Hudhuria Mikutano “Zaidi Sana Hivyo”
1 Kukutana pamoja sikuzote kumekuwa muhimu kwa watu wa Yehova. Hekalu na masinagogi yalikuwa mahali pa ibada ya kweli, elimu ya kimungu, na ushirika wenye shangwe kwa Waisraeli. Vivyo hivyo, Wakristo wa mapema hawakuacha kukutana pamoja. Kadiri mikazo na majaribu yaongezekapo katika siku hizi za mwisho zilizo zenye hatari, sisi pia twahitaji kuimarishwa kiroho ambako mikutano yetu ya kutaniko huandaa—nasi twakuhitaji “zaidi sana hivyo.” (Ebr. 10:25) Ona sababu tatu zinazotufanya sisi tuhudhurie mikutano.
2 Kwa Ajili ya Ushirika: Maandiko hutuhimiza ‘tuendelee kufarijiana na kujengana.’ (1 The. 5:11) Ushirika wa kimungu hujaza akili zetu na mawazo yenye kujenga na hutuchochea kufanya kazi nzuri. Lakini tukijitenga, tutaelekea kupokea mawazo ya kipumbavu, ya ubinafsi, au hata ya ukosefu wa adili.—Mit. 18:1.
3 Kwa Ajili ya Mafundisho: Mikutano ya Kikristo huandaa programu yenye kuendelea ya mafundisho ya Biblia yanayokusudiwa kuendeleza hai huko kumpenda Mungu katika mioyo yetu. Inatupatia mwelekezo unaofaa katika kutumia “shauri lote la Mungu.” (Mdo. 20:27) Mikutano hutuzoeza tuwe na ufundi wa stadi za kuhubiri na kufundisha habari njema, ambazo zahitajiwa zaidi sana hivyo sasa ili tuone shangwe nyingi sana ya kupata na kusaidia wale wote watakaokubali kweli ya Biblia.
4 Kwa Ajili ya Ulinzi: Katika ulimwengu huu mwovu, kutaniko ni kimbilio la kiroho la kweli, yaani, mahali salama pa amani na upendo. Tunapohudhuria mikutano ya kutaniko, roho takatifu ya Mungu ina uvutano wenye nguvu kwetu, ikitokeza matunda ya “upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujidhibiti.” (Gal. 5:22, 23) Mikutano hutuimarisha tusimame imara na thabiti katika imani. Hutuandaa tuwe tayari kwa majaribu yaliyoko mbele.
5 Kwa kuhudhuria mikutano kwa ukawaida, twaona kile ambacho mtunga-zaburi alifafanua, kama ilivyorekodiwa kwenye Zaburi 133:1, 3: “Tazama, jinsi ilivyo vema, na kupendeza, ndugu wakae pamoja, kwa umoja.” Mahali popote watu wa Mungu watumikapo na wakutanikapo pamoja leo, “ndiko BWANA alikoamuru baraka, naam, uzima hata milele.”—Italiki ni zetu.