Hakikisha Kwamba Unarudia
1 Tukiwa wahudumu wa habari njema, tumeamuriwa tufanye wanafunzi. (Mt. 28:19, 20) Kufanya ziara za kurudia ni sehemu ya maana ya kazi yetu ya kufanya wanafunzi. Tunajua kwamba maisha zinahusika, kwa hiyo tunataka tufanye kila jitihada ili kusitawisha upendezi wa kwanza ulioonyeshwa.
2 Tunapaswa tumwone kila mtu ambaye tumemwangushia kichapo kuwa astahili kurudiwa. Hata hivyo, kuangusha vichapo hakupasi kuwa ndio msingi pekee wa kufanya marudio. Wengi hupenda kuwa na mazungumzo ya ujumbe wa Biblia lakini hukataa vichapo. Kwa hiyo ikiwa upendezi unaonekana, tunapaswa kwa vyovyote kurudi na kujaribu kuusitawisha.
3 Kufuatia Ulivyoangusha: Kwa kuwa maangusho ya vichapo huzidi sana idadi ya marudio, kuna uwezekano mkubwa wa maendeleo. Painia mmoja aliangusha kitabu lakini akaona kuwa mwenye nyumba hakupendezwa sana. Alasiri moja baada ya kufanya marudio yake yote mengine, ndugu huyo aliamua kurudia mtu huyo. Funzo la Biblia lilianzishwa.
4 Ndugu mmoja alimwangushia mtu fulani magazeti mawili lakini akamsahau, akifikiri kuwa hakupendezwa kikweli. Siku kadhaa baadaye, mtu huyo aliandikia kundi la mahali hapo barua akiomba abatizwe. Dada mmoja mishonari aliulizwa ni jambo lipi aliloona kuwa la maana sana katika kuweza kusaidia watu 74 kuwa wahubiri. Yeye alisema: “Tulifanya kazi ya magazeti sana, na niliendelea kufanya marudio kwa watu waliochukua magazeti mpaka nilipoweza kuanzisha mafunzo ya Biblia pamoja nao.”
5 Nyakati nyingine huenda tukaweza tu kumwachia mwenye nyumba trakti katika ziara ya kwanza. Mara nyingi, trakti zaweza kutumiwa kwa matokeo katika marudio kuonyesha jinsi funzo la Biblia lifanywavyo. Alipokuwa akihubiri na mhubiri mwingine, mwangalizi wa mzunguko mmoja alimwachia mwanamke fulani trakti. Ilikuwa ziara fupi sana, lakini alimtia moyo dada huyo arudie. Dada huyo alifanya rudio na akaanzisha funzo la Biblia mara moja.
6 Kupendezwa Kunapoonyeshwa: Mwenye nyumba asipochukua kichapo katika ziara ya kwanza, hilo halimaanishi sikuzote kwamba yeye hapendezwi. Mhubiri mmoja alipofanya rudio kwa wenzi wa ndoa wachanga, alipata kuwa tayari walikuwa na baadhi ya vichapo vyetu na walikuwa wamejifunza hapo mbeleni. Wao walikubali bila kusita kuanza funzo lao tena. Painia wa pekee mmoja aliona kupendezwa kusikoonyeshwa wazi katika mwanamke mmoja aliyekataa magazeti nyakati zote. Painia huyo aliweka magazeti kando, na mwanamke huyo akakubali mazungumzo juu ya mafungu machache katika kimojawapo vijitabu. Baada ya ziara nyingine chache, yeye alikuwa na funzo la Biblia mara mbili kwa juma.
7 Kila mtu anayejiweka wakfu kwa Yehova apaswa ajione kuwa na daraka la kushiriki katika kazi ya kufanya wanafunzi. Tunapofanya marudio ya kawaida kwa wote wanaoonyesha kupendezwa, tutavuna matunda yatakayoleta baraka kwetu sisi na ‘wale watusikiao pia.’—1 Tim. 4:16.