“Jenga Nyumba Yako”
1 Bila shaka, katika kila utamaduni ulimwenguni pote, maisha ya familia yanachanguka. Ulimwengu wa Shetani unajiingiza sana katika udanganyifu na ukosefu wa adili. (1 Yoh. 5:19) Jambo hilo hukazia uharaka kwetu ‘kujenga nyumba yetu’ na kufundisha wengine jinsi wanavyoweza kufanya vivyo hivyo na nyumba zao.—Mit. 24:3, 27.
2 Kanuni za Biblia Ni Ulinzi Salama: Siri ya furaha ya familia ya kweli yapatikana kwa kutumia kanuni za Biblia. Kweli hizi zenye nguvu humnufaisha kila mshiriki wa nyumbani katika sehemu zote za maisha. Familia inayozitumia itafurahia amani ya kimungu.—Linganisha Isaya 32:17, 18.
3 Kanuni ambazo zaweza kutusaidia kujenga nyumba yetu zimeonyeshwa dhahiri kwa maneno machache katika kitabu kipya, Siri ya Kupata Furaha ya Familia. Kila sura yamalizia kwa sanduku lenye msaada la kufundisha ambalo hukazia kanuni ambazo washiriki wa familia wanahitaji kukumbuka. Mengi ya masanduku haya huanza kwa swali, “Kanuni hizi za Biblia zaweza kusaidiaje . . . ?” Hilo huvuta fikira kwenye mawazo ya Mungu ili tupate kufikiri kwake juu ya jambo linalozungumziwa.—Isa. 48:17.
4 Kizoelee hicho kitabu. Jifunze kupata kanuni ambazo zaweza kusaidia matatizo mbalimbali yatokeapo. Kitabu hicho chazungumzia mambo kama haya: Mambo ambayo mtu apaswa kuangalia anapomtafuta atakayekuwa mwezi wa ndoa (sura ya 2), funguo muhimu zinazofungua mlango wa kuingia kwenye maisha ya ndoa yenye kudumu (sura ya 3), jinsi wazazi wanavyoweza kulea matineja wao wawe watu wazima wenye kumhofu Mungu na wenye kutwaa madaraka (sura ya 6), jinsi ya kulinda familia na mavutano yenye kuharibu (sura ya 8), kanuni za kusaidia familia za mzazi mmoja zifanikiwe (sura ya 9), msaada wa kiroho kwa familia zinazosumbuliwa na uraibu wa alkoholi na jeuri (sura ya 12), jambo la kufanya vifungo vya familia vikiwa katika hatua ya kuvunjika (sura ya 13), linaloweza kufanywa kuwaheshimu wazazi wazee-wazee (sura ya 15), na jinsi mtu awezavyo kupata wakati ujao wenye kudumu kwa familia yake (sura ya 16).
5 Tumia Kikamili Kitabu Kipya: Ikiwa bado hamjafanya hivyo, kwa nini msijifunze kitabu Furaha ya Familia pamoja mkiwa familia? Pia, wakati wowote familia yako inapopatwa na magumu, pitia sura ambazo katika kitabu zashughulika nayo, na kwa sala mchunguze jinsi ya kutumia ushauri huo. Kwa kuongezea, wakati wa Machi, ratibu wakati mwingi wa huduma ya shambani ili uweze kujitahidi kuangushia watu wengi iwezekanavyo kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia.
6 Familia zinazodhihirisha ujitoaji kimungu zitaimarishwa kiroho na kuunganishwa na kutayarishwa vizuri ili kukabiliana na mashambulio ya Shetani. (1 Tim. 4:7, 8; 1 Pet. 5:8, 9) Twashukuru kama nini kwamba tuna mafunzo ya kimungu kutoka kwa Mwanzilishi wa familia!