
  • Kazia Uangalifu ‘Ufundi Wako wa Kufundisha’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
Pata Habari Zaidi
Huduma Yetu ya Ufalme—1996
km 6/96 kur. 3-6

Jinsi ya Kufanya Wanafunzi kwa Kutumia Kitabu Ujuzi

1 Mradi mzuri kwa Wakristo wote ni kufundisha wengine kweli na kufanya wanafunzi ‘wale waliokusudiwa [“walio na mwelekeo ufaao kwa,” NW] uzima wa milele.’ (Mdo. 13:48; Mt. 28:19, 20) Tengenezo la Yehova limeweka mikononi mwetu chombo kizuri ajabu cha kutimiza jambo hili—kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele. Kichwa chake hukazia umaana mkubwa wa mafunzo ya Biblia ya nyumbani, kwa kuwa uhai udumuo milele hutegemea kutwaa ujuzi wa Yehova, Mungu wa pekee wa kweli, na Mwanaye, Yesu Kristo.—Yn. 17:3.

2 Kitabu Ujuzi sasa ndicho kichapo kikuu cha Sosaiti cha kutumia katika kuongoza mafunzo ya Biblia. Kwa kukitumia, twaweza kufundisha kweli kwa urahisi, uwazi, na kwa ufupi. Itasaidia kufikia mioyo ya wale wanaofundishwa. (Luka 24:32) Bila shaka, kuna uhitaji wa mwenye kuongoza kutumia vizuri stadi za kufundisha. Kwa kusudi hilo, nyongeza hii imetayarishwa ili kuandaa madokezo na vikumbusha kuhusu njia za kufundisha ambazo zimethibitika kuwa zenye matokeo. Kwa ufahamu, na kulingana na hali za mtu mmoja-mmoja, huenda ukaweza kutumia hatua kwa hatua baadhi ya mambo au mambo yote yaliyoandikwa humu. Hifadhi nyongeza hii, na uirejezee mara kwa mara. Mambo kadhaa ndani yayo huenda yakakusaidia uwe mwenye matokeo zaidi katika kutumia kitabu Ujuzi ili kufanya wanafunzi.

3 Ongoza Funzo la Biblia Lenye Maendeleo: Pendezwa kihalisi na mwanafunzi anayeweza kuwa mwanafunzi Mkristo na ndugu au dada wa kiroho. Uwe mchangamfu, mwenye urafiki, na mwenye idili. Kwa kuwa msikilizaji mzuri, unaweza kujua mtu huyo—malezi yake na hali zake maishani—mambo yatakayokusaidia ufahamu jinsi ya kumsaidia vizuri kiroho. Uwe tayari kujitoa mwenyewe kwa mwanafunzi huyo.—1 The. 2:8.

4 Funzo linapokuwa limeanzishwa, inapendekezwa kwamba sura zilizo katika kitabu Ujuzi zisomwe katika jinsi zinavyofuatana. Kufanya hivi kutasaidia mwanafunzi apate uelewevu wa hatua kwa hatua wa kweli, kwa kuwa kitabu hicho hutoa masomo ya Biblia katika ufuatano wenye kusababu kuzuri. Fanya funzo liwe rahisi na lenye kupendeza ili liwe changamfu na lenye kusonga. (Rum. 12:11) Ikitegemea hali na uwezo wa mwanafunzi, huenda ikawezekana kwako kusoma sura nzima katika kipindi kimoja cha muda wa saa moja hivi, bila kuharakisha funzo. Wanafunzi watafanya maendeleo mazuri wakati mwalimu na mwanafunzi wanaposhikilia miadi yao ya funzo kila juma. Hivyo, kwa watu walio wengi, huenda ikawezekana kukamilisha sura 19 za kitabu hicho kwa miezi ipatayo sita hivi.

5 Anza kila kipindi kwa maelezo mafupi ya kuchochea kupendezwa katika habari. Utaona kwamba kichwa cha kila sura ndicho habari yayo kuu, kinachohitaji kukaziwa. Kila kichwa kidogo hutenga jambo kuu, ikikusaidia kukazia kichwa cha sura. Uwe mwangalifu usiongee kupita kiasi. Badala ya hivyo, jaribu kuvuta maelezo ya mwanafunzi. Kumuuliza mwanafunzi maswali hususa yenye kuonyesha majibu unayotaka, yakitegemea anachojua tayari, kwaweza kumsaidia asababu na kupata majibu sahihi. (Mt. 17:24-26; Luka 10:25-37; ona kitabu Kiongozi cha Shule, ukurasa 51, fungu 10.) Fuata kwa ukaribu habari iliyochapwa katika kitabu Ujuzi. Kuingiza mambo mengine mengi ya ziada kwaweza kuondoa mambo makuu au kufanya yasieleweke vizuri na kurefusha funzo. (Yn. 16:12) Swali lisilohusu funzo litokezwapo, mara nyingi unaweza kulijibu baada ya kusoma. Kufanya hivi kutakuruhusu ufunze somo la juma hilo bila kukengeushwa. Mweleze mwanafunzi kwamba hatimaye maswali yake yaliyo mengi ya kibinafsi yatajibiwa wakati wa funzo.—Ona kitabu Kiongozi cha Shule, ukurasa 94, fungu 14.

6 Ikiwa mwanafunzi anaamini sana ule Utatu, kutokufa kwa nafsi, moto wa helo, au mafundisho mengine kama hayo ya uwongo, na yanayosemwa katika kitabu Ujuzi hayamtoshelezi, unaweza kumpa kitabu Kutoa Sababu au kichapo kingine kinachozungumzia jambo hilo. Mwambie kwamba utazungumza naye habari hiyo baada ya yeye kufikiria yale atakayosoma.

7 Kuanza na kumaliza funzo kwa sala ili kuomba mwongozo na baraka za Yehova hufanya pindi hiyo kuwa ya pekee, humfanya mtu awe na akili yenye staha, na kukazia uangalifu Yehova akiwa Mwalimu wa kweli. (Yn. 6:45) Ikiwa mwanafunzi bado hutumia tumbaku, huenda hatimaye ukahitaji kumwomba ajiepushe wakati wa funzo.—Mdo. 24:16; Yak. 4:3.

8 Fundisha kwa Matokeo Ukitumia Maandiko, Vielezi, na Maswali ya Pitio: Haidhuru mwalimu mwenye ustadi amejifunza habari hiyo mara ngapi awali, mwalimu mwenye ustadi atatayarisha kila somo akifikiria mwanafunzi hasa. Kufanya hivi husaidia kutarajia baadhi ya maswali ya mwanafunzi. Ili kufundisha kwa matokeo, elewa waziwazi mambo makuu ya sura hiyo. Chunguza maandiko uone jinsi yanavyotumika kuhusu habari hiyo, na uamue ni yapi unayopaswa kusoma wakati wa funzo. Wazia jinsi unavyoweza kufundisha ukitumia picha na maswali ya pitio mwishoni mwa sura.

9 Kwa kutumia maandiko vizuri, utasaidia mwanafunzi kufahamu kwamba kwa kweli anajifunza Biblia. (Mdo. 17:11) Ukitumia sanduku “Tumia Biblia Yako Vizuri,” kwenye ukurasa 14 wa kitabu Ujuzi, mfundishe jinsi ya kupata Maandiko. Mwonyeshe jinsi ya kutofautisha mistari iliyonukuliwa katika somo. Kadiri wakati uruhusuvyo, fungueni na kusoma maandiko yaliyowekwa ambayo hayajanukuliwa. Mwache mwanafunzi atoe maelezo jinsi maandiko hayo yanavyounga mkono au kuelewesha yaliyo katika fungu. Kazia sehemu kuu za maandiko ili aje kuthamini sababu za mambo makuu ya somo hilo. (Neh. 8:8) Kwa ujumla, hakuna haja ya kuhusisha maandiko zaidi katika mazungumzo kuliko yale ambayo kitabu kimeandaa. Toa maelezo juu ya thamani ya kujua majina na utaratibu wa vitabu vya Biblia. Huenda ikasaidia mwanafunzi akisoma mafungu 27-30 ya Mnara wa Mlinzi la Juni 15, 1991. Inapofaa, tia moyo utumiaji wa New World Translation. Hatua kwa hatua unaweza kuonyesha jinsi ya kutumia sehemu mbalimbali, kama vile marejezeo ya kando-kando na faharisi ya maneno ya Biblia.

10 Somo la 34 katika kitabu Kiongozi cha Shule ya Huduma ya Kitheokrasi laeleza kwamba vielezi huchochea kufikiri kwa mtu na kufanya iwe rahisi kuelewa mawazo mapya. Vinachanganya uvutio wa kiakili pamoja na uvutano wa hisia-moyo, hivi kwamba ujumbe wapitishwa kwa nguvu ambavyo mara nyingi haiwezekani kwa maneno sahili ya hakika. (Mt. 13:34) Kitabu Ujuzi kina vielezi kadhaa vyenye kufundisha kwa njia ambayo ni sahili lakini vyenye nguvu. Kwa mfano, kielezi kinachotumiwa kwenye sura ya 17 hujenga uthamini katika jinsi, kwa njia ya kiroho, Yehova huandaa chakula, mavazi, na makao kupitia kutaniko la Kikristo. Vielezi vya picha zenye kupendeza vya kitabu Ujuzi vyaweza kutumiwa kwa matokeo kuamsha hisia-moyo. Chini ya kichwa kidogo “Ufufuo Wenye Shangwe,” kwenye ukurasa 185, uvutano wa fungu la 18 itaimarishwa kwa kumfanya mwanafunzi aangalie nyuma kwenye picha ya ukurasa 86. Hilo laweza kumsukuma afikiri juu ya ufufuo kuwa halisi chini ya Ufalme wa Mungu.

11 Wanafunzi wa Biblia wanahitaji kufanya maendeleo ya kiroho kwa kila somo. Kwa sababu hiyo, usikose kuuliza maswali ya pitio katika sanduku “Tahini Ujuzi Wako” linalopatikana katika mwisho wa kila sura. Usitosheke tu na maelezo sahihi ya yale ambayo yalisomwa. Mengine ya maswali haya yamekusudiwa kuvuta itikio la kibinafsi kutoka moyoni. Kwa mfano, ona ukurasa 31, ambapo mwanafunzi anaulizwa: “Ni sifa zipi za Yehova Mungu ambazo hasa hukuvutia wewe?”—2 Kor. 13:5.

12 Zoeza Wanafunzi Kujitayarisha Kwa Ajili Ya Funzo: Mwanafunzi asomaye somo mapema, hutia alama majibu, na kufikiri jinsi ya kuyaeleza kwa maneno yake mwenyewe atafanya maendeleo ya haraka kiroho. Kwa kielelezo chako na kitia moyo, unaweza kumzoeza kutayarisha kwa ajili ya funzo. Mwonyeshe kitabu chako, ambacho umetia alama au kupiga mstari maneno na maelezo ya msingi. Eleza jinsi ya kupata majibu ya moja kwa moja kwa maswali yaliyochapishwa. Kutayarisha sura moja pamoja kwaweza kuwa msaada kwa mwanafunzi. Mtie moyo ajieleze kwa maneno yake mwenyewe. Ndipo tu itakapokuwa wazi kama anaelewa habari hiyo. Ikiwa anasoma jibu lake kutoka kitabu, unaweza kuchochea kufikiri kwake kwa kumuuliza jinsi angemweleza mtu mwingine jambo hilo kwa maneno yake mwenyewe.

13 Mtie moyo mwanafunzi achunguze maandiko yasiyonukuliwa ikiwa sehemu ya utayarishaji wake wa kila juma, kwa kuwa huenda kusiwe na wakati wa kusoma yote wakati wa funzo. Mpongeze kwa jitihada anayoweka katika masomo yake. (2 Pet. 1:5; ona Mnara wa Mlinzi la Agosti 15, 1993, kurasa 13-14, kwa madokezo zaidi juu ya jambo linaloweza kufanywa na mwalimu na mwanafunzi ili kuongeza kujifunza katika funzo la Biblia.) Kwa njia hii, mwanafunzi anazoezwa kujitayarisha na kutoa maelezo ya maana kwenye mikutano ya kutaniko. Atajifunza jinsi ya kusitawisha mazoea mazuri ya funzo la kibinafsi la Biblia yatakayomtayarisha kuendelea kufanya maendeleo katika kweli baada ya funzo lake la kibinafsi katika kitabu Ujuzi kukamilika.—1 Tim. 4:15; 1 Pet. 2:2.

14 Elekeza Wanafunzi kwa Tengenezo la Yehova: Ni daraka la yule anayefanya mwanafunzi kuelekeza upendezi wa mwanafunzi kwa tengenezo la Yehova. Mwanafunzi atafanya maendeleo haraka zaidi hadi ukomavu wa kiroho akitambua na kuthamini tengenezo na kutambua uhitaji wa kuwa sehemu yalo. Twataka apendezwe na kushirikiana na watu wa Mungu na kutazamia kuwa nasi kwenye Jumba la Ufalme, ambamo anaweza kupokea tegemezo la kiroho na kihisia-moyo ambalo kutaniko la Kikristo hutoa.—1 Tim. 3:15.

15 Broshua Mashahidi wa Yehova—Wanafanya Mapenzi ya Mungu kwa Umoja Ulimwenguni Pote imetolewa ili kufahamisha watu kuhusu tengenezo moja tu ambalo Yehova anatumia leo kutimiza mapenzi yake. Wakati ambapo funzo limeanzishwa, kwa nini usimpe mwanafunzi nakala? Kuanzia mwanzo, endelea kumwalika mwanafunzi mikutanoni. Eleza jinsi inavyoongozwa. Unaweza kumwambia kichwa cha hotuba ya watu wote inayokuja au umwonyeshe makala itakayozungumziwa kwenye Funzo la Mnara wa Mlinzi. Labda unaweza kumpeleka aone Jumba la Ufalme wakati ambapo hakuna mikutano inafanywa ili kuondoa woga wowote ambao huenda akawa nao kuhusu kwenda mahali papya kwa mara ya kwanza. Unaweza kuandaa usafiri kwenye mikutano. Anapohudhuria, mfanye ahisi amekaribishwa na kuhisi starehe. (Mt. 7:12) Mjulishe kwa Mashahidi wengine, kutia ndani wazee. Yatumainiwa kwamba ataanza kuona kutaniko kuwa familia yake ya kiroho. (Mt. 12:49, 50; Mk. 10:29, 30) Unaweza kumwekea mradi, kama vile kuhudhuria mkutano mmoja kila juma, na hatua kwa hatua kuongeza mradi huo.—Ebr. 10:24, 25.

16 Funzo la Biblia nyumbani liendeleapo kupitia kitabu Ujuzi, kazia sehemu zinazoonyesha uhitaji wa ushirika wa kawaida na kutaniko kwenye mikutano. Angalia hasa kurasa 52, 115, 137-139, 159, na vilevile sura ya 17. Eleza hisia zako mwenyewe za ndani za uthamini kwa tengenezo la Yehova. (Mt. 24:45-47) Sema kwa mwelekeo unaofaa kuhusu kutaniko la kwenu na kuhusu yale unayojifunza kwenye mikutano. (Zab. 84:10; 133:1-3) Ingekuwa vizuri kama mwanafunzi angeweza kutazama kila vidio za Sosaiti, kuanzia Jehovah’s Witnesses—The Organization Behind the Name. Ili kupata mawazo zaidi ya jinsi ya kuelekeza upendezi kwenye tengenezo, ona Mnara wa Mlinzi la Aprili 1, 1985, kurasa 8-12, na nyongeza ya Huduma ya Ufalme Yetu ya Aprili 1993.

17 Tia Moyo Wanafunzi Watolee Wengine Ushahidi: Mradi wetu ni kujifunza na watu na kufanya wanafunzi wanaotoa ushahidi kuhusu Yehova. (Isa. 43:10-12) Hilo lamaanisha mwalimu apaswa kutia moyo mwanafunzi azungumze na wengine juu ya yale anayojifunza kutoka katika Biblia. Hilo laweza kufanywa kwa usahili kwa kuuliza: “Ungeweza kuelezaje kweli hii kwa familia yako?” au “Ni andiko gani ambalo ungetumia kuthibitisha jambo hili kwa rafiki yako?” Kazia sehemu mbalimbali kuu katika kitabu Ujuzi ambamo kutoa ushahidi kwachochewa, kama vile kurasa 22, 93-95, 105-106, na vilevile sura ya 18. Inapofaa, mwanafunzi anaweza kupewa trakti kadhaa za kutumia kuwatolea wengine ushahidi wa vivihivi. Dokeza kwamba aalike washiriki wa familia yake wajiunge naye katika funzo lake. Je, ana marafiki ambao pia wangependa kujifunza? Mwombe awaelekeze kwako wale wanaopendezwa.

18 Kwa kuhudhuria Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na Mkutano wa Utumishi, anayetazamiwa kuwa mwanafunzi anaweza kupata mazoezi ya ziada na uchocheo utakaomsaidia awe mtangazaji wa habari njema. Anapoonyesha kupendezwa katika kujiandikisha katika shule au kuwa mtangazaji asiyebatizwa, kanuni zilizo kwenye kurasa 98 na 99 za kitabu Huduma Yetu zitatumika. Ikiwa kuna hali fulani katika maisha yake inayomzuia asistahili, unaweza kufanya utafiti katika vichapo vya Sosaiti ili kupata habari yenye kusaidia ambayo inahusu jambo hilo nawe uishiriki naye. Kwa mfano, huenda mwanafunzi akawa na ugumu wa kushinda uraibu wa tumbaku au dawa nyingine za kulevya. Kitabu Kutoa Sababu chatoa sababu za Kimaandiko zenye nguvu kwa nini Wakristo waepuke mazoea hayo yenye kudhuru, na kwenye ukurasa 62 huonyesha njia ambayo imethibitika kuwa yenye mafanikio katika kusaidia wengine kuacha mazoea hayo. Sali pamoja naye kuhusu jambo hilo, ukimfundisha kuwa na uhakika katika Yehova ili apate msaada.—Yak. 4:8.

19 Utaratibu wa kufuatwa katika kuamua kama mtu anastahili kushiriki katika huduma ya peupe unaonyeshwa katika Mnara wa Mlinzi la Januari 15, 1996, ukurasa 16, fungu 6. Mwanafunzi astahilipo, itasaidia kufanya mazoezi ili kumtayarisha kwa siku yake ya kwanza katika utumishi wa shambani. Kwa njia chanya, zungumza maitikio ya watu na vipingamizi ambavyo ni vya kawaida katika eneo lenu. Mwanzishe katika mahubiri ya nyumba kwa nyumba kwanza ikiwezekana, na umzoeze hatua kwa hatua katika sehemu nyingine za huduma. Ukifanya utoaji wako uwe mfupi na sahili, itakuwa rahisi kwake kuiga. Uwe mwenye kujenga na kutia moyo, ukionyesha shangwe katika mahubiri, ili kwamba awe na roho yako na kuionyesha. (Mdo. 18:25) Mradi wa mwanafunzi mpya wapaswa kuwa awe mtangazaji wa habari njema wa kawaida, mwenye bidii. Labda unaweza kumsaidia apange ratiba ifaayo ya utumishi. Ili afaulu katika uwezo wake wa kutolea wengine ushahidi, unaweza kudokeza kwamba asome matoleo ya Mnara wa Mlinzi ya Januari 15, 1985, kurasa 12-22; Julai 15, 1988, kurasa 9-20; Januari 15, 1991, kurasa 15-20; na Januari 1, 1994, kurasa 20-25.

20 Chochea Wanafunzi Waelekee Wakfu na Ubatizo: Inapaswa kuwezekana kwa mwanafunzi mwenye moyo wa haki kujifunza mambo ya kutosha kupitia funzo la kitabu Ujuzi ili kujiweka wakfu kwa Mungu na kustahili ubatizo. (Linganisha Matendo 8:27-39; 16:25-34.) Hata hivyo, kabla mtu hajachochewa kujiweka wakfu, anahitaji kusitawisha ujitoaji kwa Yehova. (Zab. 73:25-28) Wakati wote wa funzo, tafuta fursa za kujenga uthamini kwa sifa za Yehova. Onyesha hisia zako mwenyewe kwa Mungu. Saidia mwanafunzi afikiri kuhusu kusitawisha uhusiano wenye uchangamfu na wa kibinafsi pamoja na Yehova. Akija kumjua na kumpenda Mungu kikweli, basi atamtumikia Yeye kwa uaminifu, kwa kuwa ujitoaji kimungu unahusiana na jinsi tunavyohisi juu ya Yehova akiwa mtu.—1 Tim. 4:7, 8; Ona Kitabu Kiongozi cha Shule, ukurasa 76, fungu 11.

21 Jitahidi kufikia moyo wa mwanafunzi. (Zab. 119:11; Mdo. 16:14; Rum. 10:10) Anahitaji kuona jinsi kweli inavyomwathiri kibinafsi na kuamua analopaswa kufanya na yale ambayo amejifunza. (Rum. 12:2) Je, kwa kweli anaamini ile kweli inayotolewa kwake juma kwa juma? (1 The. 2:13) Kwa kusudi hilo, unaweza kumvuta mwanafunzi kwa kuuliza maswali ya maoni yenye ufahamu, kama vile: Wahisije kuhusu jambo hili? Unaweza kutumiaje hili katika maisha yako? Kwa maelezo yake unaweza kufahamu ni upande gani anahitaji msaada zaidi ili kufikia moyo wake. (Luka 8:15; ona kitabu Kiongozi cha Shule, ukurasa 52, fungu 11.) Maelezo mafupi ya picha kwenye kurasa 172 na 174 ya kitabu Ujuzi yauliza: “Je, umejiweka wakfu kwa Mungu kupitia sala?” na “Ni nini kinachokuzuia usibatizwe?” Haya yaweza kumchochea mwanafunzi achukue hatua.

22 Utaratibu wa kufuatwa mtangazaji asiyebatizwa atamanipo kubatizwa waonyeshwa katika Mnara wa Mlinzi, Januari 15, 1996, ukurasa 17, fungu 9. Kitabu Ujuzi kiliandikwa kwa lengo la kumtayarisha mtu kujibu yale “Maswali ya Kuuliza Wanaotaka Kubatizwa,” yapatikanayo kwenye nyongeza ya kitabu Huduma Yetu, ambayo wazee watayapitia pamoja naye. Ikiwa umekazia majibu kwa maswali yaliyochapishwa katika kitabu Ujuzi, mwanafunzi apaswa kuwa ametayarishwa vizuri kwa ajili ya vipindi vya maswali yanayoongozwa na wazee katika kumwandaa kwa ajili ya ubatizo wake.

23 Saidia Wale Wanaomaliza Funzo la Biblia Nyumbani: Inatazamiwa kwamba kufikia wakati mtu anapomaliza funzo la kitabu Ujuzi, unyoofu wake na kina cha upendezi wake katika kumtumikia Mungu lazima utakuwa wazi. (Mt. 13:23) Ndiyo sababu kichwa kidogo cha mwisho cha kitabu hicho chauliza, “Utafanya Nini?” Mafungu ya kumalizia yavuta uangalifu wa mwanafunzi kwenye uhusiano anaopaswa kusitawisha pamoja na Mungu, uhitaji wa kutumia ujuzi ambao amejifunza, na uhitaji wa kutenda kwa haraka kuonyesha upendo wake kwa Yehova. Hakuna uandalizi wa kujifunza vichapo vya ziada na wale wanaomaliza kitabu Ujuzi. Kwa fadhili mweleze mwanafunzi anayeshindwa kuitikia ujuzi juu ya Mungu yale anayopaswa kufanya ili kufanya maendeleo kiroho. Unaweza kuwasiliana naye pindi kwa pindi, ukiacha njia wazi kwake ya kuchukua hatua zinazoongoza kwenye uhai udumuo milele.—Mhu. 12:13.

24 Mwanafunzi mpya anayekubali kweli na kubatizwa atakuwa na ujuzi na uelewevu mwingi zaidi wa kukuza ili kuwa imara kabisa katika imani. (Kol. 2:6, 7) Badala ya kuendeleza funzo lake la Biblia nyumbani baada ya kumaliza kitabu Ujuzi, unaweza kujitolea kuandaa usaidizi wowote wa kibinafsi ambao huenda akahitaji ili akomae kiroho. (Gal. 6:10; Ebr. 6:1) Kwa upande wake, anaweza kukamilisha uelewevu wake kwa kusoma Biblia kila siku, akijifunza kibinafsi Mnara wa Mlinzi na vichapo vingine vya ‘mtumwa mwaminifu,’ kutayarisha na kuhudhuria mikutano, na kuzungumza kweli pamoja na waamini wenzake. (Mt. 24:45-47; Zab. 1:2; Mdo. 2:41, 42; Kol. 1:9, 10) Kusoma kwake kitabu Huduma Yetu na kutumia yaliyo humo kutatimiza sehemu muhimu katika kuwa kwake mtu aliyepangwa kitheokrasi ili kutimiza huduma yake kikamili.—2 Tim. 2:2; 4:5.

25 Sitawisha Ustadi wa Kufundisha: Tumeagizwa ‘kuwafanya mataifa yote kuwa wanafunzi na kuwafundisha.’ (Mt. 28:19, 20) Kwa kuwa ustadi wa kufundisha wahusianishwa sana na kufanya wanafunzi, twataka kujitahidi kufanya maendeleo tukiwa walimu. (1 Tim. 4:16; 2 Tim. 4:2) Kwa madokezo zaidi juu ya jinsi ya kusitawisha ustadi wa kufundisha, huenda ukataka kusoma: “Kusitawisha Ustadi wa Kufundisha” na “Kuufikia Moyo wa Wasikilizaji Wako” katika kitabu Kiongozi cha Shule, masomo 10 na 15; “Teacher, Teaching” (Mwalimu, Ufundishaji) katika Insight, Buku la 2; na makala za Mnara wa Mlinzi “Kujenga kwa Vitu Visivyoweza Kuchomwa na Moto” na “Unapofundisha, Fikia Moyo,” Januari 1, 1985; “Je! Wewe Ni Mwenye Matokeo Katika Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko?,” Machi 1, 1986, na “Jinsi ya Kupata Shangwe Katika Kufanya Wanafunzi,” Februari 15, 1996.

26 Unapojitahidi kufanya wanafunzi, ukitumia kitabu Ujuzi, sikuzote sali kwamba Yehova, yule “akuzaye,” abariki jitihada zako katika kufikia mioyo ya wanadamu kwa habari njema za Ufalme. (1 Kor. 3:5-7) Na upate shangwe ya kufundisha wengine waelewe, wathamini, na kutenda kupatana na ujuzi uongozao kwenye uhai udumuo milele!

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki