Shiriki Kazi Ambayo Haitarudiwa Kamwe
1 Nyakati tofauti-tofauti katika historia ya wanadamu, ilimbidi Yehova atekeleze hukumu dhidi ya adui zake. Hata hivyo, kwa sababu ya rehema zake, aliwaandalia waadilifu fursa ya wokovu. (Zab. 103:13) Itikio lao liliamua tokeo lao la hatima.
2 Kwa kielelezo, kabla ya Gharika, katika 2370 K.W.K., Noa alikuwa “mhubiri wa uadilifu.” Wale walioangamia walikuwa wale waliopuuza onyo la kimungu. (2 Pet. 2:5; Ebr. 11:7) Kabla ya uharibifu wa Yerusalemu katika 70 W.K., Yesu alieleza waziwazi hatua itakayohitajiwa kwa yeyote kuepuka uharibifu uliokuwa ukitazamiwa kulipata jiji hilo. Wote waliokataa ujumbe wake wenye onyo walipatwa na matokeo yenye msiba. (Luka 21:20-24) Maonyo na hukumu hizo za kimungu zilirudiwa mara nyingi katika historia.
3 Kazi ya Kuonya ya Siku ya Kisasa: Yehova alitangaza zamani sana kwamba hasira yake haingezuiwa kuelekea mfumo mbovu wa leo na kwamba ni wasikivu tu ambao wangeokoka. (Sef. 2:2, 3; 3:8) Wakati wa kuhubiri ujumbe huu wenye onyo unapungua! “Dhiki kubwa” iko mbele, nao wasikivu wanakusanywa. “Mashamba” ni “meupe kwa ajili ya kuvunwa” kwelikweli. Kwa sababu hiyo, hakuna kazi nyingine yoyote iwezayo kulinganishwa na hii kwa habari ya umaana na uharaka.—Mt. 24:14, 21, 22; Yn. 4:35.
4 Twapaswa kushiriki katika kutoa onyo la siku ya kisasa kwa wengine, “kwamba watasikia au kwamba hawataki kusikia.” Huu ni mgawo wenye kupewa na Mungu, ambao ni lazima tusiupuuze. (Eze. 2:4, 5; 3:17, 18) Kushiriki kwetu kikamili katika kazi hii huandaa wonyesho wenye kusadikisha wa upendo wetu wenye kina kirefu kwa Mungu na kuhangaikia kihalisi kwa majirani wetu, na imani yetu isiyoyumbayumba katika Mwokozi wetu, Yesu Kristo.
5 Sasa Ndio Wakati wa Kutenda: Baada ya hukumu za Yehova za zamani, sikuzote uovu ulitokeza upya kwa sababu Shetani na roho wake waovu walikuwa wangali wanatenda. Hata hivyo, wakati huu itakuwa tofauti. Uvutano wa kishetani utaondoshwa. Nalo onyo la tufeni pote halitahitajiwa tena. (Ufu. 7:14; Rom. 16:20) Tuna pendeleo la pekee la kuwa sehemu ya kazi ambayo haitarudiwa kamwe. Sasa ndio wakati wa sisi kutumia vizuri fursa hii.
6 Mtume Paulo, akiwa na usadikisho mkubwa kuhusu utendaji wake wa kuhubiri, alisema hivi: “Mimi ni safi kutokana na damu ya watu wote.” (Mdo. 20:26) Yeye hakuhisi kuwa mwenye hatia kwa sababu ya kushindwa kokote kutoa onyo. Kwa nini? Kwa sababu aliweza kusema hivi kuhusu huduma yake: “Kwa madhumuni haya kwa kweli ninafanya kazi kwa bidii, nikijikakamua mwenyewe.” (Kol. 1:29) Acheni tufurahie uradhi huohuo wa kushiriki kikamili iwezekanavyo katika kazi ambayo haitarudiwa tena kamwe!—2 Tim. 2:15.