Ni Nani Atakayesikiliza Ujumbe Wetu?
1 Watu wamejazwa habari kwa wingi kuliko wakati mwingine wowote katika historia ya binadamu, na zilizo nyingi ni zile zisizo na umaana na hata zenye kuongoza vibaya. Tokeo ni kwamba, wengi wanahisi wamelemewa, hivi kwamba huwa vigumu kwetu kuwafanya wasikilize ujumbe wa Ufalme wa Mungu. Hawang’amui wanaweza kupata tokeo gani chanya kwa kusikiliza Neno la Mungu.—Luka 11:28.
2 Twashangilia kwamba katika sehemu nyingi za ulimwengu, makumi ya maelfu ya watu wanasikiliza ujumbe huo nao wanakubali toleo letu la kuongoza mafunzo ya Biblia nyumbani. Hata hivyo, katika maeneo mengine, itikio si kiasi hicho. Ziara nyingi tunazofanya katika huduma hazina matokeo chanya, na huenda tukajiuliza ni nani atakayesikiliza ujumbe wetu.
3 Ni lazima tuangalie tusije tukavunjika moyo. Paulo alieleza: “Kila atakayeliitia Jina la Bwana ataokoka. Basi wamwiteje yeye . . . wasiyemsikia? Tena wamsikieje pasipo mhubiri? . . . Kama ilivyoandikwa, Ni mizuri kama nini miguu yao wahubirio habari ya mema!” (Rum. 10:13-15) Tukipanda mbegu ya Ufalme kwa bidii, Mungu ataifanya ikue katika wale walio na mioyo yenye kufuatia haki.—1 Kor. 3:6.
4 Ufunguo Ni Kufanya Ziara za Kurudia za Kawaida: Katika maeneo yanayoonekana kuwa na watu wachache wanaosikiliza ujumbe wetu, twahitaji kukaza fikira juu ya kusitawisha kupendezwa kokote tupatako, iwe twaangusha fasihi au la. Kwa nini kuwa mwenye haraka ya kuamua kwamba hakuna jambo litakalotimizwa? Tunapopanda mbegu, hatujui mahali itakapofanikiwa. (Mhu. 11:6) Tunaporudi tukiwa tumetayarisha jambo kutoka Maandiko, hata kama ni kifupi tu, huenda tukaweza kufikia moyo wa mtu huyo. Twaweza kuacha trakti au kutoa magazeti ya karibuni. Hatimaye, huenda tukaweza kuonyesha jinsi ya kujifunza Biblia. Tutashangaa kuona jinsi ambavyo Yehova abariki jitihada zetu.—Zab. 126:5, 6.
5 Mwanamke mmoja aliyeonyesha kupendezwa aliachiwa trakti. Hakupatikana nyumbani tena hadi miezi miwili baadaye, alipokuwa mwenye shughuli mno asiweze kuongea. Aliachiwa trakti ileile tena. Zijapokuwa jitihada za kuendelea za mtangazaji za kufika nyumbani kwake, ilichukua miezi mitatu mingine kumfikia, na kupata tu yeye ni mgonjwa. Dada huyo alimtembelea tena juma lililofuata, na mazungumzo mafupi yakaanza kuhusu ile trakti. Dada aliporudi juma lililofuata, mwanamke huyo alionyesha kupendezwa kikweli katika ujumbe wa Ufalme. Badiliko la hali katika maisha yake lilimfanya akazie uangalifu uhitaji wake wa kiroho. Funzo la Biblia lilianzishwa, na akajifunza kwa idili kila juma baada ya hapo.
6 Kama ilivyo na chochote tutakacho kuona kikikua, iwe ni maua, mboga, au upendezi katika ujumbe wa Ufalme, kulima kwahitajiwa. Hilo huchukua wakati, jitihada, na kujali, na azimio la kutokufa moyo. Mwaka uliopita, watu zaidi ya theluthi moja ya milioni ambao ndani yao mbegu ya Ufalme ilikuwa imeanza kukua walibatizwa! Tukiendelea kuhubiri tutahakikishiwa kupata watu wengi zaidi ambao watasikiliza ujumbe wetu.—Linganisha Wagalatia 6:9.