Halaiki Inaongezwa
1 Kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza, ukuzi ambao kutaniko la Kikristo linapata leo ni wa ajabu. (Mdo. 2:41; 4:4) Mwaka uliopita, wanafunzi wapya 366,579 walibatizwa, wastani wa zaidi ya 1,000 kila siku! Zaidi ya milioni moja walibatizwa wakati wa miaka mitatu iliyopita. Kwa kweli, Yehova amefuliza kuongeza halaiki ya waamini.—Mdo. 5:14.
2 Wapya hao wengi ambao hawana uzoefu katika maisha ya Kikristo wanahitaji msaada na mazoezi kutoka kwa wale wenye imani yenye nguvu. (Rom. 15:1) Miongoni mwa Wakristo wa mapema, kulikuwa na wale ambao, hata miaka kadhaa baada ya ubatizo wao, walikuwa wameshindwa “kusonga mbele kwenye ukomavu.” (Ebr. 5:12; 6:1) Ndiyo sababu, katika barua yake kwa Waebrania, Paulo alikazia sehemu ambazo Wakristo wahitaji kukua kiroho. Hizo ni sehemu zipi, na msaada unaohitajiwa waweza kutolewaje?
3 Kujipatia Mazoea Mazuri ya Kujifunza: Kupatana na maagizo ya Paulo, kuwa mwanafunzi mzuri hutia ndani kujifunza kwa bidii, kurudia somo, na kutumia “chakula kigumu” kinachoandaliwa na tengenezo la Yehova. (Ebr. 5:13, 14; ona Mnara wa Mlinzi la Agosti 15, 1993, ukurasa wa 12-17.) Kwa kuwahusisha waamini wapya katika mazungumzo ya kiroho na kushiriki pamoja nao hazina zenye thamani za kweli ambazo umejifunza kupitia utafiti wa kibinafsi, huenda ukawachochea kujipatia mazoea mazuri ya kujifunza. Labda pindi kwa pindi ungeweza kumwalika mwamini mpya ajiunge nawe katika funzo lako la kibinafsi au la familia.
4 Kuhudhuria Mikutano kwa Ukawaida: Kielelezo chako cha uaminifu na maneno yenye upendo ya kutia moyo yatasaidia washiriki wapya wa kutaniko waepuke sehemu nyingine ya kuangaliwa inayotajwa na Paulo, yaani, “desturi” ambayo wengine huwa nayo ya kukosa mikutano ya Kikristo. (Ebr. 10:24, 25) Wasaidie wathamini kwamba mikutano ndiyo kamba yao ya kiroho ya kuokolea uhai inayowaunganisha na kutaniko. Chukua hatua ya kwanza kuwafanya wahisi wamekaribishwa kuwa sehemu ya udugu wetu.
5 Kumfikia Yehova kwa Uhakika: Ili kushinda udhaifu wa kimwili na dosari za kiutu, lazima tumtafute Yehova katika sala, tukimweleza mawazo yetu ya ndani sana na mahangaiko yetu ya usiri zaidi. Wapya lazima wajue kwamba kwa kumtolea Yehova dua ili kupata msaada, kama alivyosihi Paulo, hawapaswi kusita. (Ebr. 4:15, 16; 10:22) Kusimulia mambo yako ya kibinafsi yaliyoonwa kwa habari hii kutaimarisha uhakika wa aliye mpya kwamba Yehova husikia sala za kuhisiwa moyoni.
6 Kuratibu Wakati kwa Ajili ya Huduma: Paulo alionyesha pia kwamba ‘sikuzote tunapomtolea Mungu dhabihu ya sifa,’ hilo huimarisha kiroho. (Ebr. 13:15) Je, waweza kumwalika mtangazaji mpya ajiunge nawe katika mipango yako ya utumishi wa shambani ya kila juma? Labda nyinyi wawili mwaweza kutayarisha utoaji wenu mbalimbali au kufikiria sehemu ya huduma ambayo huyo mpya hajajaribu bado.
7 Halaiki inayoongezwa ni sababu ya shangwe kubwa. Kujitumia wenyewe katika kuzoeza na kuhimiza sana washiriki wapya wa kutaniko kutawasaidia wasitawishe imani yenye nguvu inayohitajiwa ili ‘kuhifadhi hai nafsi zao.’—Ebr. 3:12, 13; 10:39.