Sanduku La Swali
◼ Ni kwa kadiri gani watoto wa wazazi Wakristo wanaweza kushiriki katika utumishi wa shambani kabla ya wao kutambuliwa kuwa wahubiri wasiobatizwa?
Wazazi Wakristo wanataka watoto wao wakue wawe watumishi wakomavu, waliojitoa kwa Yehova. (1 Sam. 2:18, 26; Lk. 2:40) Hata katika umri mchanga sana, watoto katika nyumba za Wakristo wanapaswa waweze kutoa maelezo ya waziwazi kwa kutetea imani yao yenye msingi wa Biblia. Ukuzi wa kiroho wa watoto huongezewa mwendo wanapoandamana na wazazi wao katika utumishi wa shambani kuanzia utoto. Lakini ni jambo la maana kwa wachanga kuchochewa kutoka moyoni ikiwa watafurahia utumishi wa shambani, watamani kuwa wahubiri wasiobatizwa, na kuendelea kushiriki katika kazi ya kuhubiri Ufalme. Mazoezi ya uangalifu yakitolewa na wazazi yanahitajiwa. (1 Tim 4:6; 2 Tim. 2:15) Wahubiri wengine wanaostahili wanaweza kusaidia nyakati nyingine ikiwa wazazi wanakubaliana na jambo hilo.—Ona Huduma Yetu, kurasa 99-100.
Watoto wenye tabia njema waandamanapo na wazazi wao Wakristo katika kazi ya nyumba kwa nyumba, wao hujifunza jinsi ya kushiriki hudumani. Lakini wao hawatatambuliwa kuwa wahubiri wasiobatizwa hadi wanapositawisha kiasi fulani cha uwezo na ustadi wao wenyewe. Wazazi Wakristo wanaweza kuamua ni kwa kadiri gani mtoto anaweza kushiriki kutoa ushahidi wanapofanya kazi pamoja. Watoto ambao bado hawajatambuliwa kuwa wahubiri wasiobatizwa hawapaswi kufanya ziara peke yao au kuandamana na watoto wengine katika utumishi wa shambani. Wazazi wanaweza kuwatayarisha watoto wao kwa ajili ya utumishi wa shambani na kuwaruhusu washiriki katika njia mbalimbali, kama vile kusoma andiko, kutoa trakti au gazeti, au kumwonyesha mwenye nyumba kielezi katika kimojapo vichapo. Kadiri mtoto akuavyo, huenda akaweza kushiriki katika mazungumzo kwa kiwango kikubwa zaidi.
Kwa mazoezi yanayofaa, wachanga hujifunza kuthamini uzito wa huduma wanapoitikia mwelekezo wa wazazi wao na kujiendesha wenyewe katika njia yenye utaratibu. Wazazi hawapaswi kuwaacha watoto wao ambao bado hawajatambuliwa kuwa wahubiri wasiobatizwa kwenye mikutano ya utumishi wa shambani, wakiwatazamia wengine wawatunze. Wazazi wenye kuhangaikia hutambua daraka lao la kibinafsi la kuongoza utendaji wa watoto wao. Bila shaka, wahubiri wengine wenye uwezo wa kuchukua daraka huenda wakataka kusaidia katika kuzoeza watoto wadogo kundini wanaoonyesha kupendezwa kikweli kumtumikia Yehova katika huduma.