Ujuzi Kutoka kwa Mungu Hujibu Maswali Mengi
1 Kabla ya kutwaa ujuzi sahihi wa ile kweli, yamkini ulikuwa na maswali mengi juu ya maisha ambayo hukuweza kuyajibu. Ulikuwa mwenye furaha kama nini ulipopokea majibu ya maswali hayo yenye kutegemea Biblia! Sasa unaweza kusaidia wengine wapate majibu hayohayo. (Linganisha 2 Timotheo 2:2.) Unaweza kushiriki nao ujuzi wa Mungu uongozao kwenye uhai udumuo milele. (Yn. 17:3) Lakini waweza kusaidiaje mtu ang’amue thamani ya ujuzi huu? Fikiria maswali ambayo kweli ilikujibu. Ni nini ambacho watafutaji-kweli hutamani kujua? Kuwa na mambo hayo akilini kwaweza kukusaidia utoe kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele. Madokezo yafuatayo huenda yatakusaidia unapojitayarisha kutoa ushahidi wakati wa Juni.
2 Kwa kuwa watu wengi hujiuliza ni kwa nini kuteseka ni kwingi sana ulimwenguni, mfikio huu huenda ukaleta itikio zuri:
◼ “Msiba utokeapo au matendo ya uhalifu na jeuri yaongezekapo, mara nyingi watu huuliza kwa nini mambo hayo mabaya hutokea. Ungejibuje?” Ruhusu na ushukuru itikio la huyo mtu. Kisha fungua sura ya 8 katika kitabu Ujuzi, na uelekeze fikira kwenye yale yanayosemwa katika fungu la 2. Eleza kwamba kitabu hiki hutoa ufafanuzi wa Biblia kuhusu sababu ya mambo mabaya kutokea, kisha utoe toleo.
3 Unaporudi mahali ulipoangusha kitabu “Ujuzi,” ungeweza kusema:
◼ “Napendezwa na mkataa uliofikia juu ya sababu ya kuwapo kwa kuteseka kwingi ulimwenguni. Je, wakubaliana na jibu la Biblia kama linavyoonyeshwa katika kile kitabu?” Ruhusu itikio. Soma fungu la 17 kwenye ukurasa wa 77 katika kitabu Ujuzi, na ujitolee kusoma Waroma 9:14 kutoka katika Biblia ya mwenye nyumba. Kisha useme: “Habari njema ni kwamba Mungu hatusababishii bila haki maumivu na kuteseka. Ametuahidi kutupatia uhai udumuo milele katika amani na furaha. Sura ya kwanza katika kitabu hiki ina kichwa ‘Unaweza Kuwa na Wakati Ujao Wenye Furaha!’ Ningependa kukueleza jinsi hilo liwezavyo kuwa kweli kwako na kwa wapendwa wako.” Fungua sura ya 1, na uonyeshe njia yetu ya kujifunza. Jifunzeni sehemu kubwa ya sura ya kwanza kwa kufaana na hali.
4 Labda unaweza kuchagua kutumia utangulizi unaopatikana kwenye ukurasa wa 13 katika kitabu “Kutoa Sababu,” chini ya kichwa “Uzee/Kifo”:
◼ “Je! umepata kuuliza hivi, ‘Je! kifo ndio mwisho wa mambo yote? Au kuna jambo jingine baada ya kifo?’ [Ruhusu itikio.] Biblia inajibu swali lo lote tunaloweza kuwa nalo juu ya kifo. [Soma Mhubiri 9:5, 10.] Inaonyesha pia kwamba kuna tumaini kwa watu walio na imani. [Angalia fungu la 13 kwenye ukurasa wa 84 katika kitabu Ujuzi; soma na ueleze maneno ya Yesu yapatikanayo kwenye Yohana 11:25.] Sura hii yote inajibu swali hili, Inakuwaje kwa wapendwa wetu waliokufa? Ikiwa ungependa kukisoma, naweza kukuachia nakala hii kwa mchango wa ________.”
5 Unapofanya ziara ya kurudia, unaweza kufufua hali ya kujuana na mtu huyo kisha useme:
◼ “Wakati uliopita tulizungumzia jinsi inavyokuwa mtu anapokufa. Watu wengi huamini kwamba maisha yoyote baada ya kifo yatakuwa ama mbinguni ama katika helo. Lakini je, umepata kufikiri juu ya uwezekano wa wafu kuishi tena hapahapa duniani? [Ruhusu itikio.] Kulingana na Biblia, wafufuliwa watakuwa miongoni mwa watu wasikivu ambao watairithi dunia. [Soma Zaburi 37:11, 29, kisha uzungumzie fungu la 20 kwenye ukurasa wa 88 katika kitabu Ujuzi.] Tumaini hilo limeyapa faraja maisha ya mamilioni ya watu wanaoishi duniani ambao waliogopa kifo. Kitabu hiki kitakusaidia uelewe vizuri zaidi jambo hilo. Je, nikuonyeshe jinsi ya kufanya hivyo?”
6 Ukipendelea utoaji sahili, waweza kujaribu huu:
◼ “Ningependa kukuonyesha picha katika kitabu hiki, Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele. Je, hii si picha yenye kupendeza?” Fungua kitabu ili mwenye nyumba aweze kuona ukurasa wa 4-5. Ruhusu itikio lake. Kisha usome maneno yaliyo kwenye ukurasa wa 5. Malizia kwa kusema: “Unaweza kuchukua kitabu hiki ujisomee. Sisi hukitoa kwa mchango wa ________.” Mwulize ni wakati gani ungekuwa mzuri ili urudi kufuatia kupendezwa kulikoonyeshwa.
7 Tuna ujuzi kutoka kwa Mungu ambao hujibu maswali ya maana maishani. Tayarisha kwa juhudi, na Yehova atabariki jitihada zako za kushiriki habari hii ipayo uhai, pamoja na wale wanaotafuta kweli.