Mlio Wazee-Wazee Hubirini Bila Kuacha
1 Watu wanapozeeka, wengi wao hutazamia kustaafu kutoka kazi zao za kilimwengu na kufurahia maisha ya bila mawazo wakati wa miaka yao ibakiyo. Huenda wakahisi kwamba wamefanya kazi ngumu vya kutosha na sasa wanastahili pumziko. Au huenda wakataka tu kufurahia maisha, yale yanayobaki.—Luka 12:19.
2 Tukiwa watumishi wa Yehova tuliojiweka wakfu, tuna mtazamo tofauti kuhusu maisha. Twajua hakuna kustaafu katika utumishi wa Mungu. Mtazamo wetu ni mzuri kwa sababu tuna “tazamio la uhai udumuo milele.” (Yuda 21) Miaka mingi ya ujuzi na uzoefu yaweza kuboresha ufahamu na ufahamu wenye kina wa mtu. Jambo hili lingeweza kumwezesha mtu awe mwenye hekima na mwenye usawaziko zaidi naye aonyeshe uthamini wenye kina zaidi wa maisha. Sifa zote hizi zamnufaisha sana mhudumu wa habari njema.
3 Uzee si kuzeeka kimwili tu; hutia ndani pia mtazamo wa akili wa mtu. Ukitazamia kuishi kwa muda mrefu na ujitahidi kuwa mchanga katika mtazamo wako, uwezekano wa kudumisha yote mawili huenda ukaongezeka. Watu walio wazee-wazee waweza kufanya maisha yao yawe bora kwa kuongeza ujuzi wa kiroho na kuushiriki na wengine.—1 Kor. 9:23.
4 Vielelezo vya Maisha Vilivyo Halisi: Dada mmoja akiwa na umri wa miaka 86, alisema hivi: “Ninapotafakari juu ya miaka 60 ambayo imepita tangu nijifunze kweli, ahadi ya Mungu yenye kuhakikishia hufurika ndani ya moyo wangu. Ndiyo, Yehova ambaye atatenda kwa uaminifu-mshikamanifu kuelekea walio waaminifu-washikamanifu anatuacha tuvune shangwe nyingi.” (Zab. 18:25, NW) Ndugu mmoja aliye mzee-mzee alikumbuka jinsi kifo cha mke wake kilivyokuwa mshtuko mkali sana kwake, na baada ya hapo afya yake ilizorota sana. Yeye alisema hivi: “Hata hivyo kwa fadhili isiyostahiliwa ya Yehova, nilihuishwa vya kutosha hata nikaweza kuingia utumishi wa painia miaka miwili baadaye. Namshukuru Yehova kama nini kwamba afya yangu kwa kweli imepata nafuu kwa kuongeza hivyo utendaji wa kuhubiri!”
5 Ni jambo lenye kustahili pongezi kama nini kwamba wengi kati ya walio wazee-wazee wameazimia kuendelea kuhubiri kadiri afya na nguvu zao zinavyowaruhusu—bila kuacha! Wana sababu nzuri ya kusema kwa mkazo: “Ee Mungu, umenifundisha tokea ujana wangu; nimekuwa nikitangaza miujiza yako hata leo.”—Zab. 71:17.