Kushiriki na Wengine Siri ya Kupata Furaha ya Familia
1 Familia ni sehemu ya msingi ya jamii ya kibinadamu, na familia hutokeza vijiji, majiji, majimbo, na mataifa mazima. Leo sehemu hiyo ya familia iko chini ya mkazo kuliko wakati mwingine wowote. Mavutano yenye nguvu yanaathiri mambo yakitisha kuwako kwa maisha ya familia. Twamshukuru Yehova kadiri gani, Mbuni wa mpango wa familia, kwamba ametuandalia maagizo ili tuweze kupata furaha ya familia! Wale wanaofuata miongozo yake wanaona kwamba matatizo yanapungua na matokeo yanakuwa mafanikio ya familia. Wakati wa Septemba tuna pendeleo la kushiriki na wengine kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia. Chukua hatua ya kwanza kuwafikia watu ukiwa na habari ya maisha ya familia. Uwe mwenye urafiki, chanya, na mwenye ufahamu. Unaweza kusema nini?
2 Ungeweza kuanza kwa kutokeza swali kama vile:
◼ “Je, umetambua kwamba familia nyingi zinaona kuwa jambo gumu kuvumilia mikazo ya maisha? [Ruhusu itikio.] Ripoti zaonyesha kwamba watu wengi huona magumu nyumbani. Unaamini ni nini kingezisaidia familia zipate uthabiti na furaha nyingi zaidi? [Ruhusu itikio.] Kwa kuwa Mungu alianzisha mpango wa familia, je, halingekuwa jambo la busara kuchunguza miongozo ambayo ametoa? [Soma 2 Timotheo 3:16, 17.] Maagizo hayo yenye manufaa yanaonyeshwa katika kitabu hiki, Siri ya Kupata Furaha ya Familia.” Kisha umwulize mtu huyo lile analohisi ni tatizo la kawaida la familia, onyesha sura ambayo inazungumzia tatizo hilo, toa kitabu.
3 Katika ziara ya kurudia, unaweza kufuatia mradi wa kuanzisha funzo la Biblia kwa kusema:
◼ “Nimefikiria yale uliyosema kuhusu habari ya maisha ya familia, nami nimekuletea kitu ambacho nafikiri utakifurahia. [Mwonyeshe broshua Anataka, fungua ukurasa wa 16, na usome maswali sita yaliyo juu.] Bila shaka, kila mmoja katika familia lazima afanye sehemu yake ili kuchangia furaha ya familia. Ikiwa una dakika chache tu, nitakuonyesha jinsi unavyoweza kupata manufaa zaidi kutokana na habari hii.” Kisha anzeni kujifunza somo la 8.
4 Njia nyingine ya kuanzisha mazungumzo ni kutaja tatizo moja, labda kwa kusema:
◼ “Ijapokuwa kila mtu anataka kuhisi uradhi na kutosheka, yaonekana familia nyingi kwa kweli hazijafaulu katika jambo hili. Unafikiri ni nini kingewasaidia wapate furaha ya kweli? [Ruhusu itikio.] Zamani za kale, Biblia ilionyesha aina ya matatizo ambayo tungeona katika familia leo. [Soma 2 Timotheo 3:1-3.] Hata hivyo, Biblia pia huambia familia jambo la kufanya ili kutatua matatizo hayo na kupata furaha yenye kudumu. Kanuni zake zimeonyeshwa katika kitabu hiki, Siri ya Kupata Furaha ya Familia.” Kisha uonyeshe sanduku la kupitia mwishoni mwa sura ihusuyo, soma, na utoe kitabu.
5 Unaporudi, tumia broshua “Anataka” kuanzisha funzo. Ungeweza kusema:
◼ “Nilipendezwa na utayari wako wa kuchunguza kanuni za Biblia zinazohusu maisha ya familia. Mambo yaliyoonwa yameonyesha kwamba matokeo bora zaidi yanapatikana kwa kufuata shauri lenye kutumika lipatikanalo katika Biblia. Haya ni masimulizi mafupi ya sababu ya kuwa hivyo.” Soma fungu la kwanza la somo la 1 katika broshua Anataka, kutia ndani ama Zaburi 1:1-3 ama Isaya 48:17, 18. Fursa ikiruhusu, chunguza kikumbusha cha hilo somo. Jitolee kurudi mjifunze somo lifuatalo pamoja.
6 Kuhusu Michango: Fasihi zetu ni zenye thamani na ni gharama kubwa kuzichapisha, ingawa michango tunayoomba ni ya kiasi sana ikilinganishwa na fasihi nyingine. Ijapokuwa hatupaswi kuonekana kama wauzaji, twapaswa kuwa na mtazamo chanya tunapotaja michango ya kawaida ya fasihi zetu. Watu wengi katika eneo letu hupenda kusoma fasihi zetu na wengi husema kwamba michango tunayoomba kwa ajili ya vitabu na magazeti yetu ni ya kiasi.
7 Kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia kina kichwa chenye kuvutia.
Tumesikia mambo yaliyoonwa ambapo mtu anapata nakala yake kisha anaomba nakala nyingine zaidi kwa ajili ya rafiki na jamaa zake. Dada mmoja aliweza kuangusha vitabu 30 katika eneo la biashara kwa sababu kila wakati aliporudi kwenye ziara ya kwanza, wengine ambao walikuwa wameona kitabu hicho walitaka nakala zao za kitabu hicho au vitabu vingine alivyokuwa navyo. Uwe na nakala za kitabu hiki mwezi huu na utwae fursa zote za kukitoa. Fuatia kupendezwa kokote kunakoonyeshwa ukiwa na mradi wa kuanzisha mafunzo.
8 Na tutie kila jitihada tuwezayo ili kushiriki na wengine siri iongozayo kwenye furaha ya familia—tukifuata maagizo yaliyowekwa katika Neno la Mungu.—Zab. 19:7-10.