Uaminifu Unathawabishwa
1 Kwenye Waebrania 11:6 twaambiwa kwamba Mungu “huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.” Njia moja ambayo katika hiyo yeye huthawabisha watumishi wake waliojitoa ambao wamekuwa ‘waaminifu juu ya mambo machache’ ni kwa ‘kuwaweka rasmi juu ya mambo mengi.’ (Mt. 25:23) Yaani, Yehova mara nyingi huthawabisha kazi ya bidii kwa kuwapa mashahidi wake waaminifu mapendeleo ya ziada ya utumishi.
2 Uaminifu wa mtume Paulo ulithawabishwa kwa kuwa alipewa mgawo wa huduma iliyompeleka hadi kwenye majiji na vijiji vya Ulaya na Asia Ndogo. (1 Tim. 1:12) Ijapokuwa jitihada nyingi ilihusika katika kutimiza kikamili huduma yake, Paulo alithamini sana pendeleo alilopokea. (Rom. 11:13; Kol. 1:25) Alionyesha uthamini wake wa kuhisiwa moyoni kwa kutafuta kwa bidii fursa za kuhubiri. Kwa utendaji wake wenye bidii, alionyesha wazi kwamba alikuwa akiishi kulingana na imani yake. Kielelezo chake chatuchochea tuhazini mapendeleo yetu ya utumishi.
3 Yehova Ametupatia Huduma: Sisi twaonyeshaje maoni yaleyale juu ya thawabu hii yenye pendeleo ambayo Paulo alionyesha? Twatafuta njia za kuongeza kushiriki kwetu katika huduma. Twatumia manufaa za kila fursa kutoa ushahidi kivivi-hivi na vilevile mlango hadi mlango. Twafuatia wote wasiokuwako nyumbani na kurudia wote walioonyesha kupendezwa. Nasi twatimiza miadi yote tunayofanya ya kuongoza mafunzo ya Biblia nyumbani.
4 Kuhusu huduma yetu, Paulo alionya hivi kwa upole: “Lifanye kwa hima.” (2 Tim. 4:2) Jambo ambalo ni la hima huhitaji kukaziwa fikira mara moja. Je, sisi hufanya huduma yetu kwa hima, tukiitanguliza katika maisha yetu? Kwa kielelezo, hatutataka kuruhusu utendaji wetu wa tafrija na ufuatiaji mwingine wa kibinafsi kwenye mwisho-juma uingilie wakati tunaopaswa kutoa katika huduma ya shambani. Kwa kuwa tunasadiki kwamba mwisho wa mfumo huu unakaribia sana, pia tunasadiki kwamba kuhubiri habari njema ya Ufalme ndiyo kazi ya maana zaidi tunayoweza kufanya.
5 Uaminifu wetu kwa Mungu waonyeshwa kwa kuwa kwetu wa kweli na waaminifu-washikamanifu kwake na wenye kudumu katika kazi aliyotugawia. Na tutimize huduma yetu kikamili, ili Yehova athawabishe uaminifu wetu kwa njia kubwa.