Mwe Wenye Moyo Mkuu!
“Mwe wenye moyo mkuu na kusema: ‘Yehova ndiye msaidizi wangu.’”—WAEBRANIA 13:6, NW.
1. Ni ujasiri upi ulioonyeshwa na wale waliojifunza kweli ya Mungu katika karne ya kwanza W.K.?
ILIKUWA karne ya kwanza ya Wakati wa Kawaida wetu. Mesiya aliyengojewa kwa muda mrefu alikuwa amekuja. Alikuwa amewafundisha wanafunzi wake vema na alikuwa ameanzisha kazi muhimu ya kuhubiri. Ulikuwa wakati wa watu kusikia habari njema za Ufalme wa Mungu. Kwa hiyo, wanaume na wanawake waliokuwa wamejifunza kweli walijulisha ujumbe huo wa ajabu kwa ujasiri.—Mathayo 28:19, 20.
2. Kwa nini Mashahidi wa Yehova wahitaji moyo mkuu leo?
2 Ufalme haukusimamishwa katika siku hizo. Lakini Mfalme-Mteule, Yesu Kristo, alikuwa ametoa unabii juu ya kuwapo kwake kwa wakati ujao kusikoonekana katika mamlaka ya Ufalme. Kungetiwa alama na mambo kama vile vita isiyo na kifani, njaa kali, magonjwa ya kipuku, matetemeko ya dunia, na kuhubiriwa kwa habari njema ulimwenguni pote. (Mathayo 24:3-14; Luka 21:10, 11) Tukiwa Mashahidi wa Yehova, twahitaji moyo mkuu ili kukabiliana na hali hizo na mnyanyaso tunaopatwa nao. Kwa hiyo itanufaisha kuzungumzia masimulizi ya Biblia juu ya wapiga mbiu ya Ufalme wenye moyo mkuu wa karne ya kwanza W.K.
Moyo Mkuu wa Kumwiga Kristo
3. Ni nani huandaa kielelezo bora kabisa cha moyo mkuu, na ni nini kilichosemwa juu yake kwenye Waebrania 12:1-3?
3 Yesu Kristo huandaa kielelezo bora kabisa cha moyo mkuu. Baada ya kutaja lile “wingu kubwa” la mashahidi wa Yehova wenye moyo mkuu wa kabla ya Ukristo, mtume Paulo alikazia Yesu kwa kusema hivi: “Kwa kuwa tunazungukwa na wingu kubwa la mashahidi namna hii, na tuweke kando kila mzigo mzito, na dhambi ile ituzingayo kwa upesi; na tupige mbio kwa saburi katika yale mashindano yaliyowekwa mbele yetu, tukimtazama Yesu, mwenye kuanzisha na mwenye kutimiza imani yetu; ambaye kwa ajili ya furaha iliyowekwa mbele yake aliustahimili msalaba [mti wa mateso, NW] na kuidharau aibu, naye ameketi mkono wa kuume wa kiti cha enzi cha Mungu. Maana mtafakarini sana yeye aliyeyastahimili mapingamizi makuu namna hii ya watendao dhambi juu ya nafsi zao, msije mkachoka, mkizimia mioyoni mwenu.”—Waebrania 12:1-3.
4. Yesu alionyeshaje moyo mkuu aliposhawishwa na Shetani?
4 Baada ya ubatizo wake na siku 40 za kutafakari, kusali, na kufunga kula akiwa jangwani, Yesu alimpinga Shetani kwa uhodari. Aliposhawishwa na Ibilisi kugeuza mawe kuwa mkate, Yesu alikataa kwa sababu haikufaa kufanya muujiza ili kuridhisha tamaa ya kibinafsi. “Imeandikwa,” akasema Yesu, “Mtu hataishi kwa mkate tu, ila kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Mungu.” Shetani alipomtolea mwito aruke kutoka kinara cha hekalu, Yesu alikataa kwa sababu kungalikuwa dhambi kumshawishi Mungu amwokoe kutoka ule ulioelekea kuwa ujiuaji. “Tena imeandikwa,” Kristo akasema, “Usimjaribu Bwana Mungu wako.” Shetani alimtolea falme zote za ulimwengu kwa ajili ya “tendo [moja] la ibada,” (NW) lakini Yesu hangeasi imani na kuunga mkono dhihaka la Ibilisi kwamba wanadamu hawangebaki wakiwa waaminifu kwa Mungu wakiwa chini ya mtihani. Kwa hiyo Yesu alijulisha hivi: “Nenda zako, Shetani; kwa maana imeandikwa, Msujudie Bwana [Yehova, NW] Mungu wako, umwabudu yeye peke yake.” Ndipo, yule Mshawishi “akamwacha akaenda zake kwa muda [hadi wakati mwingine unaofaa, NW].”—Mathayo 4:1-11; Luka 4:13.
5. Ni nini kiwezacho kutusaidia tustahimili kishawishi?
5 Yesu alijitiisha kwa Yehova na alimpinga Shetani. Sisi ‘tukijitiisha kwa Mungu vivyo hivyo na kumpinga Ibilisi, yeye atatukimbia.’ (Yakobo 4:7, NW) Kama vile Yesu, twaweza kustahimili kishawishi kwa moyo mkuu tukiyatumia Maandiko, labda hata kuyanukuu wakati ule tunaposhawishwa kufanya jambo fulani lenye dhambi. Je! yaelekea kwamba tutashindwa na kishawishi cha kufanya wizi ikiwa wakati huo twajikariria sheria ya Mungu: “Usiibe”? Je! Wakristo wawili wataelekea kuangukia ukosefu wa adili katika ngono ikiwa hata mmoja wao anukuu kwa moyo mkuu neno: “Usizini”?—Warumi 13:8-10; Kutoka 20:14, 15.
6. Yesu alikuwaje mshindi wa ulimwengu mwenye moyo mkuu?
6 Tukiwa Wakristo wanaochukiwa na ulimwengu huu, twaweza kuepuka roho na mwenendo wao wenye dhambi. Yesu aliwaambia wafuasi wake: “Ulimwenguni mnayo dhiki; lakini jipeni moyo; mimi nimeushinda ulimwengu.” (Yohana 16:33) Aliushinda ulimwengu kwa kutokuwa kama huo. Kielelezo chake akiwa mshindi na tokeo la mwendo wake wa kushika uaminifu-maadili waweza kutujaza moyo mkuu wa kumwiga kwa kubaki tukiwa tumejitenga na ulimwengu huu na kutotiwa unajisi nao.—Yohana 17:16.
Moyo Mkuu wa Kuendelea Kuhubiri
7, 8. Ni nini kitakachotusaidia tuendelee kuhubiri ujapokuwa mnyanyaso?
7 Yesu na wanafunzi wake walimtegemea Mungu ili kupata moyo mkuu wa kuendelea kuhubiri ujapokuwa mnyanyaso. Kristo alitimiza huduma yake kwa ujasiri ujapokuwa mnyanyaso, na baada ya Pentekoste 33 W.K., wafuasi wake walionyanyaswa waliendelea kupiga mbiu ya habari njema hata ingawa viongozi wa kidini wa Kiyahudi walijaribu kuwazuia. (Matendo 4:18-20; 5:29) Wanafunzi hao walisali hivi: “Bwana [Yehova, NW], yaangalie matisho yao; ukawajalie watumwa wako kunena neno lako kwa ujasiri wote.” Na ni nini kilichotukia? “Walipokwisha kumwomba Mungu, mahali pale walipokusanyika pakatikiswa,” simulizi lasema, “wote wakajaa Roho Mtakatifu [roho takatifu, NW], wakanena neno la Mungu kwa ujasiri.”—Matendo 4:24-31.
8 Kwa kuwa watu walio wengi leo hawaitikii habari njema, mara nyingi ujasiri hutakwa ili kuendelea kuwahubiri. Hasa wanaponyanyaswa, watumishi wa Yehova huhitaji moyo mkuu wa kupewa na Mungu ili kutoa ushahidi kamili. (Matendo 2:40; 20:24) Kwa hiyo yule mpiga mbiu ya Ufalme mwenye moyo mkuu Paulo alimwambia hivi mfanyakazi mwenzake kijana, aliyekuwa na maarifa kidogo zaidi: “Mungu hakutupa roho ya woga, bali ya nguvu na ya upendo na ya moyo wa kiasi. Basi usiuonee haya ushuhuda wa Bwana wetu, wala usinionee haya mimi mfungwa wake, bali uvumilie mabaya pamoja nami kwa ajili ya Injili, kwa kadiri ya nguvu ya Mungu.” (2 Timotheo 1:7, 8) Tukisali ili kupata moyo mkuu, tutaweza kuendelea kuhubiri, na hata mnyanyaso hautatunyang’anya shangwe yetu tukiwa wapiga mbiu ya Ufalme.—Mathayo 5:10-12.
Moyo Mkuu wa Kujipanga Upande wa Yehova
9, 10. (a) Wayahudi na wasio Wayahudi wa karne ya kwanza walifanya nini ili kuwa wafuasi wa Kristo waliobatizwa? (b) Kwa nini kuwa Mkristo kulitaka moyo mkuu?
9 Wayahudi na wasio Wayahudi wengi wa karne ya kwanza waliacha mapokeo yasiyo ya kimaandiko kwa moyo mkuu ili kuwa wafuasi wa Kristo waliobatizwa. Muda mfupi baada ya Pentekoste 33 W.K., “hesabu ya wanafunzi i[li]zidi sana katika Yerusalemu; jamii kubwa ya makuhani wakaitii ile Imani.” (Matendo 6:7) Wayahudi hao walikuwa na moyo mkuu wa kuvunja vifungo vya kidini na kumkubali Yesu kuwa Mesiya.
10 Kuanzia 36 W.K., wasio Wayahudi wengi walikuja kuwa waamini. Wakati Kornelio, washiriki wa familia yake, na wasio Wayahudi wengine waliposikia habari njema, waliikubali upesi, wakapokea roho takatifu, na ‘kubatizwa kwa jina la Yesu Kristo.’ (Matendo 10:1-48) Katika Filipi mlinzi wa gereza mmoja Asiye Myahudi pamoja na nyumba yake walikubali Ukristo upesi, “kisha akabatizwa, yeye na watu wake wote wakati uo huo.” (Matendo 16:25-34) Moyo mkuu ulitakwa ili kuchukua hatua hizo kwa sababu Wakristo walikuwa watu wachache wenye kunyanyaswa, waliochukiwa na wengi. Wangali hivyo. Lakini ikiwa hujajiweka wakfu kwa Mungu na kubatizwa kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, je, huu si wakati wako wa kuchukua hatua hizo zenye moyo mkuu?
Moyo Mkuu Katika Nyumba Zilizogawanyika
11. Eunike na Timotheo waliandaa vielelezo vipi vyema vya moyo mkuu?
11 Eunike na mwanae Timotheo waliweka vielelezo vyema vya imani yenye moyo mkuu katika nyumba iliyogawanyika kidini. Ingawa Eunike alikuwa na mume mpagani, alimfundisha mwanae “maandiko matakatifu” tangu utoto wake. (2 Timotheo 3:14-17) Alipokuwa Mkristo, alidhihirisha ‘imani isiyo na unafiki.’ (2 Timotheo 1:5) Alikuwa pia na moyo mkuu wa kumpa Timotheo mafundisho ya Kikristo huku akionyesha staha kwa ajili ya ukichwa wa mume wake asiye mwamini. Kwa hakika, imani na moyo mkuu wake ulithawabishwa wakati mwanae aliyefundishwa vema alipochaguliwa kuandamana na Paulo katika safari za mishonari. Hilo laweza kuwatia moyo kama nini wazazi Wakristo wanaojipata wenyewe katika hali kama hizo!
12. Timotheo alikuja kuwa mtu wa aina gani, na ni nani wanaothibitika kuwa kama yeye sasa?
12 Ingawa Timotheo aliishi katika nyumba iliyogawanyika kidini, alikubali Ukristo kwa moyo mkuu akawa mtu wa kiroho ambaye Paulo angeweza kusema hivi juu yake: “Natumaini katika Bwana Yesu kumtuma Timotheo afike kwenu [Wafilipi] karibu, nifarijiwe na mimi, nikiijua hali yenu. Maana sina mtu mwingine mwenye nia moja nami, atakayeiangalia hali yenu kweli kweli. . . . Mwajua sifa yake, ya kuwa ametumika pamoja nami kwa ajili ya Injili, kama mwana na baba yake.” (Wafilipi 2:19-22) Leo, wavulana na wasichana wengi katika nyumba zilizogawanyika kidini hukubali Ukristo wa kweli kwa uhodari. Kama vile Timotheo, wao wanatoa uthibitisho juu yao wenyewe, na sisi twashangilia kama nini kwamba wao ni sehemu ya tengenezo la Yehova!
Moyo Mkuu wa ‘Kuwa Tayari Hata Kukatwa Kichwa’
13. Akila na Prisila walionyesha moyo mkuu kwa njia gani?
13 Akila na mke wake, Prisila (Priska), waliweka kielelezo kwa ‘kuwa tayari kukatwa kichwa’ kwa ajili ya mwamini mwenzao. Walimpokea Paulo nyumbani mwao, wakafanya kazi naye katika kutengeneza mahema, na kumsaidia kujenga lile kutaniko jipya katika Korintho. (Matendo 18:1-4) Katika urafiki wao wa miaka 15, hata walihatarisha maisha zao kwa niaba yake kwa njia isiyofunuliwa. Walikuwa wakiishi katika Roma alipowaambia Wakristo huko hivi: “Nisalimieni Priska na Akila, watenda kazi pamoja nami katika Kristo Yesu; waliokuwa tayari hata kukatwa kichwa kwa ajili ya maisha yangu; ambao ninawashukuru, wala si mimi tu, ila na makanisa [makutaniko, NW] ya Mataifa yote pia.”—Warumi 16:3, 4.
14. Kwa kuwa tayari hata kukatwa kichwa kwa ajili ya Paulo, Akila na Priska walikuwa wakitenda kulingana na amri gani?
14 Kwa kuwa tayari hata kukatwa kichwa kwa ajili ya Paulo, Akila na Priska walitenda kulingana na maneno ya Yesu: “Amri mpya nawapa, Mpendane. Kama vile nilivyowapenda ninyi, nanyi mpendane vivyo hivyo.” (Yohana 13:34) Amri hiyo ilikuwa “mpya” kwa kuwa ilipita takwa la Sheria ya Kimusa kwamba mtu ampende jirani yake kama alivyojipenda mwenyewe. (Mambo ya Walawi 19:18) Ilitaka upendo wa kujidhabihu ambao ungefikia hatua ya mtu kutoa uhai wake kwa ajili ya wengine, kama vile Yesu alivyofanya. Mwandikaji Tertuliano wa karne ya pili na ya tatu W.K. alinukuu maneno ya watu wa kilimwengu kuhusu Wakristo alipoandika hivi: “‘Tazama,’ [walimwengu] husema, ‘jinsi [Wakristo] wanavyopendana mmoja na mwenzake . . . na namna walivyo tayari kufa kwa ajili ya mmoja na mwenzake.’” (Apology, sura 39, 7) Hasa kati ya mnyanyaso ndipo huenda tukawa na wajibu wa kuonyesha upendo wa kidugu kwa kuhatarisha maisha zetu kwa moyo mkuu ili kuepuka kuwafunua waamini wenzetu wapatwe na ukatili au kifo mikononi mwa adui.—1 Yohana 3:16.
Moyo Mkuu Huleta Shangwe
15, 16. Kama ionyeshwavyo katika Matendo sura 16, moyo mkuu na shangwe zaweza kuhusianishwaje?
15 Paulo na Sila waandaa ithibati kwamba kuonyesha moyo mkuu kati ya majaribu kwaweza kuleta shangwe. Kwa amri ya maofisa-hakimu wa kesi za raia katika jiji la Filipi, walipigwa kwa fito hadharani na kutiwa katika mikatale ya gereza. Lakini, hawakujikunyata kwa hofu kwa kukata tamaa. Zijapokuwa hali zao zenye kujaribu, bado walikuwa na moyo mkuu wa kupewa na Mungu pamoja na shangwe ambayo huo huwaletea Wakristo waaminifu.
16 Karibu usiku wa manane, Paulo na Sila walikuwa wakisali na kumsifu Mungu kwa wimbo. Kwa ghafula, tetemeko la dunia lilitikisa gereza, likalegeza vifungo vyao, na kuifungua milango. Mlinzi wa gereza mwenye hofu kuu pamoja na familia yake walitolewa ushahidi wenye ujasiri ulioongoza kwenye ubatizo wao kuwa watumishi wa Yehova. Yeye mwenyewe ‘alifurahi sana, yeye na nyumba yake yote, maana alikuwa amekwisha kumwamini Mungu.’ (Matendo 16:16-34) Hilo lazima liliwaletea Paulo na Sila shangwe iliyoje! Baada ya kuzungumzia kielelezo hicho na vinginevyo vya Kimaandiko vya moyo mkuu, twaweza kubakije tukiwa wenye moyo mkuu tukiwa watumishi wa Yehova?
Endeleeni Kuwa Wenye Moyo Mkuu
17. Kama ionyeshwavyo katika Zaburi 27, kumtumaini Yehova kunahusikaje na moyo mkuu?
17 Kumtumaini Yehova kutatusaidia tubaki tukiwa wenye moyo mkuu. Daudi aliimba hivi: “Umtumaini Yehova; uwe mwenye moyo mkuu na uache moyo wako uwe wenye nguvu. Ndiyo, umtumaini Yehova.” (Zaburi 27:14, NW) Zaburi 27 yaonyesha kwamba Daudi alimtegemea Yehova kuwa “ngome” ya uhai wake. (Mstari 1) Akiwa amekwisha kuona jinsi Mungu alivyoshughulika na maadui wa Daudi katika wakati uliopita kulimpa yeye moyo mkuu. (Mistari 2, 3) Uthamini kuelekea kitovu cha ibada cha Yehova ulikuwa jambo jingine. (Mstari 4) Kuitibari msaada wa Yehova, ulinzi wake, na kukombolewa naye kulijenga moyo mkuu wa Daudi pia. (Mistari 5-10) Jambo lililokuwa lenye msaada pia ni maagizo yenye kuendelea katika kanuni za njia ya Yehova yenye uadilifu. (Mstari 11) Sala yenye uhakika kuomba ili kupata kukombolewa kutoka kwa maadui wake, pamoja na imani na tumaini, kulimsaidia Daudi awe mwenye moyo mkuu. (Mistari 12-14) Twaweza kujenga moyo mkuu wetu katika njia kama hizo, hivyo tukionyesha kwamba kwa kweli ‘twamtumaini Yehova.’
18. (a) Ni nini kionyeshacho kwamba ushirika wa kawaida pamoja na waabudu wa Yehova wenzetu waweza kutusaidia kubaki tukiwa wenye moyo mkuu? (b) Mikutano ya Kikristo ina daraka jipi katika kujenga moyo mkuu?
18 Ushirika wa kawaida pamoja na waabudu wa Yehova wenzetu waweza kutusaidia tubaki tukiwa wenye moyo mkuu. Paulo alipokata rufani kwa Kaisari na alikuwa akisafiri kwenda Roma, waamini wenzake walimlaki kwenye Soko la Apio na Mikahawa Mitatu. “Paulo alipowaona,” simulizi hilo lasema, “alimshukuru Mungu, akachangamka [akawa na moyo mkuu, NW].” (Matendo 28:15) Tuhudhuriapo mitukano ya Kikristo kwa kawaida, twatii shauri hili la Paulo: “Tukaangaliane sisi kwa sisi na kuhimizana katika upendo na kazi nzuri; wala tusiache kukusanyika pamoja, kama ilivyo desturi ya wengine; bali tuonyane [kutiana moyo, NW]; na kuzidi kufanya hivyo, kwa kadiri mwonavyo siku ile kuwa inakaribia.” (Waebrania 10:24, 25) Kutiana moyo kwamaanisha nini? Kutia moyo humaanisha “kuchochea [mtu awe] na moyo mkuu, nguvu, au tumaini.” (Webster’s Ninth New Collegiate Dictionary) Twaweza kufanya mengi kuwachochea Wakristo wengine kwa moyo mkuu, na kitia-moyo chao chaweza vilevile kujenga sifa hiyo ndani yetu.
19. Maandiko na vichapo vya Kikristo vinahusikaje na kubaki kwetu tukiwa wenye moyo mkuu?
19 Ili kubaki tukiwa wenye moyo mkuu, ni lazima tujifunze Neno la Mungu kwa kawaida na kutumia shauri lalo maishani mwetu. (Kumbukumbu la Torati 31:9-12; Yoshua 1:8) Funzo letu la kawaida lapaswa kutia ndani vichapo vya Kikristo vyenye msingi wa Maandiko, kwa kuwa shauri timamu linaloandaliwa hivyo litatusaidia kukabili mitihani ya imani kwa moyo mkuu wa kupewa na Mungu. Kutokana na masimulizi ya Biblia, tumeona jinsi watumishi wa Yehova wamekuwa wenye moyo mkuu katika hali mbalimbali. Hivi sasa, huenda tusijue jinsi habari hiyo iwezavyo kutusaidia, lakini Neno la Mungu lina nguvu, na yale tunayojifunza kutokana nalo yaweza kutunufaisha sikuzote. (Waebrania 4:12) Mathalani, iwapo hofu ya mwanadamu yaanza kuathiri huduma yetu, twaweza kukumbuka jinsi Henoko alivyokuwa na moyo mkuu wa kutoa ujumbe wa Mungu kwa wale wasiomcha Mungu.—Yuda 14, 15.
20. Kwa nini yaweza kusemwa kwamba sala ni muhimu ikiwa tutabaki tukiwa wenye moyo mkuu tukiwa watumishi wa Yehova?
20 Ili kubaki wenye moyo mkuu tukiwa watumishi wa Yehova, ni lazima tudumu katika sala. (Warumi 12:12) Yesu alivumilia majaribu yake kwa moyo mkuu kwa sababu alitoa “maombi na dua pamoja na kulia sana na machozi, akasikilizwa kwa jinsi alivyokuwa mcha Mungu.” (Waebrania 5:7) Kwa kubaki karibu na Mungu katika sala, hatutakuwa kama waoga wa kilimwengu ambao mwishoni watapatwa na “kifo cha pili” ambacho katika hicho hakuna ufufuo. (Ufunuo 21:8) Ulinzi wa kimungu na uhai katika ulimwengu mpya wa Mungu ni wa watumishi wake wenye moyo mkuu.
21. Kwa nini Mashahidi wa Yehova waaminifu-washikamanifu waweza kuwa wenye moyo mkuu?
21 Tukiwa Mashahidi wa Yehova waaminifu-washikamanifu, hatuhitaji kuhofu maadui wa kishetani na wa kibinadamu, kwani tuna utegemezo wa Mungu na kielelezo cha Yesu chenye moyo mkuu akiwa mshindi wa ulimwengu. Ushirika wenye kujenga kiroho pamoja na watu wa Yehova watusaidia vilevile tuwe wenye moyo mkuu. Moyo mkuu wetu unajengwa pia kupitia mwongozo na shauri la Maandiko na vichapo vya Kikristo. Na masimulizi ya Biblia juu ya watumishi wa Mungu wa wakati uliopita hutusaidia tutembee katika njia zake kwa moyo mkuu. Kwa hiyo katika siku hizi zenye hatari, acheni tusonge mbele katika utumishi mtakatifu kwa ujasiri. Ndiyo, acheni watu wa Yehova wote wawe wenye moyo mkuu!
Ungejibuje?
◻ Kielelezo cha Yesu chaweza kutujazaje moyo mkuu?
◻ Ni nini kilichompa Yesu na wanafunzi wake moyo mkuu wa kuendelea kuhubiri?
◻ Kwa nini Wayahudi na wasio Wayahudi walihitaji moyo mkuu ili kujipanga upande wa Yehova?
◻ Ni vielelezo vipi vya moyo mkuu vilivyoandaliwa na Eunike na Timotheo?
◻ Kuna ithibati gani kwamba moyo mkuu huleta shangwe hata kati ya mnyanyaso?
[Picha katika ukurasa wa 18]
Kama vile Yesu, twaweza kustahimili kishawishi tukiyatumia na kuyanukuu Maandiko