Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w93 11/15 kur. 12-17
  • Tembeeni Katika Njia za Yehova kwa Moyo Mkuu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Tembeeni Katika Njia za Yehova kwa Moyo Mkuu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Maana ya Moyo Mkuu
  • Moyo Mkuu wa Kujulisha Ujumbe wa Mungu
  • Moyo Mkuu Chini ya Jaribu
  • Moyo Mkuu wa Kumtii Mungu
  • Moyo Mkuu wa Kusimama Pamoja na Watu wa Mungu
  • Moyo Mkuu wa ‘Kumfuata Yehova Kikamili’
  • Moyo Mkuu wa Kumwitibari (Kumtumaini) Mungu
  • Moyo Mkuu wa Kumheshimu Yehova na Kuendeleza Ibada Safi
  • “Uwe Hodari na Mwenye Nguvu Sana”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
  • Mwe Wenye Moyo Mkuu!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Uwe Hodari Yehova Yupo Pamoja Nawe!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
  • “Uwe Hodari . . . Nawe Utende”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2017
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
w93 11/15 kur. 12-17

Tembeeni Katika Njia za Yehova kwa Moyo Mkuu

“Mwenye furaha ni kila mtu ahofuye Yehova, anayetembea katika njia zake.”—ZABURI 128:1, NW.

1, 2. Maandishi ya Kibiblia ya maneno na matendo ya mashahidi wa mapema wa Yehova ni ya msaada gani?

NENO Takatifu la Yehova limejaa masimulizi juu ya majaribu na shangwe za watumishi wake waaminifu-washikamanifu. Maono ya Noa, Abrahamu, Sara, Yoshua, Debora, Baraka, Daudi, na wengine ni wazi sana na yenye kutokeza ndani yalo. Wote hao walikuwa watu halisi wenye jambo fulani la pekee lililofanana. Walikuwa na imani katika Mungu na walitembea katika njia zake kwa moyo mkuu.

2 Maneno na matendo ya mashahidi wa mapema wa Yehova yaweza kuwa yenye kitia-moyo kwetu tujitahidipo kutembea katika njia za Mungu. Zaidi ya hayo, tutakuwa na furaha tuonyeshapo staha kwa Mungu na hofu ifaayo ya kutompendeza. Hilo ni kweli ingawa twakabili majaribu maishani, kwani mtunga-zaburi aliyepuliziwa aliimba hivi: “Mwenye furaha ni kila mtu ahofuye Yehova, anayetembea katika njia zake.”—Zaburi 128:1, NW.

Maana ya Moyo Mkuu

3. Moyo mkuu ni nini?

3 Ili kutembea katika njia za Yehova, ni lazima tuwe na moyo mkuu. Kwa kweli, Maandiko huwaamuru watu wa Mungu kuonyesha sifa hiyo. Mathalani, mtunga-zaburi Daudi aliimba hivi: “Iweni hodari [wenye moyo mkuu, NW], mpige moyo konde, ninyi nyote mnaomngoja BWANA [Yehova, NW].” (Zaburi 31:24) Moyo mkuu ni “nguvu za akilini au za kiadili za kujasiria, kudumu, na kustahimili hatari, hofu, au ugumu.” (Webster’s Ninth New Collegiate Dictionary) Mtu mwenye moyo mkuu ni mwenye nguvu, mwenye ujasiri, hodari. Kwamba Yehova huwapa watumishi wake moyo mkuu ni wazi kutokana na maneno haya ya mtume Paulo kwa mfanyakazi mwenzake Timotheo: “Mungu hakutupa roho ya woga, bali ya nguvu na ya upendo na ya moyo wa kiasi.”—2 Timotheo 1:7.

4. Njia moja ya kupata moyo mkuu ni gani?

4 Njia moja ya kupata moyo mkuu wa kupewa na Mungu ni kutolea Neno la Yehova, Biblia, ufikirio wenye sala. Masimulizi mengi yaliyo katika Maandiko yaweza kutusaidia kuwa wenye moyo mkuu zaidi. Kwa hiyo, acheni kwanza tuone yale tuwezayo kujifunza kutokana na maandishi katika Maandiko ya Kiebrania juu ya watu fulani waliotembea katika njia za Yehova kwa moyo mkuu.

Moyo Mkuu wa Kujulisha Ujumbe wa Mungu

5. Moyo mkuu wa Henoko waweza kuwanufaishaje watumishi wa Yehova wa siku hizi?

5 Moyo mkuu wa Henoko waweza kuwasaidia watumishi wa Yehova wa leo waseme ujumbe wa Mungu kwa moyo mkuu. Kabla ya Henoko kuzaliwa, “mwanzo ulifanywa wa kuita juu ya jina la Yehova.” Wasomi wengine husema kwamba watu ‘walianza kwa unajisi’ kuita juu ya jina la Yehova. (Mwanzo 4:25, 26; 5:3, 6, NW) Huenda ikawa jina la kimungu lilikuwa likitumiwa kwa wanadamu au hata kwa sanamu. Kwa hiyo, dini bandia ilikuwa ikisitawi Henoko alipozaliwa katika 3404 K.W.K. Kwa kweli, yaonekana kuwa yeye alikuwa peke yake katika ‘kutembea pamoja na Mungu,’ akifuatia mwendo mwadilifu uliopatana na kweli ya Yehova iliyofunuliwa.—Mwanzo 5:18, 24, NW.

6. (a) Henoko alijulisha ujumbe upi wenye nguvu? (b) Twaweza kuwa na uhakika gani?

6 Henoko alitoa ujumbe wa Mungu kwa moyo mkuu, yaelekea kwa kuhubiri. (Waebrania 11:5; linganisha 2 Petro 2:5.) Shahidi huyo aliyekuwa peke yake alijulisha hivi: “Angalia, Bwana [Yehova, NW] alikuja na watakatifu wake, maelfu maelfu, ili afanye hukumu juu ya watu wote, na kuwaadhibisha wote wasiomcha Mungu, kwa ajili ya kazi zao zote za upotevu walizozitenda bila kumcha Mungu, na kwa ajili ya maneno magumu yote ambayo hao wenye dhambi wasiomcha Mungu wameyanena juu yake.” (Yuda 14, 15) Henoko alikuwa na moyo mkuu wa kutumia jina la Yehova alipokuwa akitoa ujumbe huo wa kuwalaani vikali wale wasiomcha Mungu. Na kama vile Mungu alivyompa Henoko moyo mkuu wa kujulisha ujumbe huo wenye nguvu, ndivyo Yehova amewatia nguvu Mashahidi Wake wa siku hizi waseme neno Lake kwa ujasiri katika huduma, shuleni, na kwingineko.—Linganisha Matendo 4:29-31.

Moyo Mkuu Chini ya Jaribu

7. Noa aandaa kielelezo kipi cha moyo mkuu?

7 Kielelezo cha Noa chaweza kutusaidia tuwe wenye moyo mkuu katika kufanya matendo yenye uadilifu tunapokuwa chini ya jaribu. Kwa moyo mkuu na imani, alitenda kulingana na onyo la kimungu juu ya furiko la duniani pote na “aliunda safina, apate kuokoa nyumba yake.” Kwa matendo ya utii na yenye uadilifu, Noa aliulaani vikali ulimwengu wa wasioamini kwa sababu ya matendo yao maovu na aliuthibitisha kuwa wenye kustahili uharibifu. (Waebrania 11:7; Mwanzo 6:13-22; 7:16) Kutafakari juu ya mwendo wa Noa husaidia watumishi wa Mungu wa ki-siku-hizi washiriki kwa moyo mkuu katika matendo yenye uadilifu kama vile huduma ya Kikristo.

8. (a) Noa alikabili nini akiwa “mhubiri wa uadilifu” mwenye moyo mkuu? (b) Yehova atatufanyia nini tukiwa wahubiri wa uadilifu wenye moyo mkuu?

8 Ikiwa tunafuatia mwendo mwadilifu lakini hatujui jinsi ya kushughulika na jaribu fulani, acheni tusali ili kupata hekima ya kukabiliana nalo. (Yakobo 1:5-8) Uaminifu-mshikamanifu wa Noa kwa Mungu akiwa chini ya mtihani waonyesha kwamba inawezekana kukabili majaribu kwa moyo mkuu na uaminifu. Yeye alistahimili msongo kutoka ulimwengu mwovu na kutoka kwa malaika waliojivika miili na wazao wao waliokuwa mivyauso (muungano wa jamii mbalimbali). Ndiyo, Noa alikuwa “mhubiri wa uadilifu” mwenye moyo mkuu kwa “ulimwengu wa kale” uliokuwa ukielekea kwenye uharibifu. (2 Petro 2:4, 5, NW; Mwanzo 6:1-9) Ingawa alisema kwa ujasiri akiwa mtangazaji mwenye kupiga mbiu juu ya onyo la Mungu kwa wale walioishi kabla ya furiko, ‘hawakutambua, hata Gharika ikaja, ikawachukua wote.’ (Mathayo 24:36-39) Lakini acheni tukumbuke kwamba ujapokuwa mnyanyaso na kukataliwa mbali kwa ujumbe wetu wenye msingi wa Biblia na watu walio wengi leo, Yehova atatutegemeza kama alivyomtegemeza Noa tukionyesha imani na moyo mkuu uleule tukiwa wahubiri wa uadilifu.

Moyo Mkuu wa Kumtii Mungu

9, 10. Abrahamu, Sara, na Isaka walionyesha utii wenye moyo mkuu kuhusu mambo gani?

9 “Rafiki wa Mungu [Yehova, NW]” Abrahamu ni kielelezo chema cha utii wenye moyo mkuu kwa Mungu. (Yakobo 2:23) Abrahamu alihitaji imani na moyo mkuu ili kumtii Yehova na kuondoka Uru wa Wakaldayo, jiji lenye faida nyingi za kimwili. Aliamini ahadi ya Mungu kwamba “jamaa zote za dunia” zingejibariki zenyewe kupitia yeye na kwamba mbegu yake ingepewa bara. (Mwanzo 12:1-9; 15:18-21) Kwa imani Abrahamu “alikaa ugenini katika ile nchi ya ahadi” akautazamia “mji wenye misingi [halisi, NW]”—Ufalme wa Mungu wa kimbingu, ambao chini yao angefufuliwa kwenye uhai duniani.—Waebrania 11:8-16.

10 Mke wa Abrahamu, Sara, alikuwa na imani na moyo mkuu uliohitajiwa ili kuondoka Uru, kuandamana na mume wake hadi bara la kigeni, na kuvumilia magumu yoyote ambayo wangekabili huko. Na alithawabishwa kama nini kwa ajili ya utii wake kwa Mungu wenye moyo mkuu! Ingawa alikuwa tasa mpaka miaka 90 hivi na ‘kupita umri,’ Sara alitiwa nguvu ‘ya kuwa na mimba, kwa kuwa alimhesabu yeye aliyeahidi kuwa mwaminifu.’ Hatimaye, akamzaa Isaka. (Waebrania 11:11, 12, Habari Njema kwa Watu Wote; Mwanzo 17:15-17; 18:11; 21:1-7) Miaka kadhaa baadaye, Abrahamu alimtii Mungu kwa moyo mkuu ‘na ni kana kwamba alimtoa Isaka.’ (NW) Kwa kuzuiwa na malaika, babu wa ukoo huyo alimpokea mwana wake mwenye moyo mkuu na aliye mtiifu kutoka katika kifo “kwa mfano.” Hivyo yeye na Isaka walionyesha kiunabii kwamba Yehova Mungu angeandaa Mwanae, Yesu Kristo, kuwa fidia ili wale wazoeao imani katika yeye waweze kuwa na uhai wa milele. (Waebrania 11:17-19; Mwanzo 22:1-19; Yohana 3:16) Kwa hakika, utii wenye moyo mkuu wa Abrahamu, Sara, na Isaka wapaswa utusukume kumtii Yehova na kufanya mapenzi yake sikuzote.

Moyo Mkuu wa Kusimama Pamoja na Watu wa Mungu

11, 12. (a) Musa alionyeshaje moyo mkuu kuhusu watu wa Yehova? (b) Kwa sababu ya moyo mkuu wa Musa, ni swali jipi liwezalo kuulizwa?

11 Musa alichukua msimamo wake kwa moyo mkuu pamoja na watu wa Mungu walioonewa. Katika karne ya 16 K.W.K., wazazi wa Musa wenyewe walionyesha moyo mkuu. Bila kuhofu amri ya mfalme ya kuua watoto wa kiume Waebrania waliotoka kuzaliwa, walimficha Musa, kisha wakamweka ndani ya kisafina kati ya matete kando ya mto Naili. Kwa kupatikana na binti ya Farao, alilelewa kama mwana wake mwenyewe, ingawa kwanza alipokea mazoezi ya kiroho katika nyumba ya wazazi wake. Akiwa sehemu ya nyumba ya Farao, Musa ‘alifundishwa hekima yote ya Wamisri’ akawa “hodari wa maneno na matendo,” mwenye nguvu katika uwezo mbalimbali wa kiakili na kimwili.—Matendo 7:20-22; Kutoka 2:1-10; 6:20.

12 Zijapokuwa faida za kimwili za nyumba ya kifalme, Musa alichagua kuchukua msimamo wake kwa moyo mkuu pamoja na waabudu wa Yehova, ambao wakati huo walikuwa wametiwa utumwani na Wamisri. Kwa kumkinga Mwisraeli mmoja, alimuua Mmisri kisha akakimbia hadi Midiani. (Kutoka 2:11-15) Miaka 40 hivi baadaye, Mungu alimtumia kuongoza Waisraeli kutoka utumwani. Wakati huo Musa ‘aliondoka Misri, asiogope ghadhabu ya mfalme,’ aliyemtisha kwa kifo kwa sababu ya kumwakilisha Yehova kwa niaba ya Israeli. Musa alitembea kana kwamba alimwona “yeye asiyeonekana,” Yehova Mungu. (Waebrania 11:23-29; Kutoka 10:28) Je! wewe una imani na moyo mkuu wa jinsi hiyo hivi kwamba utashikamana na Yehova na watu wake ujapokuwa ugumu na mnyanyaso?

Moyo Mkuu wa ‘Kumfuata Yehova Kikamili’

13. Yoshua na Kalebu walitoaje vielelezo vya moyo mkuu?

13 Yoshua na Kalebu wenye moyo mkuu waliandaa ithibati kwamba twaweza kutembea katika njia za Mungu. “Walimfuata Yehova kikamili.” (Hesabu 32:12, NW) Yoshua na Kalebu walikuwa miongoni mwa wale wanaume 12 waliotumwa kupeleleza Bara Lililoahidiwa. Kwa kuwahofu wakazi walo, wapelelezi kumi walijaribu kushawishi Israeli wasiingie Kanaani. Hata hivyo, Yoshua na Kalebu walisema hivi kwa moyo mkuu: “Ikiwa BWANA [Yehova, NW] anatufurahia, atatuingiza katika nchi hii atupe iwe yetu, nayo ni nchi yenye wingi wa maziwa na asali. Lakini msimwasi BWANA [Yehova, NW], wala msiwaogope wale wenyeji wa nchi, maana wao ni chakula kwetu; uvuli uliokuwa juu yao umeondolewa, naye BWANA [Yehova, NW] yu pamoja nasi; msiwaogope.” (Hesabu 14:8, 9) Kwa kukosa imani na moyo mkuu, kizazi hicho cha Waisraeli hakikufika bara la ahadi kamwe. Lakini Yoshua na Kalebu, pamoja na kizazi kipya, waliliingia.

14, 15. (a) Yoshua alipotumia maneno ya Yoshua 1:7, 8, yeye na Waisraeli walijionea nini? (b) Tunajifunza somo jipi linalohusu moyo mkuu kutoka kwa Yoshua na Kalebu?

14 Mungu alimwambia Yoshua: “Uwe hodari [mwenye moyo mkuu, NW] tu na ushujaa mwingi, uangalie kutenda sawasawa na sheria yote aliyokuamuru Musa mtumishi wangu; usiiache, kwenda mkono wa kuume, au wa kushoto, upate kufanikiwa sana kila uendako. Kitabu hiki cha torati kisiondoke kinywani mwako, bali yatafakari maneno yake mchana na usiku, upate kuangalia kutenda sawasawa na maneno yote yaliyoandikwa humo; maana ndipo utakapoifanikisha njia yako, kisha ndipo utakapositawi sana.”—Yoshua 1:7, 8.

15 Yoshua alipotumia maneno hayo, Yeriko na majiji mengine yalishindwa na Waisraeli. Mungu hata alifanya jua lisimame tuli hivi kwamba liliendelea kung’aa mpaka Israeli wakawa wameshinda katika Gibeoni. (Yoshua 10:6-14) Walipotishwa na majeshi ya adui yaliyoungana “kama mchanga ulio ufuoni mwa bahari kwa wingi,” Yoshua alitenda kwa moyo mkuu, na Mungu akafanya Israeli washinde tena. (Yoshua 11:1-9) Ingawa sisi ni wanadamu wasio wakamilifu, kama vile Yoshua na Kalebu, twaweza kumfuata Yehova kikamili, na Mungu aweza kututia nguvu kutembea katika njia zake kwa moyo mkuu.

Moyo Mkuu wa Kumwitibari (Kumtumaini) Mungu

16. Debora, Baraka, na Yaeli walionyesha moyo mkuu katika njia zipi?

16 Kumwitibari Mungu kwa moyo mkuu kunathawabishwa, kama ionyeshwavyo na matukio katika siku ambazo waamuzi walitekeleza hukumu katika Israeli. (Ruthu 1:1) Kwa kielelezo, Mwamuzi Baraka na nabii wa kike Debora walimwitibari Mungu kwa moyo mkuu. Mfalme Mkanaani Yabini alikuwa ameonea Israeli kwa miaka 20 wakati Yehova alipomwamuru Debora amchochee Baraka awakusanye wanaume 10,000 kwenye Mlima Tabori. Mkuu wa jeshi la Yabini, Sisera, alienda kwa kasi hadi mvo wa Kishoni, akiwa na hakika kwamba juu ya ardhi hiyo iliyo sawa wanaume wa Israeli hawangelishinda jeshi lake na magari-farasi yalo ya vita 900 yenye panga za chuma kwenye magurudumu yayo. Waisraeli walipopiga miguu hadi kwenye uwanda wa bonde, Mungu alitenda kwa niaba yao, na furiko la ghafula likageuza uwanja wa pigano kuwa bwawa la tope lililokwamisha magari-farasi ya Sisera. Wanaume wa Baraka walishinda, hivi kwamba “jeshi lote la Sisera likaanguka kwa makali ya upanga.” Sisera alikimbia hadi kwenye hema la Yaeli, lakini alipokuwa akilala usingizi, Yaeli alikuwa na moyo mkuu wa kumuua kwa kupigilia kigingi katika kipaji chake. Hivyo sawasawa na taarifa ya Debora ya kiunabii kwa Baraka, “jambo lenye kutia uzuri” (NW) la ushindi huo lilimwendea mwanamke. Kwa sababu Debora, Baraka, na Yaeli walimwitibari Mungu kwa moyo mkuu, Israeli ‘walistarehe miaka arobaini.’—Waamuzi 4:1-22; 5:31.

17. Ni kielelezo kipi cha kumwitibari Yehova kwa moyo mkuu kilichoandaliwa na Mwamuzi Gideoni?

17 Mwamuzi Gideoni alimwitibari Yehova Mungu kwa moyo mkuu wakati Wamidiani na wengine waliposhambulia Israeli. Ingawa idadi yao ilipitwa na idadi ya wale washambulizi karibu 135,000, wanaume wapiga-vita wa Israeli 32,000 wangaliweza bado kuwa na mbetuko wa kujivunia ushindi wenye kupewa na Mungu. Kwa hiyo, kwa mwelekezo wa Yehova, Gideoni alipunguza majeshi yake kuwa vikundi vitatu vya wanaume 100. (Waamuzi 7:1-7, 16; 8:10) Wale 300 walipoizunguka kambi ya Midiani wakati wa usiku, kila mmoja alikuwa na pembe na mtungi wa maji wenye mwenge ndani yao. Kwa ishara fulani, walipuliza pembe, wakaivunja-vunja mitungi, wakainua mienge yenye kuwaka, na kupaaza sauti: “Upanga wa BWANA [Yehova, NW] na wa Gideoni”! (Waamuzi 7:20) Wamidiani waliotishwa walianza kukimbia wakashindwa. Matukio kama hayo yapaswa kutusadikisha kwamba kumwitibari Mungu kwa moyo mkuu kunathawabishwa leo pia.

Moyo Mkuu wa Kumheshimu Yehova na Kuendeleza Ibada Safi

18. Alipomuua Goliathi, Daudi alifanya nini kwa moyo mkuu?

18 Baadhi ya vielelezi vya Biblia hupa moyo mkuu wa kumheshimu Yehova na kuendeleza ibada safi. Daudi mchanga, aliyeokoa kondoo za baba yake kwa ujasiri, alithibitika kuwa mwenye moyo mkuu mbele ya lile jitu la Kifilisti Goliathi. “Wewe unanijia mimi na upanga, na fumo, na mkuki,” akasema Daudi, “bali mimi ninakujia wewe kwa jina la BWANA [Yehova, NW] wa majeshi, Mungu wa majeshi ya Israeli uliowatukana. Siku hii ya leo BWANA [Yehova, NW] atakutia mkononi mwangu, nami nitakupiga, na kukuondolea kichwa chako, . . . Nao jamii ya watu wote pia wajue ya kwamba BWANA [Yehova, NW] haokoi kwa upanga wala kwa mkuki; maana vita ni vya BWANA [Yehova, NW].” (1 Samweli 17:32-37, 45-47) Kwa msaada wa kimungu, Daudi alimheshimu Yehova kwa moyo mkuu, akamuua Goliathi, na hivyo akawa na daraka muhimu katika kuondoa tisho la Kifilisti kuelekea ibada safi.

19. Sulemani alihitaji moyo mkuu kwa ajili ya mradi upi, na njia aliyofanya hivyo yaweza kutumiwaje katika siku yetu?

19 Wakati Sulemani mwana wa Mfalme Daudi alipokuwa karibu kujenga hekalu la Mungu, baba yake aliyezeeka alimsihi hivi: “Uwe hodari, mwenye moyo mkuu, ukatende hivyo; usiogope wala usifadhaike; kwa kuwa BWANA [Yehova, NW], Mungu, Mungu wangu, yu pamoja nawe; yeye hatakupungukia wala kukuacha, hata itakapomalizika kazi yote ya huo utumishi wa nyumba ya BWANA [Yehova, NW].” (1 Mambo ya Nyakati 28:20) Kwa kuchukua hatua yenye moyo mkuu, Sulemani alimaliza hekalu kwa mafanikio. Programu ya ujenzi ya kitheokrasi inapotokeza ugumu leo, acheni tuyakumbuke maneno ya Daudi: “Uwe hodari, mwenye moyo mkuu, ukatende.” Ni njia nzuri kama nini kumheshimu Yehova na kuendeleza ibada safi!

20. Mfalme Asa alikuwa na moyo mkuu kuhusu nini?

20 Kwa sababu ya tamaa ya Mfalme Asa ya kumheshimu Mungu na kuendeleza ibada safi, yeye aliondolea Yuda sanamu na malaya wa kiume wa hekaluni. Pia alimwondoa nyanya yake mwasi-imani kutoka kwenye cheo chake cha juu akateketeza “sanamu [yake] ya kuchukiza.” (1 Wafalme 15:11-13) Ndiyo, Asa “a[li]tiwa nguvu [alikuwa na moyo mkuu, NW], akayaondolea mbali machukizo yote katika nchi ya Yuda na Benyamini, na katika miji aliyoitwaa milimani mwa Efraimu; akaifanyiza tena madhabahu ya BWANA [Yehova, NW], iliyokuwako mbele ya ukumbi wa BWANA [Yehova, NW].” (2 Mambo ya Nyakati 15:8) Je! wewe pia hukatalia mbali uasi-imani na kuendeleza ibada safi kwa moyo mkuu? Je! unatumia mali zako za kimwili ili kuendeleza masilahi ya Ufalme? Na je! unajaribu kumheshimu Yehova kwa kushiriki kwa kawaida katika kujulisha habari njema ukiwa mmoja wa Mashahidi wake?

21. (a) Masimulizi ya washika uaminifu-maadili wa kabla ya Ukristo yaweza kutusaidiaje? (b) Ni nini kitazungumziwa katika makala ifuatayo?

21 Twashukuru kama nini kwamba Mungu amehifadhi masimulizi ya Kimaandiko kuhusu washika uaminifu-maadili wenye moyo mkuu wa kabla ya Ukristo! Kwa hakika, vielelezo vyao vyema vyaweza kutusaidia tumtolee Yehova utumishi mtakatifu kwa moyo mkuu, hofu ya kimungu, na kicho. (Waebrania 12:28) Lakini Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo pia yana vielelezo vya moyo mkuu wa kimungu kwa matendo. Baadhi ya masimulizi hayo yaweza kutusaidiaje tutembee katika njia za Yehova kwa moyo mkuu?

Ungejibuje?

◻ Moyo mkuu ni nini?

◻ Henoko na Noa walionyeshaje moyo mkuu?

◻ Abrahamu, Sara, na Isaka walitenda kwa moyo mkuu kuhusu mambo gani?

◻ Musa, Yoshua na Kalebu waliweka vielelezo vipi vya moyo mkuu?

◻ Wengine walionyeshaje kwamba walikuwa na moyo mkuu wa kumwitibari Mungu?

[Picha katika ukurasa wa 15]

Gideoni na kikosi chake kidogo walimwitibari Yehova kwa moyo mkuu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki