“Fanyeni Hata Zaidi Yote Kabisa Mwezayo”
1 Tulipojiweka wakfu kwa Yehova, tuliahidi kumpa yaliyo bora zaidi. Kwa kufaa, mtume Petro, alitia moyo Wakristo wa karne ya kwanza wafanye yote wawezayo kabisa katika kuhakikisha msimamo wao mbele ya Yehova. (2 Pet. 1:10) Kwa hakika twataka kufanya yote kabisa tuwezayo ili tumpendeze Yehova katika kumtumikia leo. Hilo latia ndani nini? Uhusiano wetu pamoja na Yehova uongezekapo na tunapotafakari yote ambayo ametufanyia, mioyo yetu hutusukuma sikuzote tufanye yote tuwezayo katika utumishi wake. Twataka kuongeza ubora, na iwezekanapo, wingi wa huduma yetu.—Zab. 34:8; 2 Tim. 2:15.
2 Ndugu mmoja mchanga aliyetaka kufanya mengi zaidi katika huduma aliona kwamba funzo la kawaida la Neno la Mungu liliongeza uthamini wake kwa Yehova na likamchochea kuwa na bidii zaidi. Hilo lilimchochea ajiandikishe katika utumishi wa painia. Dada mmoja aliyekuwa na ugumu wa kuongea na watu wasiojulikana alijizoeza utoaji mbalimbali upatikanao katika kitabu Kutoa Sababu na punde si punde akaanza kufurahia mafanikio bora zaidi katika huduma yake. Aliweza kuongoza funzo la Biblia na wenzi wawili waliooana walioikubali kweli.
3 Shangilia Katika Yale Unayoweza Kufanya: Wengine wetu hupatwa na magumu kama vile afya mbaya, upinzani wa familia, umaskini, au ubaridi katika eneo. Matatizo mengine yaliyo ya kawaida katika hizi siku za mwisho yanaweza kuzuia utumishi wetu. (Luka 21:34, kielezi-chini katika New World Translation of the Holy Scriptures—With References; 2 Tim. 3:1) Je, hilo lamaanisha kwamba tumeshindwa kutimiza wakfu wetu kwa Yehova? Sivyo, ikiwa twamtumikia kwa kufanya yote kabisa tuwezayo.
4 Si jambo la hekima kujihukumu kulingana na yale ambayo wengine wanaweza kutimiza. Badala ya hivyo, Maandiko hututia moyo ‘kuacha kila mmoja athibitishe kazi yake mwenyewe ni nini.’ Kujitoa kikamili kadiri tuwezavyo kibinafsi, humpendeza Yehova na kwatupa “sababu ya mchachawo.”—Gal. 6:4; Kol. 3:23, 24.
5 Na tutii maneno ya Petro ya ‘kufanya kabisa yote tuwezayo na mwishowe tupatikane na Mungu tukiwa bila doa na bila waa na katika amani.’ (2 Pet. 3:14) Roho hiyo itatufanya tuhisi tukiwa salama, nayo itatuletea amani ya akili ambayo ni Yehova tu awezaye kutoa.—Zab. 4:8.