Hubiri Ukiwa Jirani Mwema
1 Yesu alisema “umpende jirani yako kama wewe mwenyewe.” (Mt. 22:39) Bila shaka, ‘unafanya lililo jema’ kuelekea waamini wenzako, lakini je, unaweza kupanua upendo wako kuelekea watu wanaoishi karibu nawe? (Gal. 6:10) Kwa njia zipi?
2 Kwa Kujitambulisha: Je, jirani zako wanajua kwamba wewe ni Shahidi? Ikiwa hawajui, kwa nini usiwahubirie unapokuwa katika utumishi wa shambani? Huenda ukashangazwa na matokeo yake! Au kama ukiona ni rahisi zaidi, jaribu kuwahubiria kivivi hivi. Ukiwa nje ya nyumba, huenda ukawaona wakifanya kazi katika uwanja wa nyumba yao au kutembea kistarehe barabarani. Wasalimu kwa tabasamu changamfu. Jitahidi kuongea juu ya imani yako. Waambie mahali ambapo Jumba la Ufalme lipo, na kinachoendelea huko, na uwaambie kuhusu yeyote katika ujirani ambaye huhudhuria.Waalike kwenye mikutano. Azimia kutangazia kila mtu unayemjua habari njema.—Mdo. 10:42; 28:23.
3 Kwa Mfano Wako Mzuri: Ujirani wako mwema huonyesha mengi kukuhusu na huenda ukafungua njia ya kutoa ushahidi. Pia ‘huremba fundisho la Mungu.’ (Tito 2:7, 10 ) Pendezwa kabisa na jirani zako. Uwe mwenye urafiki na huruma. Heshimu haki yao ya kuwa na faragha na mazingira yasiyo na kelele. Mmoja wao akiwa mgonjwa, uwe mwenye huruma na usaidie. Familia mpya ikihamia kwenye ujirani, wakaribishe. Matendo hayo yenye fadhili yanampendeza Yehova na kuwafanya jirani wawe na maoni mazuri.—Ebr. 13:16.
4 Kwa Kutunza Mali Yako: Kuwa jirani mwema hutia ndani kutunza nyumba yako ili ionekane yenye kupendeza. Nyumba na uwanja safi wenye kuvutia hutoa ushahidi bila maneno. Lakini nyumba chafu au iliyo na vitu vilivyotupwa-tupwa ovyoovyo kwa kweli haitafanya ujumbe wa Ufalme uvutie. Kwa hiyo, ni muhimu sana nyumba yako, uwanja, na magari yawe safi na katika hali nzuri.
5 Kuwajali wale wasio wa kutaniko la Kikristo huonyesha kwamba unawapenda jirani zako. Huenda matokeo yakawa nini? Huenda ikawa kwamba kwa sababu ya “kazi zenu bora ambazo wamekuwa mashahidi wa kujionea,” baadhi yao ‘wakamtukuza Mungu.’—1 Pet. 2:12.