“Yehova Ni Msaidiaji Wangu”
1 Yesu alipowapa utume wanafunzi wake wa kwanza, aliwaambia hivi: “Tazama! Mimi ninawatuma nyinyi kama kondoo katikati ya mbwa-mwitu.” (Mt. 10:16) Je, hilo liliwafanya wawe na wasiwasi na kurudi nyuma? La. Baadaye walikuwa na mtazamo unaoelezwa na mtume Paulo alipowaambia Wakristo wenzake hivi: “[Muwe] wenye moyo mkuu na kusema: ‘Yehova ni msaidiaji wangu; hakika sitaogopa. Mwanadamu aweza kunifanya nini?’” (Ebr. 13:6) Walishangilia kuhesabiwa kustahili kutoheshimiwa kwa niaba ya jina la Yesu, nao wakaendelea bila kuacha kufundisha na kutangaza habari njema.—Mdo. 5:41, 42.
2 Leo kazi ya kuhubiri ya ulimwenguni pote iko katika hatua zake za mwisho. Kama tu Yesu alivyotabiri, tumekuwa vyombo vya kuchukiwa na mataifa yote. (Mt. 24:9) Kazi yetu ya kuhubiri imepingwa na kudhihakiwa, na katika sehemu nyingine za dunia, hata imepigwa marufuku. Ikiwa tungekuwa tunakosa imani, tungeogofywa. Hata hivyo, kujua kwamba Yehova ni Msaidiaji wetu hutuburudisha sisi na kutuimarisha tustahimili.
3 Moyo mkuu ni sifa ya kuwa mwenye nguvu, jasiri, shujaa. Ni kinyume cha hofu, haya, woga. Wanafunzi wa Yesu sikuzote wamehitaji moyo mkuu ili kuvumilia. Ni muhimu ikiwa tutaepuka kuvunjwa moyo na mitazamo na matendo ya ulimwengu ulio na uadui na Mungu. Inatia moyo jinsi gani kwetu kufikiri juu ya kielelezo chema cha Yesu, mshindi wa ulimwengu! (Yn. 16:33) Pia, kumbuka mitume ambao walipokabili majaribu makali walitangaza hivi kwa ujasiri: “Lazima sisi tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.”—Mdo. 5:29.
4 Sisi Si Namna Irudiyo Nyuma: Twapaswa kujitahidi kudumisha mtazamo ufaao kuelekea kazi yetu. (Ebr. 10:39) Sikuzote kumbuka kwamba tunatumwa na Yehova ukiwa wonyesho wa upendo na rehema yake kuelekea wanadamu wote. Yeye hawaombi watumishi wake kamwe wafanye jambo lolote ambalo halitimizi kusudi lenye mafaa. Kila tugawiwacho kufanya mwishowe kitakuwa na matokeo mazuri kwa wale wenye kumpenda Mungu.—Rom. 8:28.
5 Mwelekeo wa kutazamia mazuri utatusaidia tufulize kutafuta wenye mfano wa kondoo katika eneo letu. Twaweza kuona ubaridi ambao watu huonyesha kuwa wonyesho wa kuvunjika kwao moyo na hali yao ya kukosa tumaini. Acheni upendo wetu utusukume kuwa wenye kusikitikia na wenye subira. Kila wakati tuangushapo fasihi au kutambua upendezi wowote, mradi wetu wapaswa kuwa kufanya ziara ya kurudia bila kukawia na kuchochea upendezi zaidi. Hatupaswi kutilia shaka uwezo wetu wa kuanzisha funzo la Biblia au kuwa wenye matokeo katika kuliongoza. Badala yake, twapaswa daima na kwa kusali kutafuta msaada wa Yehova na mwelekezo wake, tukiwa na uhakika kwamba atatusaidia.
6 Twaamini kwa uthabiti kwamba Yehova ataichunga kazi hadi ukamilisho wake. (Linganisha Wafilipi 1:6.) Itibari yetu thabiti kwake akiwa Msaidiaji wetu hutuimarisha, ili “tusife moyo katika kufanya lililo bora.”—Gal. 6:9.