Toa Ushahidi Mahali Popote Palipo na Watu
1 Akitambua fungu ambalo roho takatifu ya Mungu lilitimiza katika huduma yake, mtume Paulo aliandika hivi: “Mungu akafuliza kuikuza.” Pia alikiri hivi: “Sisi ni wafanyakazi wenzi wa Mungu.” (1 Kor. 3:5-9) Hili ni pendeleo la ajabu. Twaweza kuonyeshaje mbele ya watu kwamba twathamini kuwa wafanyakazi wenzi wa Mungu? Kwa kutangaza habari njema kwa wote tunaowapata katika mahubiri ya nyumba hadi nyumba na mahali pengine pote.
2 Twaamriwa ‘kufanya watu kuwa wanafunzi.’ (Mt. 28:19) Tukiwafikia watu wachache tu tunaposhiriki katika huduma, huenda tukachoka haraka na kuhisi hatukutimiza mengi. Kwa upande mwingine, twafurahia huduma yetu zaidi tunapoweza kupata watu wengi na kuzungumza nao. Jambo hili laweza kuwa gumu, kwa kuwa lahitaji tuchukue hatua ya kwanza kwenda mahali popote palipo na watu ili tuweze kuwafikia.
3 Vielelezo Vyenye Kutumika: Twaweza kutolea watu ushahidi kwenye masoko, mabustani, mahali pa mapumziko, vituo vya usafiri, maegesho ya teksi, vituo vya basi na stesheni za garimoshi. Unapopanda magari ya umma, je, unajitayarisha kutoa ushahidi? Mashahidi wawili waliokuwa wakisafiri kwa basi lililojaa kuelekea kwenye mkutano wao wa utumishi waliendelea na mazungumzo juu ya picha ya Paradiso iliyo katika kitabu Ujuzi, wakizungumzia ahadi za Mungu za wakati ujao. Kama walivyokuwa wametumaini lingetokea, mwanamume mchanga aliyekuwa amesimama karibu na hapo alisikiliza naye akapendezwa na yale aliyosikia. Kabla ya kuondoka kwenye basi hilo, alikubali kitabu na kuomba kwamba mtu fulani amtembelee nyumbani kwake.
4 Wahubiri wengi wamepata shangwe katika kutoa ushahidi wa vivi hivi. Dada mmoja alienda madukani kwao alasiri moja na kufikia watu waliokuwa tu wamemaliza ununuzi wao lakini hawakuonekana kuwa na haraka. Aliangusha fasihi zote alizokuwa nazo katika mfuko wake. Mwanamume mmoja mchanga aliyekuwa akingoja ndani ya gari lake alifurahia kupokea magazeti kutoka kwake. Alikuwa amehudhuria mikutano hapo awali, na mazungumzo yao yaliamsha upya kupendezwa kwake.
5 Ni pendeleo kukweza jina la Yehova. Kwa kuonyesha bidii yetu katika kazi ya kuhubiri, twaonyesha kwamba hatukosi kusudi la fadhili isiyostahiliwa ya Mungu kwetu. Kwa sababu “sasa ndio wakati wenye kukubalika hasa” kusaidia wengine, na twende popote palipo na watu, tuwatolee ushahidi juu ya “siku ya wokovu” ya Yehova.—2 Kor. 6:1, 2.