Sisi Sote Twahitajiwa ili Kutimiza Kazi
1 Kila mwanafunzi wa Yesu Kristo apaswa kuelewa kwamba jitihada zake za kuunga mkono na kushiriki katika kazi ya kuhubiri Ufalme ni za maana. Yesu alitambua kwamba wanafunzi wake wangetokeza matunda ya Ufalme katika viwango mbalimbali. (Mt. 13:23) Ijapokuwa kiwango kikubwa cha utendaji wa kuhubiri chafanywa na mapainia wengi wenye bidii, wote ambao wanaendelea kwa bidii kumtukuza Mungu kwa kuzaa matunda mengi iwezekanavyo wanapongezwa.—Yn. 15:8.
2 Jitihada za Pamoja Hutimiza Mengi: Yesu alitabiri kwamba jitihada zenye kuongezeka za wanafunzi wake wote zingetokeza kazi kubwa kuliko zake. (Yn. 14:12) Iwe hali zetu za kibinafsi zazuia yale tuwezayo kufanya au kuturuhusu kutoa wakati mwingi katika kuhubiri Ufalme, sisi sote twahitajiwa ili kutimiza kazi. Ni kama tu vile Paulo alivyosema: “Mwili wote, kwa kuunganishwa pamoja kwa upatano na kufanywa ushirikiane kupitia kila kiungo ambacho hupa kile kihitajiwacho, kulingana na utendaji wa kila kiungo kimoja-kimoja katika kipimo kipasacho, hutokeza ukuzi wa mwili.”—Efe. 4:16.
3 Huenda wengine wakahisi kwamba hawachangii mengi. Hata hivyo, machoni pa Yehova jambo la maana ni kwamba utumishi wetu uwe wa nafsi yote. Kila kitu tumfanyiacho ni chenye thamani na chathaminiwa.—Linganisha Luka 21:1-4.
4 Endelea Kutegemeza Kazi: Sisi sote tuna pendeleo la kuchangia kimwili kazi ya ulimwenguni pote. Pia wengine wanaweza kusaidia na kazi ya kimwili inayohusika katika kutegemeza kazi ya Ufalme. Kila mmoja anaweza kujitahidi kutoa maelezo yaliyotayarishwa vizuri mikutanoni na kushiriki katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Kwa kutumia kwa manufaa fursa hizi kutia wengine moyo, twatoa mchango wenye thamani katika hali ya kiroho ya kutaniko, na hilo huongezea uwezo wa kutimiza kazi ambayo kutaniko limekabidhiwa.
5 Kwa kweli, sisi sote twahitajiwa ili kutimiza kazi. Mtu yeyote asihisi kwamba hahitajiwi. Jitihada zetu za pamoja, ziwe kubwa au ndogo, katika kumtumikia Yehova hututofautisha kuwa waabudu pekee wa kweli wa Mungu. (Mal. 3:18) Kila mmoja wetu anaweza kuwa na sehemu ya maana katika kumheshimu Yehova na kusaidia wengine wamjue na kumtumikia.