Huduma Yetu—Wonyesho wa Upendo wa Kweli
1 Kupitia huduma yetu twaonyesha utii wetu kwa amri mbili zilizo kubwa kupita zote. (Mt. 22:37-39) Upendo wetu kwa Yehova hutuchochea tuseme kumhusu kwa njia yenye kujenga. Upendo wetu kwa jirani hutusukuma tuwatie moyo kutafuta ujuzi juu ya mapenzi ya Mungu na makusudi yake ili kama sisi, waweze kupata kumpenda Yehova ili wastahili kuipata zawadi ya uhai udumuo milele. Hivyo basi, kupitia huduma yetu twaliheshimu jina la Yehova na kushiriki tumaini la Ufalme lenye thamani pamoja na jirani. Naam, huduma yetu ni wonyesho wa upendo wa kweli kwa Mungu na kwa mwanadamu.
2 Upendo wetu watushurutisha kwenda kusema na watu wa aina zote katika vikao vya aina zote. (1 Kor. 9:21-23) Ili kutoa kielezi: Akiwa ndani ya ndege, mzee Mkristo alikaa kando ya kasisi wa Katoliki ya Roma. Mzee huyo alimfanya kasisi azungumze kwa kumwuliza maswali machache ya busara kisha akaelekeza mazungumzo kwenye Ufalme. Kufikia wakati ambapo kasisi aliondoka ndani ya ndege, alikuwa amepokea vitabu vyetu viwili. Lilikuwa tokeo zuri kama nini la wonyesho wa mzee huyo wa upendo wa kweli kwa jirani yake!
3 Upendo wa Kweli Hutuchochea Kuhubiri: Wale ambao hushiriki katika kazi ya upainia-msaidizi na upainia wa wakati wote hakika wanaonyesha upendo wa kweli kwa Mungu na kwa jirani. Mapainia hudhabihu wakati na nishati zao daima kusaidia wengine kiroho. Ni nini ambacho huwachochea kufanya hivyo? Painia mmoja alisema: “Najua kwamba upendo ni tunda la roho ya Mungu. Kwa hiyo bila huo, singekuwa katika kweli hata kidogo, na zaidi, singefanikiwa kuwa painia. Upendo hunifanya nihangaikie watu, nikitambua mahitaji yao, na kuthamini kwamba watu wanaitikia upendo huo.” Yesu aliwaonyesha watu upendo huo. Wakati mmoja yeye na wanafunzi wake waliochoka walipokuwa wakienda mahali fulani ili ‘kupumzika kidogo,’ umati ulifika mahali hapo mbele yao. Yesu alifanyaje? ‘Akisukumwa na sikitiko kwa ajili yao,’ aliacha mahitaji yake ya kibinafsi ili ‘awafundishe mambo mengi.’—Mr. 6:30-34.
4 Hata watu wakikataa habari njema tunazotoa, twaona shangwe ya ndani, tukijua kwamba tukisukumwa na upendo, tumefanya yote tuliyoweza kuwasaidia wapate wokovu. Wakati sisi sote tutakapohukumiwa na Kristo, tutakuwa na furaha sana kwamba tulionyesha upendo wa kweli kwa ‘kutimiza kikamili huduma yetu.’—2 Tim. 4:5.