“Nyakati za Hatari Zilizo Ngumu Kushughulika Nazo”—Tunaweza Kukabilianaje Nazo?
1 Kuzorota kwa uchumi, kufutwa kazi, ukosefu wa kazi ya kuajiriwa, na kufilisika ni maneno yajulikanayo sana siku hizi. Ingawa hivyo, watumishi wa Yehova ambao “si sehemu ya ulimwengu” uliotengwa mbali na Mungu, wanalazimika kuishi katika ulimwengu ulio na msukosuko wa kiuchumi. (Yn. 17:15, 16; 1 Kor. 7:31) Ili kuonyesha hangaiko la hali hiyo, waangalizi fulani wasafirio waliandikiwa waeleze wazi kuhusu matatizo ambayo akina ndugu hukabili, jinsi wanavyokabiliana nayo, na msaada na ushauri unaohitajiwa.
2 Kwa akina ndugu wengi, kuzorota kwa uchumi kunakotukia sasa kumewafungulia fursa za kupanua utendaji wao wa Kikristo. Wengine wametumia wakati wao wa ziada kujitolea katika programu yetu ya karibuni ya ujenzi wa Jumba la Ufalme, na wanapongezwa kwa kufanya hivyo. Wengine wamekuwa mapainia-wasaidizi na wa kawaida. Roho ya kujitolea inatia moyo!
3 Kwa upande mwingine, wengine wameona likiwa jambo gumu kusitawisha usawaziko wanapokabili matatizo ya kiuchumi. Wakristo wote walio vichwa vya familia wana daraka zito la kuandalia familia zao utunzi wa kutosha. (1 Tim. 5:8) Lakini hangaiko la kutafuta riziki limesababisha mkazo katika ndoa kadhaa. Ukosefu wa kazi ya kuajiriwa na kufutwa kazi kumeongeza wasiwasi, kukifanya wengi wavunjike moyo. Kwa kusikitisha, katika hali hizo, maoni ya Mkristo kuhusu kutokamilika kwa ndugu zake yanaweza kukosa usawaziko na kutokeza kutokuelewana na kupunguza bidii yake katika utumishi wa Ufalme. Mwenye kusimamia mambo hayo, bila shaka akifurahia, ni adui mkuu wa Yehova, “mungu wa huu mfumo wa mambo,” Shetani Ibilisi. Basi je, waweza kufanya nini ili udumishe uaminifu-maadili na uendelee kuwa mwenye nguvu kiroho katika “nyakati [hizi] za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo”?—Mit. 27:11; 2 Kor. 4:4; 2 Tim. 3:1.
4 ‘Dumisha Jicho Sahili’: Fikiria maana ya maneno haya ya Yesu: “Taa ya mwili ni jicho. Basi, ikiwa jicho lako ni sahili, mwili wako wote utakuwa mwangavu.” (Mt. 6:22) Naam, twapaswa kujizoeza maisha sahili, “kukaza macho yetu juu ya masilahi ya Ufalme tu, kufanya kila jambo jinginelo liwe la pili.” (Mnara wa Mlinzi, Julai 15, 1989, ukurasa wa 14) Hilo lawezekanaje?
5 Katika miongo iliyopita, familia nyingi za Kikristo zimeweza kudumisha kiwango cha maisha chenye kustarehesha bila taabu nyingi. Tokeo likawa kwamba, “ndugu zetu mara nyingi wamekuwa na tatizo la kuelewa ‘maisha sahili’ yanamaanisha nini hasa kwa sababu walio wengi hawajalazimika kupunguza matumizi yao katika njia kubwa,” aripoti mwangalizi mmoja asafiriye. Kwa sababu ya kuishi katika jamii yenye kuhangaikia mambo ya kimwili na starehe, ndugu hao wameruhusu hisia zao zitiwe ganzi na ulimwengu huu wenye kuendeleza mtindo wa maisha ya anasa.
6 Unaposihiwa kuishi maisha sahili, waonaje jambo hilo? Labda wasababu kwamba hufanyi vibaya sana, maisha yako yakilinganishwa na ya jirani yako, kwa kweli si yenye mambo mengi mno, una tumaini la wakati ujao. Kumbuka kielelezo kilichotolewa katika Mnara wa Mlinzi: “Wakristo wanaotii shauri la Yesu kutafuta kwanza Ufalme wa Mungu wanasonga mbele kwa mwendo mzuri katika funzo la Biblia lenye ukawaida, hudhurio la mikutano, na huduma ya shambani. Msogeo huo wa mbele ni himaya ya kweli dhidi ya kuanguka. Waweza kulinganisha na kuendesha baiskeli. Wale ambao wamepata kujaribu kusawazisha baiskeli ambayo imepunguza mwendo ikawa ni kama imesimama kabisa huthamini umaana wa kujichochea kusonga mbele. Vivyo hivyo, maadamu wewe unasonga mbele kwa mwendo mzuri katika kawaida fulani ya utendaji wa kiroho, unapata himaya usipoteze usawaziko wako na kuanguka.”—Flp. 3:16.
7 Badala ya kutia maanani jinsi ya kudumisha kiwango chako cha maisha, kwa nini usifikirie jinsi ya kusahilisha mtindo wako wa maisha? Baada ya kutukumbusha tuwe macho, Mnara wa Mlinzi lilitusihi tusisahau kwamba “kujiondolea mizigo ya mambo kwaweza kuturuhusu wakati mwingi zaidi wa kujifunza, wa kutayarisha mikutano, na wa kusaidia wengine. ‘Kila nishawishwapo kununua kitu fulani nisichohitaji, au kuanza kazi nisiyohitaji,’ akasema Mkristo mmoja [mfanyakazi], ‘mimi hujizuia kwa kikumbusha cha kwamba sahilisha mambo. Nyakati fulani mimi hujilazimisha kujinyima mambo fulani.’ Je! hicho si kikumbusha chema kwetu sote? Ufikiriapo mradi fulani, labda kujenga nyongeza kwa nyumba yako au kitu kingine, mbona usijiulize hivi: Je! kitu hiki kitachangia hali yangu ya kiroho na ile ya jamaa yangu au kitaizuia? Je! mimi navihitaji kweli kweli vitu vyote ambavyo walimwengu huvifuatia kwa hamu nyingi, au naweza kukaa bila?” (Mnara wa Mlinzi, Julai 15, 1989, ukurasa wa 12) Kile ambacho huenda tukawa tumezoea huenda kisiwezekane tena kiuchumi, wala huenda hata lisiwe jambo la hekima hali za uchumi zinapobadilika-badilika.
8 Pia, ndugu kadhaa wamefilisika kwa kununua vitu vingi kupita kiasi kwa kutumia kadi za mkopo. Kutumia bila hekima kadi za mkopo kumeleta matatizo mengi sana. Ni afadhali kuweka akiba ya fedha, kisha uwe na pesa za kutosha kuweza kununua kitu kwa pesa taslimu. Kwa kweli, uhitaji wa kungoja kabla ya kununua vitu umesaidia wengi watambue kwamba walichopanga kununua hakikuwa cha lazima.
9 Weka Kielelezo Chema: Wewe binafsi unaweza kufanya mengi ili kusaidia washiriki wa familia yako. Fundisha watoto wako umuhimu wa kutumia pesa kwa njia inayompendeza Yehova. Wasaidie pia wasitawishe ‘jicho sahili.’ Kazia mambo ya kiroho wala si ya kilimwengu. Kumbuka kwamba, vijana watakuiga. Jinsi wanavyotumia pesa zao huenda ikaonyesha jinsi unavyotumia mali zako. Jiulize, Je, mimi hutenga pesa kwa ajili ya michango ya kawaida ya kazi ya Ufalme? Je, mimi hutimiza kwa uaminifu ahadi zangu za kifedha za kutegemeza utunzaji wa Jumba la Ufalme, mapainia wa pekee, mishonari, na kazi ya Ufalme ya ulimwenguni pote? Hasa sasa tunapotoa vichapo kwa njia ya michango, twataka kukumbuka kwamba kazi ya ulimwenguni pote yategemezwa na michango yetu.
10 Sisi huwawekea vijana wetu mtindo gani wa maisha? Je, twawatia moyo wachukue mkopo wenye kufilisisha ili wawe na nyumba yao wenyewe? Je, twawapendekezea wenzi wa ndoa waliooana hivi karibuni wawe na vitu vyote vya nyumbani vya kisasa mara tu wafungapo ndoa? Je, maneno yetu huwatia moyo watumie miaka yao ya kwanza ya ndoa katika utumishi wa wakati wote? Je, mitazamo hiyo yasaidia vijana wajenge maisha yao kwenye msingi imara? Kwa sababu ya uharaka wa nyakati tunamoishi, ni jambo la hekima kama nini kuchochea maisha yaliyo imara kiroho, yaliyo sahili!—Flp. 1:27.
11 Tenda kwa Busara Katika Shughuli za Kibiashara: Katika miezi ya hivi karibuni yenye uchumi usioimarika, wale ambao wamefanya maisha yao yawe sahili wameiweza hali. Twatambua ukweli wa onyo la Paulo: “Msiongozwe vibaya: Mungu si wa kudhihakiwa. Kwa maana lolote lile mtu analopanda, hilo atavuna pia.” (Gal. 6:7) Matatizo yoyote ya kiuchumi tunayokabili sasa huenda ikawa ni kwa sababu tumekosa kutenda kwa busara. “Mwenye busara huyaona mabaya na kujificha; bali wajinga huendelea mbele wakaumia.” (Mit. 22:3) Basi, kila mmoja wetu anaweza kufanya nini ili kuhakikisha kwamba anaendelea kutenda kwa busara?
12 Kielelezo cha Yesu chathibitika kuwa chenye kufaa kabisa: “Ni nani kati yenu atakaye kujenga mnara asiyeketi kwanza na kupiga hesabu ya gharama, ili aone kama ana kiasi cha kutosha kuukamilisha? Kama sivyo, yeye angeweza kuuwekea msingi lakini asiweze kuumaliza, na watazamaji wote wangeweza kuanza kumdhihaki, wakisema, ‘Mtu huyu alianza kujenga lakini hakuweza kumaliza.’ ” (Luka 14:28-30) Naam, lazima tupige hesabu ya gharama ya shughuli ya kibiashara. Lakini huenda ukauliza, ni nani ambaye angeweza kuona kimbele jinsi ambavyo nyakati hizi zingekuwa ngumu?
13 Ni nini kilichotokea wakati shamba la mtu mmoja tajiri lilipozaa sana? Alisababu kwamba kama angebomoa ghala zake na kujenga kubwa zaidi, basi angeweza kusema: “Nafsi, wewe una vitu vyema vingi vilivyolimbikwa kwa miaka mingi; starehe, kula, kunywa, jifurahishe mwenyewe.” Lakini Mungu alimwambiaje? “Wewe mwenye kukosa akili, usiku huu wanadai nafsi yako kutoka kwako. Ni nani, basi, atakayepaswa kuwa na vitu ulivyoviweka akiba?” Na tunaweza kujifunza somo gani hapa? Yesu aeleza: “Hivyo ndivyo huwa kwa mtu ajilimbikiaye hazina mwenyewe lakini si tajiri kuelekea Mungu.” Basi kumbuka kwamba, ni muhimu tuchunguze kile tunachofikiria kufanya, kulingana na maoni ya Yehova!—Luka 12:16-21.
14 Mtume Paulo hutusaidia tuelewe maoni yanayofaa alipomsihi Timotheo hivi: “Kwa hakika, huo ni njia ya kupata faida kubwa, ujitoaji-kimungu huu pamoja na ujitoshelevu. Kwa maana hatukuleta kitu katika ulimwengu, wala hatuwezi kupeleka kitu chochote nje. Kwa hiyo, tukiwa na riziki na cha kujifunika, tutakuwa wenye kuridhika na vitu hivi.” Ona onyo aliloongezea Paulo: “Hata hivyo, wale waazimiao kuwa matajiri huanguka ndani ya kishawishi na mtego na tamaa nyingi zisizo za akili na zenye kuumiza, ambazo hutumbukiza watu ndani ya uharibifu na uangamizo.”—1 Tim. 6:6-9.
15 Epuka kutumia fedha kupita kiasi. Jifunze kutokana na kielelezo cha Yosefu huko Misri. Wakati ulipofaa aliweka akiba. Kisha mambo yalipobadilika, alikuwa na yale yaliyohitajika hata akawasaidia wengine. Kwa hiyo weka katika bajeti yako akiba ya kutosha kwa ajili ya wakati wa taabu.—Mwa. 41:46-57.
16 Omba Msaada: Hali ya uchumi usioimarika ulimwenguni kwa hakika inaweza kuathiri hali ya kiroho ya mtu. Tufanye nini basi? Tii ushauri wa mwanafunzi Yakobo: “Acheni aendeleze sala. . . . Acheni awaite kwake wanaume wazee wa kutaniko.” Wazee wa kutaniko kwa kweli hutumika wakiwa chanzo cha faraja na msaada katika maisha. “Acheni wasali juu yake,” Yakobo ashauri, “wakimpaka mafuta katika jina la Yehova. Na sala ya imani itamfanya huyo asiyejisikia vizuri apone, na Yehova atamwinua.”—Yak. 5:13-16.
17 Wazee, onyesheni huruma. Sitawisheni namna ya kufikia watu inayochochea tumaini. Kufanya hivyo kutafanya walioshuka moyo wawajie. Kisha “semeni kwa kuliwaza.” (1 The. 5:14) Hakuna haja kamwe ya kukemea watu au kuwakaripia. Hakuna faida kukazia jinsi ambavyo mtu amekosa hekima. Badala yake tieni moyo. Pongezeni waaminifu. Toeni ushauri utakaosaidia kutatua matatizo. Saidieni mtu atengeneze bajeti itakayotumika. Inapohitajika, saidieni kutafuta msaada unaotolewa na serikali kisha msaidie pia kujaza fomu za madai. Bila shaka, hali za kiuchumi zinapofanya ndugu awe na uhitaji mkubwa, kumbukeni daraka lenu la Kimaandiko la kujulisha wazee wenzenu ili muamue ni msaada gani mtakaotoa.—Yak. 2:15-17.
18 “Dhiki kubwa” ikaribiapo na hali ya uchumi ya ulimwengu huu ikaribiapo kuanguka, sisi sote na tukimbilie tumaini la Ufalme! Kumbuka ahadi ambayo Yehova alimpa Baruku mwandishi wa Yeremia. Badala ya ‘kutafuta mambo makuu’ sasa, kazia macho yako kwenye masilahi ya Ufalme kwa kuwa ni “nafsi yako,” uhai wako, ambao Yehova anakuhakikishia kuuokoa.—Yer. 45:5, NW; Mt. 24:21, 22.