Utoaji Ulio Rahisi Ndio Bora
1 Kwa nini watu huvutiwa na ujumbe wa Ufalme wanapohubiriwa na wahubiri wachanga? Sababu moja ni kwamba maelezo yao ni rahisi. Wahubiri fulani huhisi kwamba ili kuhubiri kwa matokeo wanahitaji utoaji wenye mambo mengi. Hata hivyo, mambo yaliyoonwa yaonyesha kwamba utoaji rahisi na ulio wazi ndio bora.
2 Yesu alitangaza Ufalme wa Mungu kwa njia rahisi, ya moja kwa moja na akazoeza wanafunzi wake kufanya vivyo hivyo. (Mt. 4:17; 10:5-7; Luka 10:1, 9) Alitumia utangulizi rahisi, maswali, na mifano inayovuta fikira za wasikilizaji wake na kuwafikia mioyo. (Yn. 4:7-14) Itafaa tuige kielelezo chake na kuhubiri kwa njia iliyo rahisi kueleweka.
3 Tunapaswa kutangaza ujumbe wa ‘Habari njema ya Ufalme.’ (Mt. 24:14) Ukitumia Ufalme kuwa kichwa cha msingi wa mazungumzo yako, utoaji wako utakuwa rahisi. Zungumzia mambo yanayohangaisha wasikilizaji wako. Mara nyingi wanawake hupendezwa na familia yao kuliko mambo ya kisiasa. Akina baba nao huhangaishwa na kazi ya kuajiriwa na usalama wa familia zao. Vijana nao hupendezwa na wakati wao ujao, watu wazee hupendezwa na afya bora na usalama wao. Kwa kawaida watu huhangaikia matukio ya kwao kuliko ya nchi za mbali. Baada ya kuzungumza juu ya mambo mnayokubaliana, elekeza fikira kwenye baraka ambazo wanadamu watiifu watafurahia chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu. Maneno machache yaliyo rahisi, yakiambatana na andiko, yanaweza kuwa njia bora zaidi ya kuchochea upendezi wa msikilizaji wako.
4 Unaweza kuanzisha mazungumzo kwa kusema hivi:
◼ “Labda utakubali kwamba wanadamu wamepatwa na magonjwa mengi yasiyo na tiba. Je, ulijua kwamba Mungu ameahidi hivi karibuni kuwa ataondoa aina zote za magonjwa, hata kifo?” Ngoja akujibu, kisha usome Ufunuo 21:3, 4.
5 Na ufikie akili na mioyo ya watu wengi zaidi katika eneo lenu kwa utoaji ulio wazi na rahisi, ukiwasaidia wajifunze juu ya Yehova na taraja la kufurahia uhai udumuo milele.—Yn. 17:3.