Sanduku La Swali
◼ Wazazi wanapaswa kuwa waangalifu kuhusu mambo gani watoto wao wadogo wanaposhiriki katika utumishi wa shambani?
Wazazi Wakristo huandamana ifaavyo pamoja na watoto wao katika huduma ya shambani, wakiwazoeza kushiriki habari njema za Ufalme na wengine. Katika kufanya hivyo, kuna uhitaji wa kuangalia kwa makini watoto wao kwa sababu ya hatari zinazoweza kutokea katika eneo, hata katika ujirani “ulio salama zaidi.” Mara nyingi, watoto hutendwa kijeuri na kutendwa vibaya kwa sababu ya ongezeko la pupa na upotovu wa kingono katika hizi “nyakati za hatari” tunamoishi. (2 Tim. 3:1-5) Wazazi wanahitaji kuwa waangalifu ifaavyo ili kuwalinda watoto wao na wale ambao wangewasumbua. Ni nini liwezalo kufanywa?
Biblia hushauri kwa hekima kwamba tuwe waangalifu na kufikiria mapema kuona hatari. (Mit. 22:3; Mt. 10:16) Hatukusudii kutoa sheria, lakini ni jambo la hekima mzazi au mtu mwingine mzima kuandamana na mtoto anaposhiriki katika utumishi wa shambani. Wahubiri wawili wachanga wenye kuwajibika wakihubiri pamoja, yafaa mzazi au mtu mwingine mzima awaangalie nyakati zote. Bila shaka, mtoto awapo mkubwa zaidi na kuwa mwenye kuwajibika, wazazi wanaweza kuamua kama anahitaji usimamizi kidogo wa moja kwa moja kutoka kwa wazazi.—Ona pia Sanduku la Swali la Huduma ya Ufalme Yetu ya Oktoba 1992.
Pia ni jambo la hekima kujali usalama sikuzote mnaposafiri kwa gari au mnapotembea-tembea. Kuwa wenye tahadhari ifaavyo mara nyingi huzuia aksidenti na maumivu yenye kulemea, gharama za kitiba, na uwezekano wa kuwajibika kisheria katika ulimwengu wenye kupenda mashtaka unaotuzunguka.
Inafaa vijana “walisifu jina la BWANA [“Yehova,” NW] .” (Zab. 148: 12, 13) Maneno yao yenye uvutio mwingi na mwenendo wao mzuri katika huduma ya shambani huwavutia wengine na kumletea Yehova heshima. Wazazi, kwa vyovyote vile, saidieni watoto wenu washiriki kwa ukawaida kutangaza habari njema, huku mkiwa chonjo daima pia kuwalinda kutokana na hatari zozote zilizoko zinazoweza kutokea!