Kusonga Mbele Kwako na Kuwe Dhahiri kwa Watu Wote
1 Maendeleo na kusonga mbele ni ishara moja ya Ukristo wa kweli. Tukiwa wanafunzi wa Kristo twafuata uongozi wake, na tujitiishapo kwa utendaji-kazi wa roho takatifu ya Mungu, twaweza kusonga mbele kufikia hali ya kuwa “mtu mkamilifu, hata kufika kwenye cheo cha kimo cha utimilifu wa Kristo.” (Efe. 4:13) Ndipo kusonga mbele kwetu ‘kwaweza kuwa dhahiri kwa watu wote’ kama Paulo anavyoonyesha kwenye 1 Timotheo 4:15. Katika miezi ya majuzi tumeona vilele vipya katika idadi ya watangazaji na Yehova anabariki kazi hiyo.
2 Huduma yetu ya shambani ni sehemu moja ambayo kusonga mbele kwetu huwa dhahiri ikiwa twajitiisha chini ya maongozi ya roho takatifu katika tengenezo la Yehova na kuonyesha kuwa sisi ni wenye maendeleo. Vipi wewe binafsi? Je, unafanya maendeleo? Je, umesonga mbele? Mathalani, je, wewe huhubiri tofauti na wakati ulipokuwa mpya katika kweli? Je, mahubiri ya nyumba hadi nyumba yamekuwa sehemu ya huduma yako ya shambani ya kila mwezi? Pia, je, wewe huripoti utendaji wako wa huduma ya shambani bila kukawia mwishoni mwa kila mwezi? Je, wewe hutumia namna mbalimbali za mfikio, tangulizi, na vichwa, ukifuata madokezo yanayopokewa kwenye makusanyiko na mikutano? Au bado unasema kwamba unataka kuongea kuhusu Biblia au Ufalme wa Mungu, ukiuliza msikilizaji wako kama anapendezwa? Kila mwezi Huduma ya Ufalme Yetu huwa na madokezo mazuri, na Yehova hubariki wote wenye maendeleo ambao hutumia madokezo haya.
3 Watangazaji wenye maendeleo pia wamegundua shangwe ya kazi ya magazeti. Wao hubeba magazeti sikuzote na wametenga siku za kutoa magazeti kwa utoaji mfupi. Mara nyingi magazeti haya husomwa na watu zaidi ya mmoja. Hebu fikiria ushahidi mkubwa unaotolewa kupitia magazeti haya! Je, waweza kusonga mbele katika sehemu hii ya kazi ya magazeti? Kwa nini usifanye agizo la kibinafsi la magazeti ya kugawanya?
4 Kutumia toleo la kila mwezi ni sehemu nyingine ya huduma yetu ambayo kwayo mtu aweza kufanya kusonga kwake mbele kuwe dhahiri. Hutoa uradhi wa pekee kwenda sambamba na tengenezo la Yehova na kufuata yanayodokezwa kwenye Huduma ya Ufalme Yetu. Je, wewe hubeba fomu ya rekodi ya nyumba kwa nyumba uandike? Unapopata wenye kupendezwa je, wewe hufanya matayarisho ya mapema ya ziara za kurudia? Kufanya hivyo kutasaidia katika kupata ziara za kurudia nyingi na zilizo bora. Halafu, je, wewe hutumia madokezo kutoka Huduma ya Ufalme Yetu kwenye ziara hizi ukiwa na lengo la kuanzisha mafunzo ya Biblia? Hata watangazaji walio na uwezo mdogo wa kusoma wanaweza kuongoza mafunzo ya Biblia katika broshua zetu!
5 Kuna sehemu katika mitazamo na mwenendo wetu ambazo katika hizo lazima sikuzote twendelee kusonga mbele. Mathalani, ingawa katika ulimwengu hisia za kikabila na fahari ya ukabila huonekana kuwa yenye nguvu, je, sisi huondoshea mbali tabia kama hizo za kimwili kutoka mioyoni na akilini mwetu? Je, sisi huonyesha kusonga mbele katika utu mpya, tukikuza upendo kwa ushirika wa ulimwenguni pote wa akina ndugu, vitu vyenye kutamanika vya mataifa yote? (1 Pet. 2:17; Hag. 2:7) Ukosefu wowote katika sehemu hiyo ungeonyesha kushindwa kufuata kiongozi wetu, Yesu Kristo. Tumepokea ripoti zenye kutia moyo sana, zikisema jinsi ndugu zetu wameonyesha upendo wa kujidhabihu kwa ndugu wenzao wa kabila au kikundi cha kikabila tofauti, kama ielezwavyo katika 1 Yohana 3:16, 17. Jambo hili limetokeza ushahidi mzuri na limeletea jina la Yehova sifa. Katika sehemu hizi zote acheni tufanye kusonga kwetu mbele kuwe dhahiri kwa watu wote.—1 Tim. 4:15.