Mikusanyiko ya Wilaya ya 1999 ya “Neno la Mungu la Kiunabii”
1 Waisraeli walipokuwa karibu kuingia Bara Lililoahidiwa, Musa aliwasihi wathamini maagizo ya Mungu. Aliwaambia: “Si jambo lisilofaa kwenu; maana, ni maisha yenu.” (Kum. 32:45-47) Je, hatumshukuru Yehova kwamba maisha yetu yana thamani sana kwake hivi kwamba yeye huendelea kutuongoza kupitia Neno lake lenye thamani sana? Kwa hiyo, twatazamia kwa hamu Mkusanyiko wa Wilaya wa siku tatu wa “Neno la Mungu la Kiunabii” na yale ambayo Yehova ametuwekea akibani.
2 Mwaka huu, mikusanyiko ya wilaya inapangwa sehemu zifaazo 22 kotekote Afrika Mashariki. Mbali na Kiingereza na Kiswahili, programu ya mkusanyiko itafasiliwa katika Lugha ya Ishara ya Marekani na kufanywa katika Kifaransa, Kinyarwanda, Kirundi, na Kiganda.
3 Labda tayari umefanya mipango ya kuhudhuria kila siku ya mkusanyiko kwa sababu waamini kwamba Yehova anakutazamia uhudhurie. Uwe na uhakika kwamba anaona jitihada za mtu mmoja-mmoja na kujidhabihu ambako watumishi wake wanafanya ili kuhudhuria, naye hukumbuka watu hao kwa uthamini. (Ebr. 6:10) Kwa kuhudhuria kila siku ya mkusanyiko kuanzia wimbo wa kufungua hadi sala ya kumalizia, twamwonyesha Yehova kwamba twathamini maneno yake kwetu. (Kum. 4:10) Pia twaonyesha uthamini kwa kazi ngumu ya ndugu zetu wengi wanaohusika katika kutayarisha mkusanyiko.
4 Kupangia maelfu ya watu wa Mungu wakusanyike kila mwaka katika sehemu za mkusanyiko huhitaji upangaji wa mapema na mpango mzuri. Kujua kwamba tumefanyiwa mipango ya mkusanyiko kwa upendo kwapaswa kutuchochea kushirikiana, ili “mambo yote yatukie kwa adabu na kwa mpango.” (1 Kor. 14:40) Habari na vikumbusha vifuatavyo vimetolewa ili uweze kufika kwenye mkusanyiko ukiwa umejitayarisha kikamili kufurahia chakula cha kiroho na ushirika wa Kikristo.
Kabla ya Mkusanyiko
5 Je, wale unaojifunza nao Biblia na watu wengine wenye kupendezwa wanahitaji msaada katika kufanya mipango ya kibinafsi ya kuhudhuria mkusanyiko? Yale wanayoona na kusikia huko huenda yakawachochea wawe waabudu wa Yehova. (1 Kor. 14:25) Wazee wapaswa kujua yeyote anayehitaji msaada wa mahali pa kulala na usafiri, hasa washiriki wa kutaniko walio wazee-wazee, na kuwasaidia kwa upendo waone mahitaji yao yanatimizwa.—Gal. 6:10.
6 Je, mipango yako ya mahali pa kulala imekamilika? Kama wakaa hotelini, je, umethibitisha kwamba utapata chumba na umepeleka amana hotelini? Fomu zozote za Ombi la Mahali pa Kulala kwa Wenye Mahitaji ya Pekee zilizokubaliwa na Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko zapasa kupelekwa kwenye anwani ifaayo ya mkusanyiko na mwandishi wa kutaniko. Ikiwa umegawiwa mahali pa kulala chini ya mpango wa mahitaji ya pekee na wataka kuupangua, tafadhali julisha Idara ya Mahali pa Kulala ya kwenu bila kukawia ili watu wengine wagawiwe mahali hapo pa kulala.
7 Ikiwa wahitaji habari kuhusu mkusanyiko, unaweza kujulisha ofisi. Tafadhali usipigie simu au kuandikia wasimamizi wa majengo ya mkusanyiko.
8 Kwa kuwa Idara ya Huduma ya Kwanza kwenye mkusanyiko imewekwa kushughulikia hali za dharura pekee, twapendekeza kwamba ulete kwenye mkusanyiko asprini zako mwenyewe, bendeji, vifaa vya kuvutia dawa, visaidizi vya umeng’enyaji, na vifaa kama hivyo ukiona kwamba huenda vikahitajiwa. Ikiwa wewe au mpendwa wako ana tatizo kubwa, kama vile tatizo la moyo, ugonjwa wa kisukari, au hatari ya kifafa, tafadhali beba dawa zinazohitajika mkusanyikoni ili utunze mahitaji hayo kama vile ungefanya ukiwa nyumbani au likizoni. Lingekuwa jambo la hekima mshiriki wa familia au rafiki wa karibu anayeelewa hali hiyo aandamane na mtu huyo kila mara, kwa kuwa ndiye atakayeweza kumpa msaada unaohitajiwa.
9 Bila shaka fursa za kutoa ushahidi wa vivi hivi zitatokea unaposafiri kwenda na kutoka mkusanyikoni. Je, utajitayarisha kushiriki kweli na wengine? Sisi sote, kutia ndani watoto, twaweza kuwapa trakti wafanyakazi wa kituo cha petroli, wafanyakazi wa basi, na wengine unaokutana nao katika safari zako. Kutakuwa na fursa za kutoa magazeti, broshua, au fasihi nyinginezo kwa watu wenye kupendezwa. Jitayarishe kutoa ushahidi wa vivi hivi kwa watu ambao huenda wakakosekana tunapotumia njia zile nyingine za kawaida za kuhubiri.
Wakati wa Mkusanyiko
10 Milango itafunguliwa saa 2:00 asubuhi kila siku mkusanyikoni. Unaweza kuhifadhi viti kwa wale tu ambao ni wa familia yako ya karibu au walio katika kikundi chako cha gari. Mahali pa kuketi panapofaa patahifadhiwa ndugu na dada wazee-wazee, na mahali pa wasiojiweza patatengwa kwa wale wanaohitaji viti vya magurudumu. Haiwezekani kutenga vyumba vya pekee kwa wale wenye magonjwa yanayosababishwa na mazingira au mizio, mkusanyikoni. Kila siku unapoondoka mahali pako pa kuketi, tafadhali angalia uhakikishe kwamba una vitu vyako vyote.
11 Ili tuweze kukusanyika katika mikusanyiko yetu ya wilaya kwa idadi kubwa zaidi, twahitajiwa kutii amri za kwetu, sheria za moto, na mambo mengine ya usalama. Tafadhali tii maagizo ya kutopikia mahali pa kulala au sehemu nyinginezo ambazo hazijaidhinishwa.
12 Je, utabatizwa kwenye mkusanyiko wa wilaya? Katika kipindi cha Jumamosi asubuhi, sehemu yenye viti itahifadhiwa kwa wataka-kubatizwa, na wakaribishaji watakuongoza kwenye sehemu hiyo. Ikiwezekana, tafadhali keti hapo kabla ya kipindi kuanza. Lete Biblia yako, kitabu cha wimbo, taulo, na nguo ya kuogelea ya kiasi. Kaptura, tishati zilizo na maandishi, na mavazi kama hayo hayafai kwa pindi hiyo yenye adhama. Wazee wanaopitia maswali katika kitabu Huduma Yetu pamoja na wataka-kubatizwa wapaswa kuhakikisha kwamba kila mmoja anaelewa mambo hayo. Kwa kuwa ubatizo ni ishara ya kibinafsi ya kujiweka wakfu kwa Yehova Mungu, haingefaa wataka-kubatizwa kushikana mikono wanapobatizwa.
13 Unaweza kutumia kamera, vidiokamera, na virekodio vya kaseti kwenye mkusanyiko. Hata hivyo, mahali vinapowekwa au kutumiwa hapapaswi kufunga njia, kuzuia watu wengine kuona, au kukengeusha fikira kutoka kwa programu. Havipaswi kuunganishwa kwenye mifumo ya umeme au sauti.
14 Kwa wale walio na tatizo la kusikia, mipango itafanywa ili waketi mahali ambapo wanaweza kunufaika na programu. Tafadhali omba msaada kutoka kwa wakaribishaji kuhusu mipango hii.
15 Kadiri simu za mkononi na pagers ziongezekavyo, tafadhali mwe waangalifu kwamba vifaa hivi havivurugi kusikiliza kwenu programu wala wale wanaoketi karibu nanyi wanaokaza fikira kwenye programu. Vifaa hivi havipasi kuruhusiwa kulia kwa sauti unapokuwa umeketi miongoni mwa wasikilizaji. Ukilazimika kutumia simu za mkononi programu inapoendelea, tafadhali fanya hivyo nje ya jengo la mkusanyiko.
16 Kuhusu mafaa ya wakati na usahili, Sosaiti imetuomba tulete vyakula vyetu wenyewe mkusanyikoni kila siku. Ndugu wengi wamefuata mwelekezo huu, na wameona kwamba baada ya kipindi cha asubuhi kwisha, wanaweza kuketi na familia zao na kula chakula walicholeta siku hiyo. Wengi wamesema kwamba fursa ya kupumzika wakati wa mchana na kutumia wakati wa ziada na ndugu na dada zao imekuwa yenye kufurahisha. Ili jambo hilo liwezekane, vyakula na vinywaji vyapasa kununuliwa mapema kabla ya wakati na kuvipakia katika vyombo vidogo au vyombo vya kufanya vinywaji viwe baridi vinavyoweza kutoshea chini ya kiti. Twaomba wahudhuriaji wote wafuate maagizo hayo. Hivi majuzi, wasimamizi wa jengo na wauza-chakula katika majengo ambayo mikusanyiko yetu inafanyiwa, wameona akina ndugu wakiondoka mahali pa mkusanyiko ili kununua chakula kutoka kwa wauza-chakula wa barabarani na kwenye maduka yanayotayarisha chakula cha haraka karibu na hapo. Baadhi ya wauza-chakula kwenye majengo ya mkusanyiko yanayotumiwa sasa wanadai waruhusiwe kufungua vibanda vyao vya chakula na kuuzia wajumbe wanaohudhuria mikusanyiko yetu. Jambo hilo likiruhusiwa, walimwengu wengi watachangamana nasi mchana kutwa. Pia, msongamano na foleni ndefu katika vibanda vilivyokubaliwa utarudi, ukivuruga hali yenye kustarehesha ya mikusanyiko yetu. Kwa hiyo, twamwomba kila mtu ajitahidi kubeba chakula na vinywaji vyake mwenyewe kila siku mkusanyikoni. Watu wenye kupendezwa wanaoandamana nawe mkusanyikoni wanapaswa pia kubeba chakula chao wenyewe. Vyombo vya gilasi na vileo haviruhusiwi mkusanyikoni.
17 Je, unaweza kujitolea kusaidia kusafisha jengo hilo baada ya vipindi vya kila siku? Au je, unaweza kufanya kazi katika mojawapo ya idara za mkusanyiko? Ikiwa unaweza kusaidia, tafadhali ripoti kwenye Idara ya Utumishi wa Kujitolea kwenye mkusanyiko. Watoto walio chini ya umri wa miaka 16 wanaweza kutoa usaidizi mzuri kwa kufanya kazi chini ya mwelekezo wa mzazi au mtu mzima mwingine. Bila shaka, kila mtu anaweza kusaidia kusafisha jengo kwa kuhakikisha kwamba takataka zozote zinaokotwa na kutupwa ifaavyo.
18 Tumepokea miongozo mizuri kuhusu mavazi na mapambo mazuri kwenye mikusanyiko yetu. Kwa kielelezo: Tuna mwelekezo wa habari hii kwenye nyongeza za Huduma ya Ufalme Yetu, tuna vielezi na picha katika fasihi zetu, na la maana zaidi ya yote, tuna yale ambayo Yehova husema katika Biblia. (Rom. 12:2; 1 Tim. 2:9, 10) Watu wanatujua na wanajua sababu iliyotufanya tukusanyike katika jiji lao. Hivyo basi, mavazi na mapambo yetu hutoa ushahidi mkubwa sana. Watu wa Yehova walio wengi huweka kielelezo chema katika upande huu. Ingawa hivyo, mara kwa mara, twaona roho ya ulimwengu ikionyeshwa katika mavazi na mapambo ya watu fulani wanaohudhuria mikusanyiko yetu. Mavazi yenye kufunua mwili ya aina yoyote ile hupinga dai la mtu huyo la kuwa mtu wa kiroho. Mapambo ya kiasi, safi, na yaliyo nadhifu ndiyo yenye kuvutia zaidi. Kwa hiyo, vichwa vya familia vyapaswa kuangalia kile ambacho washiriki wa familia yao wanapanga kuvaa. Hilo lahusika pia tunapokuwa mbali na mkusanyiko. Kuvaa beji zetu kabla na baada ya vipindi vya siku hututambulisha zaidi kuwa watu wa Yehova walio safi.—Linganisha Marko 8:38.
19 Mfalme Solomoni mwenye hekima alipuliziwa kuona kwamba “ujinga umefungwa ndani ya moyo wa mtoto” na “mwana aliyeachiliwa humwaibisha mamaye.” (Mit. 22:15; 29:15) Twawapongeza nyinyi wazazi kwa njia mnayoendelea kusimamia watoto wenu. Tunapendezwa kuona vijana wetu walio wengi wakikaza fikira ili kunufaika na programu ya mkusanyiko. Tumesikia maelezo mazuri kuhusu watoto wetu kutoka kwa wajumbe wa kigeni ambao wamehudhuria mikusanyiko yetu.
20 Kwa sababu sisi hualika watu wote kwenye mikusanyiko yetu, ni jambo la hekima kuwa waangalifu kuhusu watoto na mali zetu. Watoto wetu ni zawadi yenye thamani kutoka kwa Yehova. Lakini twajua kwamba ulimwengu hudhihirisha asili ya Shetani ya utekaji. Kwa sababu hiyo, tafadhali sikuzote jua mahali waliko watoto wako. Pia wapaswa kubeba kamera, vibeti, na vitu vingine vyenye thamani nyakati zote na usiviache kitini pako. Hakikisha kwamba gari lako limefungwa, na uweke mali ya kibinafsi kwenye buti au uichukue. Kufanya hivyo hupunguza kumshawishi mtu kuvunja gari lako.
21 Vikumbusha vya Mkusanyiko:
▪ Kadi za Beji: Tafadhali vaa kadi ya beji ya 1999 nyakati zote unapokuwa katika jiji la mkusanyiko na unaposafiri kwenda au kutoka huko. Mara nyingi hilo hutokeza fursa kwetu kutoa ushahidi mzuri. Kadi na vifuko vya beji vyapasa kununuliwa kupitia kutaniko lako, kwa kuwa havitapatikana mkusanyikoni. Usingoje hadi siku chache kabla ya mkusanyiko ili kuomba kadi kwa ajili yako na familia yako. Kumbuka kubeba kadi yako ya karibuni ya Mwelekezo wa Mapema Kuhusu Tiba/Ondoleo la Hatia.
▪ Mahali pa Kulala: Wale wanaohitaji mahali pa kulala katika madarasa au kwenye mabweni ya shule au katika majengo mengine ambamo hakuna vitanda wala matandiko yawapasa wakumbuke kuleta matandiko yao wenyewe. Mahali pengine, kwaweza kuwa na baridi sana usiku. Katika maeneo mengine, akina ndugu wameliona likiwa jambo lenye hekima kuwa na aina fulani ya kujilinda na mbu. Tafadhali iweni waangalifu mnapokunywa maji na hasa mwangalie watoto wanywe maji safi. Waandishi wa makutaniko wapaswa kuhakikisha kwamba fomu za Ombi la Mahali pa Kulala kwa Wenye Mahitaji ya Pekee zapelekwa bila kukawia kwenye anwani ifaayo ya mkusanyiko. Ikiwa lazima upangue mahali pa kulala palipopangwa kupitia mpango wa mahitaji ya pekee, wapaswa kujulisha mwenye nyumba au hoteli mara moja na Idara ya Mahali pa Kulala ili chumba hicho kipewe mtu mwingine.
▪ Nyimbo: Nyimbo zifuatazo zimeteuliwa kwa ajili ya programu ya mwaka huu: 3, 13, 15, 19, 53, 59, 72, 91, 111, 113, 129, 155, 174, 177, 180, 181, 187 na 191. Watu mmoja-mmoja na vikundi vya familia huenda wakataka kupanga vipindi vya mazoezi ili waweze kushiriki kikamili katika kuimba nyimbo zote wakati wa programu ya mkusanyiko.
▪ Uangalifu wapasa kudhihirishwa ili kuepuka kujaza kupita kiasi magari yaliyokodiwa na kutaniko kwa ajili ya safari ya mkusanyiko. Ni afadhali kutumia fedha za ziada kwa gharama za usafiri kuliko kuvunja sheria za Kaisari, au vibaya hata zaidi kuweka akina ndugu katika hatari za aksidenti na uwezekano wa kupoteza uhai kwa sababu ya kujaza gari kupita kiasi au kumtia moyo dereva aendeshe kwa kasi zaidi ili mfike mnakoenda mapema. (Rom. 13:1-7; Kum. 21:1-9) Akina ndugu wenye jukumu wanaosafiri kwenye magari hayo wanapaswa kuhisi huru kutoa shauri lenye upendo kuhusiana na jambo hili ikihitajika.
22 Inatia moyo kuona ndugu na dada wakiandika wakati wa vipindi vya mkusanyiko. Maandishi mafupi yatakusaidia ukaze fikira na kukumbuka mambo makuu. Kupitia maandishi yako na familia yako au rafiki zako hukufanya utafakari mambo makuu ya mkusanyiko ili usiyasahau.
23 Watu wa Yehova wamekuwa wakarimu sikuzote katika kutoa mchango kwa masilahi ya kitheokrasi. (Kut. 36:5-7; 2 Nya. 31:10; Rom. 15:26, 27) Michango yenu ya hiari kuelekea kazi ya ulimwenguni pote hutumiwa kulipia gharama zinazohusiana na kukodisha majengo makubwa ambamo mikusanyiko inafanywa. Michango yako ikitolewa kupitia cheki, tafadhali ilipe kwa “I.B.S.A.” au kwa jina la shirika la kwenu. Ikiwa huna hakika, waweza kuuliza wasimamizi kuhusu jina linalotumika kwenu.
24 Kama ilivyorekodiwa kwenye Amosi 3:7, Yehova alisema “hatafanya neno lo lote, bila kuwafunulia watumishi wake manabii siri yake.” Akiwa “Mfunuaji wa siri,” Yehova amefanya mamia ya unabii urekodiwe ambao umetimia kwa usahihi na kikamili. (Dan. 2:28, 47) Ahadi tukufu zitatimizwa. Mikusanyiko ya Wilaya ya 1999 ya “Neno la Mungu la Kiunabii” itaimarisha imani yako katika ahadi za Mungu. Sikiliza kwa makini neno analokuambia Yehova. Tumia utakayoona na kusikia—katika huduma, katika kutaniko, na katika maisha yako ya kibinafsi. Twaomba baraka tele za Yehova kwa mipango yako yote ya kuhudhuria kila siku, karamu hii nono ya kiroho!
[Blabu katika ukurasa wa 3]
Panga uhudhurie siku yote Ijumaa, Jumamosi, na Jumapili!