Sanduku La Swali
◼ Je, wahubiri na mapainia wanapaswa kuhisi kwamba wana wajibu wa kutoa michango kwa ajili ya kazi ya Sosaiti ya ulimwenguni pote kila mara wanapochukua vichapo vya utumishi wa shambani kwenye Jumba la Ufalme?
La. Wahubiri wanaweza kutoa michango yao wenyewe ya kutegemeza kazi ya ulimwenguni pote kulingana na uwezo wao na tamaa yao, wakati wowote wanapochagua kufanya hivyo.—2 Kor. 8:10-15; 9:6-14.
Hata hivyo, wahubiri fulani wamechagua kutoa michango yao wakati wanapochukua vichapo. Wao hufanya hivyo kwa sababu kuchukua vichapo huwa kama kikumbusha kinachofaa cha pendeleo lao na daraka lao la kutegemeza kazi ya ulimwenguni pote kwa ukawaida. Wengine hutoa michango yao binafsi pamoja na michango ya hiari wanayopokea kutoka kwa watu wanaopendezwa waliowapata katika huduma ya shambani. Wengi wameamua kutoa michango hususa kila juma. Na hata wengine huweka kando kiasi fulani kila mwezi kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote, kama wafanyavyo kwa ajili ya gharama nyingine za Jumba la Ufalme. Tunapotoa michango, kila mmoja anapaswa kuazimia kile ambacho atafanya ili kutegemeza kazi ya ulimwenguni pote.