“Njia ya Mungu ya Maisha” Mkusanyiko wa Wilaya na wa Kimataifa wa 1998
1 Mithali 10:29 hutukumbusha kwamba “Njia ya BWANA ni kimbilio.” Mkusanyiko wa mwaka huu una kichwa kifaacho kama nini—“Njia ya Mungu ya Maisha”! Kichwa hiki kitasitawishwaje hasa katika programu ya siku tatu? Sisi sote twatazamia kwa hamu nyingi yale ambayo tumetayarishiwa. Na mambo ya maana yatakaziwa.
2 Wamishonari, wafanyakazi wa kimataifa, au wengine wanaotumikia katika migawo ya nchi za kigeni huenda ikawa watahudhuria mkusanyiko wenu. Inatazamiwa kwamba kutakuwako maelfu ya wajumbe kutoka nchi nyingine katika jiji la Nairobi ambamo mkusanyiko wa kimataifa utafanywa. Labda utakutana na baadhi ya wageni hawa. Programu ya mkusanyiko itakazia ripoti za jinsi Yehova anavyobariki kazi katika maeneo mbalimbali.
3 Jitihada ya Kuhudhuria Yastahili: Wengi kati ya ndugu zetu katika Afrika wameona magumu kwa sababu ya vita na msukosuko unaotokea sehemu fulani-fulani katika bara hilo. Wao huona mikusanyiko ya watu wa Yehova kuwa tegemeo lao kuu. Wengine hulazimika kutembea umbali mrefu ili kuhudhuria mkusanyiko, hata hivyo, hawafikirii kukosa hata mmoja. Ndugu mwenye umri wa miaka 73 katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (iliyokuwa Zaire) alitembea kilometa zipatazo 450 kuhudhuria mkusanyiko. Alifika huko siku 16 baada ya kuanza safari yake, miguu yake ikiwa imevimba, lakini mwenye furaha kwa sababu ya kuwa huko. Baada ya mkusanyiko, akiwa na shangwe nyingi zaidi na akiwa ameimarishwa kiroho, alirudi nyumbani kwa miguu. Hiyo imekuwa kawaida yake kwa miaka mingi!
4 Katika Msumbiji mwangalizi wa wilaya na mke wake walipanda mlima na kuvuka eneo kubwa kama jangwa kwa miguu ili kuhudhuria kusanyiko la mzunguko. Walitembea mwendo wa kilometa 90 kwa muda wa saa 45. Wote waliohudhuria walitiwa moyo sana na kielelezo bora cha wenzi hao. Familia nyingi zilizokuwapo zilikuwa zimefanya jitihada hizohizo ili kuhudhuria. Mwangalizi wa wilaya aliripoti kwamba ndugu wengine, kutia ndani mmoja aliyekuwa na umri wa miaka 60, alisafiri kilometa 200 kwa miguu!
5 Je, umefanya mipango hususa ya kuhudhuria mkusanyiko wa mwaka huu? Haielekei kwamba wengi wenu mtalazimika kutembea umbali mrefu, lakini jitihada kadhaa na kujidhabihu kutawalazimu ili nyinyi na familia zenu mwepo. Panga kuhudhuria programu yote nzima kuanzia mwanzo hadi mwisho. Wanafunzi wengi wa Biblia wanafanya maendeleo kuelekea ubatizo. Kuhudhuria kwao mkusanyiko kutawasaidia wafanye uamuzi ufaao. Je, umealika wanafunzi wako wa Biblia na wengine wenye kupendezwa wahudhurie pamoja nawe?
6 Programu ya Siku Tatu: Mwaka huu programu itatolewa kwenye mikusanyiko 16 katika Afrika Mashariki. Kuongezea mkusanyiko wa Kiingereza, mingine itafanywa katika Kiganda, Kinyarwanda, na Kiswahili. Kutakuwa na Lugha ya Ishara ya Kimarekani katika mikusanyiko ifuatayo ya Kiingereza: Nairobi, Mombasa na Kampala. Ndugu zetu viziwi na watu wenye kupendezwa wapasa kuelekezwa kwenye mmoja wa mikusanyiko hii mitatu. Mnara wa Mlinzi, Februari 15, 1998, unaorodhesha tarehe na mahali pa mikusanyiko hiyo. Kufikia sasa umejulishwa mkusanyiko ambao kutaniko lako limegawiwa.
7 Taarifa ya Pekee: Ni jambo la maana hasa kuhudhuria mkusanyiko ambao kutaniko lako limegawiwa. Staha yako ya kibinafsi na ushirikiano kuhusu mipango hii itahakikisha kwamba kila jambo latendeka kwa adabu na mpango.—1 Kor. 14:33, 40.
8 Ijumaa, Jumamosi, na Jumapili asubuhi, programu itaanza saa 3:30. Ijumaa na Jumamosi, programu itamalizika saa 11:00 jioni, na Jumapili, saa 10:00 jioni. Milango itafunguliwa kila siku saa 2:00 asubuhi. Ni wale tu walio na migawo ya kazi watakaoruhusiwa kuingia mapema zaidi ya hapo. Hata hivyo, hakuna atakayeruhusiwa kuhifadhi viti mpaka baada ya saa 2:00 asubuhi.
9 Tunaposafiri kwenda na kutoka mkusanyikoni, twapaswa kutafuta fursa za kutoa ushahidi wa vivi hivi. Wafanyakazi wa vituo vya petroli, makarani wa duka, wafanyakazi wa hoteli, na wahudumu-meza huenda wakapendezwa na ujumbe wa Ufalme. Jitayarishe kwa ajili ya hilo kwa kubeba trakti, magazeti ya karibuni, broshua, au fasihi nyingineyo, ili uweze kutumia kwa faida fursa za kutolea ushahidi watu ambao huenda wasifikiwe na habari njema.—2 Tim. 3:17.
10 “Kazieni Uangalifu Jinsi Msikilizavyo”: Wajumbe wa mkusanyiko watakuwa na hekima wakitii shauri hilo lipatikanalo kwenye Luka 8:18. Wote wanatiwa moyo kubeba Biblia, vilevile kitabu cha nyimbo na kitabu cha kuandikia. Sikiliza kwa makini mambo makuu kutoka katika kila hotuba, na uandike maandishi mafupi. Jiulize mwenyewe jinsi unavyoweza kutumia habari hiyo kibinafsi. Kila usiku wa mkusanyiko, kabla ya kwenda kulala, kwa nini usipitie maandishi yako na uchanganue jinsi unavyoshikamana kwa ukaribu na njia ya Yehova ya maisha.—Mit. 4:10-13.
11 Imeonekana kuwa wakati wa vipindi, wengine huondoka mahali pa wahudhuriaji na kuketi mahali kwingineko, hivyo wakikosa hotuba za programu. Wengine wameonwa wakitembea bila sababu katika njia za kuingilia ilhali walipaswa kuketi pamoja na wahudhuriaji na kusikiliza. Baadhi ya watumishi wa Yehova katika nyakati za zamani walifanya makosa mazito maishani mwao kwa sababu hawakusikiliza kwa makini vikumbusha vya Yehova. Hakika tungependa kuepuka kufanya kosa hilohilo. (2 Fal. 17:13-15) “Mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ametayarisha mafundisho ambayo sisi sote twahitaji. Ni muhimu kwetu “kukazia uangalifu zaidi kuliko ilivyo kawaida mambo yaliyosikiwa nasi” wakati wa kila kipindi cha programu hiyo ya mkusanyiko wa siku tatu. Jambo fulani lenye kutupendeza litakaziwa kila siku, kutia ndani habari itakayoathiri ifaavyo kikweli njia yetu ya maisha wakati ujao. Tukisikiliza kwa makini na kutumia kabisa yale ambayo Yehova huandaa kiroho kwenye habari za mkusanyiko unaokuja, tumaini letu litatiwa nanga imara, ili “tusipate kamwe kupeperushwa mbali” kutoka katika njia ya Mungu ya maisha.—Mt. 24:45; Ebr. 2:1.
12 Mavazi Yanayomheshimu Yehova: Nyakati hizi zilizo ngumu, twahitaji kutoa uangalifu kuliko ilivyo kawaida ili tusishawishiwe na roho ya ulimwengu huu. (1 Kor. 2:12) Mavazi yetu na kujipamba kwetu kwapasa kuwe kwa kiasi na kwapaswa kudhihirisha adhama ya Mungu ambaye twamwabudu. (1 Tim. 2:9, 10) Mavazi yaliyo ghali hayahitajiwi ili kuwa miongoni mwa wale wenye “kuremba fundisho la Mwokozi wetu, Mungu.” (Tito 2:10) Angalia shauri lililo bora kabisa litumikalo na la Kimaandiko kwenye ukurasa wa 17 na 18 wa toleo la Juni 15, 1997 la Mnara wa Mlinzi, fungu la 14-18. Usidharau kamwe ushahidi wenye nguvu tuwezao kutoa kwa kuvalia katika njia impendezayo Yehova.
13 Shahidi mwenye umri wa miaka 16 alisimulia kwamba yeye na ndugu yake walienda kwenye mkahawa jioni moja baada ya vipindi, walitambua kwamba baadhi ya akina ndugu na dada waliokuwa huko walibadili mavazi yao na kuvaa yasiyofaa. Hata hivyo, wasimamizi wengi wa mkahawa huo waliwatendea vizuri kwa kuona Mashahidi waliokuwa wamevalia kinadhifu na ifaavyo na waliovaa beji zao. Hilo lilifungua njia ya kutolea ushahidi baadhi ya wasimamizi hao.
14 Mwenendo Umleteao Yehova Sifa: Twajua kwamba mwenendo wetu wa Kikristo waweza kuathiri jinsi ambavyo wengine huona ibada ya kweli. Kwa hiyo, twataka kujiendesha nyakati zote katika njia ambayo yastahili habari njema na humletea Yehova sifa.—Flp. 1:27.
15 Mwaka jana, mkusanyiko wa wilaya ulifanywa kwa mara ya kwanza kaskazini mwa Angola. Siku ya pili ya mkusanyiko huo, maofisa wawili mapolisi wa mahali hapo walitumwa kuangalia ili kuhakikisha kwamba kulikuwa na utaratibu. Walikaa huko siku yote. Mwishoni mwa siku, walisema vile walivyopendezwa na yale waliyosikia na mwenendo wenye utaratibu ambao waliona. Mmoja wao alisema hivi: “Kwa nini tulitumwa hapa? Twajua kwamba Mashahidi wa Yehova huwa na utaratibu katika vikusanyiko vyao.”
16 Mwanachama wa chama cha kisiasa katika nchi moja ya Kiafrika alikimbilia Ulaya wanachama wenzake walipouawa. Alipata matatizo mengi ya kibinafsi na akavunjika moyo sana. Mwishowe alikubali funzo la Biblia. Alipokuwa akihudhuria mkusanyiko wake wa kwanza wa wilaya, alipendezwa kwamba watu kutoka malezi mbalimbali walikuwa wanakutana pamoja kwa amani na upatano. Alisadikishwa kwamba alikuwa ameipata kweli, na wakati wa mkusanyiko huo aliamua kuvunja mahusiano yake ya kisiasa. Baadaye alibatizwa, na sasa yeye na watoto wake wanamtumikia Yehova.
17 Mwenendo wetu mwaka huu kwenye mikusanyiko utaathirije wale watakaohudhuria kwa mara ya kwanza? Je, wataona roho ya ushirikiano ikiwa dhahiri tunapofanya kazi pamoja tukiwa wajitoleaji? Je, watapendezwa na usafi wa mazingira yetu na kwa kuona kwamba kabla ya kuondoka mkusanyikoni, sisi na watoto wetu twaokota takataka ambazo huenda zikawa zimerundamana karibu na viti vyetu? Je, wataona mwenendo wetu mwema tunaposafiri kwenda na kutoka mahali petu pa kulala na mkusanyikoni? Je, wataona kwamba wazazi wanasimamia watoto wao kwa uangalifu nyakati zote? Na tuhakikishe kwamba tutakuwa wonyesho mzuri iwezekanavyo kwa wote watuangaliao.
18 Kulipia Gharama za Mkusanyiko: Tikiti ya kuingia ili kupata kiti mahali pa michezo au tamasha nyingineyo katika stediamu au jumba la mkusanyiko yaweza kuwa ghali katika ulimwengu wa leo. Hiyo ni kwa sababu ya gharama za juu za kulipia gharama za ukodishaji katika miji mikuu. Kwenye mikusanyiko sikuzote Sosaiti imekuwa ikisema, “kiingilio ni bure, hakuna sadaka.” Basi, je, gharama za kukodisha na gharama nyingine za mkusanyiko zitalipiwaje? Kwa michango ya ukarimu ya wahudhuriaji. Tuna uhakika kwamba mtaonyesha roho ya ukarimu kama ile iliyoonyeshwa na watumishi wa Mungu zamani kwa kumwiga Yehova Mungu na Yesu Kristo. (2 Kor. 8:7) Uangalifu mkubwa unafanywa ili kuhakikisha kwamba michango yote inalindwa, inarekodiwa, na kutumiwa kwa kusudi inayolipasa. Michango yoyote ya kutolewa kwa hundi yapasa kulipwa kwa “I.B.S.A,” au jina la shirika katika Tanzania na Rwanda.
19 Viti: Mielekezo ambayo imetolewa kwa miaka kadhaa itaendelea kutumika, yaani, VITI VYAWEZA KUHIFADHIWA TU KWA AJILI YA WASHIRIKI WA KARIBU WA FAMILIA YAKO NA WOWOTE AMBAO HUENDA WAKAWA WANASAFIRI PAMOJA NAWE. Imekuwa vizuri kuona maendeleo kuhusu jambo hili, na hili limeongeza hali ya upendo ambayo imeonyeshwa mikusanyikoni. Mahali pengi pa mikusanyiko, viti vingine vyapatikana kwa urahisi zaidi kuliko vingine. Tafadhali onyesha ufikirio, na uachie wale ambao hali zao zataka viti vifaavyo zaidi. Kumbuka kwamba ‘upendo hautafuti masilahi yake wenyewe.’—1 Kor. 13:4, 5; Flp. 2:4.
20 Wenye Matatizo ya Kusikia: Wale wenye matatizo ya kusikia huenda wakahitaji kuketi mahali ambapo watanufaika na programu. Ikiwa wewe una tatizo la kusikia, waweza kuomba msaada kutoka kwa wakaribishaji kuhusu mahali pa kukaa.
21 Kamera, Vidiokamera, na Virekodio vya Kaseti: Kamera na vifaa vya kurekodia vyaruhusiwa kutumiwa mikusanyikoni. Hata hivyo, jinsi unavyovitumia haipaswi kuwakengeusha fikira wengine. Kutembea-tembea kupiga picha kutasumbua wengine wanaojaribu kuikazia fikira programu. Vifaa vya aina yoyote vya kurekodia havipaswi kuunganishwa kwenye mifumo ya umeme au sauti, wala vifaa hivi havipaswi kufunga vijia vya kupitia, au kuzuia wengine kuona.
22 Msaada wa Kwanza: Idara ya Msaada wa Kwanza ni ya dharura tu. Tafadhali beba aspirini, visaidizi vya umeng’enyaji, bendeji, pini, na vifaa vifananavyo na hivyo, kwa kuwa vitu hivyo havitagawanywa kusanyikoni. Wowote wawezao kupatwa na ugonjwa wa ghafula (kama kifafa), ugonjwa wa kisukari, matatizo ya moyo, na kadhalika, wapaswa kubeba dawa zao wanazohitaji. Wanapaswa kuwa na mshiriki wa familia au wa kutaniko anayeelewa hali yao na anayeweza kushughulikia dharura, itokeapo. Matatizo yametokea kwenye mikusanyiko wakati watu walio na matatizo ya kudumu ya afya walipoachwa peke yao, wakawa wagonjwa. Ikiwa kuna wale wenye mahitaji ya pekee ya afya ambao hawana washiriki wa familia wanaoweza kuwasaidia, wazee watahitaji kujulishwa kuhusu hali hiyo na wapaswa kufanya mipango ya lazima ili kusaidia. Haiwezekani kuandaa vyumba vya pekee mkusanyikoni vya kutunza wale walio na ugonjwa unaosababishwa na mazingira au mizio.
23 Chakula Mkusanyikoni: Kila mtu anayehudhuria apaswa kuleta chakula chake mwenyewe badala ya kuondoka mahali pa mkusanyiko wakati wa pumziko fupi la mchana kununua chakula nje. Chakula chepesi chenye kujenga na kilicho rahisi kubeba yaelekea kitatosha. Nyongeza ya Huduma ya Ufalme Yetu ya Oktoba 1995, fungu la 24, hutupatia wazo la vitu vya kubeba. Vyombo vya gilasi na vinywaji vyenye alkoholi havipaswi kuletwa mahali pa mkusanyiko. Vyombo vya kuwekea chakula vyapasa kuwa vyenye udogo wa kutosha kuwekwa chini ya kiti chako. Wengine kati ya wasikilizaji wameonwa wakila na kunywa wakati wa programu. Hilo laonyesha ukosefu wa staha kwa pindi hiyo.
24 Twafurahi kama nini kwamba “Njia ya Mungu ya Maisha” Mkusanyiko wa 1998 utaanza hivi punde! Je, umekamilisha mipango yako ya kuhudhuria? Na uwe na safari njema na urudi nyumbani ukiwa umeburudishwa, ukiazimia kuendelea mbele katika utumishi wenye thamani wa Yehova na kuendelea kufuatia njia ya Mungu ya maisha ili upate baraka za milele.
[Sanduku katika ukurasa wa 6]
Vikumbusha vya Mkusanyiko
▪ Ubatizo: Wataka kubatizwa wapaswa kuwa vitini mwao mahali palipoteuliwa kabla ya programu kuanza Jumamosi asubuhi. Kila mtu anayepanga kubatizwa apaswa kuleta vazi lake la kuogelea la kiasi au nguo nyingineyo ifaayo na taulo. Wakati uliopita baadhi ya watu wamevaa vazi ambalo halikufaa na hilo lilikengeusha fikira kwa pindi hiyo. Ni muhimu kuangalia mapema kama nguo ambazo mtu anapanga kuvaa zitabaki zikiwa zenye kiasi hata zikilowa maji. Wazee wanaopitia maswali ya wataka kubatizwa yaliyo katika kitabu Huduma Yetu wapaswa kuhakikisha kwamba kila mtu anaelewa mambo haya. Ubatizo ukiwa ishara ya wakfu wa mtu ni jambo la kindani na la kibinafsi kati yake na Yehova. Hivyo, haifai wataka kubatizwa kukumbatiana au kushikana mikono wanapobatizwa.
▪ Kadi za Beji: Tafadhali vaa kadi ya beji ya 1998 nyakati zote unapokuwa katika jiji la mkusanyiko na unaposafiri kwenda au kutoka huko. Mara nyingi hilo hutokeza fursa kwetu kutoa ushahidi mzuri. Kadi na vifuko vya beji vyapasa kununuliwa kupitia kutaniko lako, kwa kuwa havitapatikana mkusanyikoni. Usingoje hadi siku chache kabla ya mkusanyiko ili kuomba kadi kwa ajili yako na familia yako. Kumbuka kubeba kadi yako ya wakati uliopo ya Mwelekezo wa Mapema Kuhusu Tiba/Ondoleo la Hatia.
▪ Mahali pa Kulala: Wale wanaohitaji mahali pa kulala katika madarasa au vyumba vya shule katika majengo mengine ambamo hakuna vitanda wala matandiko yawapasa wakumbuke kuleta matandiko yao wenyewe. Mahali pengine, usiku waweza kuwa wenye baridi sana. Katika maeneo mengine, akina ndugu wameliona likiwa jambo lenye hekima kuwa na aina fulani ya kujilinda na mbu. Tafadhali iweni waangalifu mnapokunywa maji na hasa mwangalie watoto wanywe maji safi. Waandishi wa makutaniko wapaswa kuhakikisha kwamba fomu za Ombi la Mahali pa Kulala kwa Wenye Mahitaji ya Pekee zatumwa bila kukawia kwenye anwani ifaayo ya mkusanyiko. Ikiwa lazima upangue mahali pa kulala palipopangwa kupitia mpango wa mahitaji ya pekee, wapaswa kujulisha mwenye nyumba au hoteli mara moja na Idara ya Mahali pa Kulala ili chumba kipewe mtu mwingine.
▪ Nyimbo: Nyimbo zifuatazo zimeteuliwa kwa ajili ya programu ya mwaka huu: 10, 15, 42, 43, 79, 85, 89, 91, 105, 151, 155, 164, 174, 177, 191, 202, 211 na 220. Watu mmoja-mmoja na vikundi vya familia huenda wakataka kupanga vipindi vya mazoezi ili waweze kushiriki kikamili katika kuimba nyimbo zote wakati wa programu ya mkusanyiko.
▪ Viti vya Kutembezea Watoto: Katika sehemu zilizo nyingi, viti vya kutembezea watoto haviwezi kutumiwa mahali penye kusanyiko la watu wote. Kanuni za moto hukataza viwe kwenye makorido na vijia kati ya safu za viti. Kwa kuwa umati wa watu waweza kusababisha hali zenye kusongamana, viti vya kutembezea watoto vyaweza kusababisha hatari, kwa mtoto na yeyote awezaye kujikwaa navyo. Kwa hiyo tafadhali usilete viti vya kutembezea watoto mkusanyikoni. Viti vyenye usalama vya mtoto vilivyowekwa kwa ukaribu sana na viti vya wazazi vyaruhusiwa. Tafadhali usilete viti vya bafta. Matumizi yake hayaruhusiwi kwenye majengo makubwa ya umma. Ushirikiano wako ni wa muhimu na wathaminiwa.
▪ Utumishi wa Kujitolea: Je, waweza kutenga kando wakati kwenye mkusanyiko ili usaidie katika mojawapo ya idara? Kutumikia ndugu zetu, japo kwa saa chache tu, kutasaidia sana nako huleta uradhi mwingi sana wa kibinafsi. Ikiwa waweza kusaidia, tafadhali ripoti kwenye Idara ya Utumishi wa Kujitolea kwenye mkusanyiko. Watoto walio chini ya umri wa miaka 16 wanaweza kutoa usaidizi mzuri kwa kufanya kazi chini ya mwelekezo wa mzazi au mtu mzima mwingine mwenye daraka.
▪ Ukaribishaji-Wageni: Tutazamiapo kukaribisha wajumbe wengi kutoka ng’ambo kwenye mkusanyiko wetu wa kimataifa, twataka kukumbuka kwamba ni daraka letu kuwakaribisha wageni wetu kwa uchangamfu, na kwa upendo wa Kikristo. Hilo lamaanisha kwamba tuna daraka la kuwakirimu na kuwapa vitu wageni wetu badala ya kuwatazamia watupatie sisi. (Mdo. 20:35) Zaidi ya yote, kumbukeni kwamba twahudhuria mkusanyiko tujengwe kiroho wala si kuomba-omba au kutazamia kupokea vitu vya kimwili kutoka kwa wageni wetu au mtu mwingine yeyote.
▪ Maneno ya Tahadhari: Hakikisha gari lako limefungwa nyakati zote, na usiache kitu chochote kinachoonekana kamwe ili kushawishi mtu alivunje. Wezi na wezi wa mifukoni hukazia uangalifu vikusanyiko vikubwa. Si jambo la hekima kuacha vitu vyenye thamani kwenye kiti chako. Huwezi kuwa na uhakika kwamba kila mtu karibu nawe ni Mkristo. Kwa nini utoe kishawishi chochote? Ripoti zimepokewa za watu kutoka nje kujaribu kushawishi watoto. ANGALIA WATOTO WAKO NYAKATI ZOTE.
Uangalifu wapaswa kudhihirishwa ili kuepuka kujaza kupita kiasi magari yaliyokodiwa na kutaniko kwa ajili ya safari ya mkusanyiko. Ni afadhali kutumia fedha za ziada kwa gharama za usafiri kuliko kuvunja sheria za Kaisari au vibaya hata zaidi kuweka akina ndugu katika hatari za aksidenti na uwezekano wa kupoteza uhai kwa sababu ya kujaza gari kupita kiasi au kumtia moyo dereva aendeshe kwa kasi zaidi ili mfike mnakoenda mapema. (Rom. 13:1-7; Kum. 21:1-9) Akina ndugu wenye daraka wanaosafiri kwenye magari hayo wanapaswa kuhisi huru kutoa shauri lenye upendo kuhusiana na jambo hili ikihitajika.
Huduma za televisheni na vidio katika hoteli nyingi huonyesha programu zisizofaa. Usiruhusu watoto watazame televisheni bila usimamizi chumbani.
Tafadhali usipigie simu au kuandikia usimamizi kwa ukumbi wa mkusanyiko. Ikiwa habari haipatikani kutoka kwa wazee, waweza kuandika ukitumia anwani ya mkusanyiko hususa, kama ipatikanavyo nyuma ya fomu ya Ombi la Mahali pa Kulala kwa Wenye Mahitaji ya Pekee.