Watu Wenye Furaha Zaidi Duniani
1 “Heri watu wenye BWANA [“Yehova,” NW] kuwa Mungu wao.” (Zab. 144:15) Maneno hayo yanaonyesha Mashahidi wa Yehova kuwa watu wenye furaha zaidi duniani. Hakuna shangwe kuu kupita ile ya kumtumikia Mungu wa pekee wa kweli na aliye hai, Yehova. Kwa kuwa yeye ni “Mungu mwenye furaha,” wale wanaomwabudu huiga furaha yake. (1 Tim. 1:11) Ni baadhi ya mambo gani ya ibada yetu ambayo hutufanya tuwe na furaha zaidi?
2 Sababu za Kuwa Wenye Furaha: Yesu alituhakikishia kwamba furaha hutokana na “kuona uhitaji [wetu] wa kiroho.” (Mt. 5:3) Kuendelea kujifunza Biblia na kuhudhuria mikutano yote ya Kikristo hutosheleza uhitaji huo. Kujifunza kweli ya Neno la Mungu kumetuweka huru na mafundisho ya uwongo na makosa ya dini. (Yn. 8:32) Maandiko pia yametufundisha njia bora ya kuishi. (Isa. 48:17) Kwa sababu hiyo, twafurahia ushirika wa Kikristo wenye kujenga pamoja na ndugu zetu wenye furaha.—1 The. 2:19, 20; 1 Pet. 2:17.
3 Twaridhika kabisa tunapotii viwango vya juu vya adili vya Mungu, kwa kuwa twajua vinatulinda na kumfurahisha Yehova. (Mit. 27:11) Mwandishi mmoja wa gazeti alisema hivi: “Wajapokuwa na viwango vya juu sana, Mashahidi wa Yehova huonekana kuwa wenye furaha. Vijana kwa wazee [miongoni mwao] huonekana kuwa na furaha na usawaziko usio wa kawaida.” Twaweza kusaidiaje wengine wawe na furaha kama yetu?
4 Saidia Wengine Wapate Furaha: Ulimwengu umejawa na ukosefu wa furaha, na watu kwa ujumla wanaonekana kuwa hawana tumaini zuri la wakati ujao. Hata hivyo, sisi tuna mtazamo mzuri, tukijua kwamba siku moja huzuni yote itakwisha. (Ufu. 21:3, 4) Kwa hiyo, twahubiri kwa bidii, tukitafuta watu wenye mioyo minyofu, ambao twaweza kuwaambia kuhusu tumaini letu na imani yetu juu ya Yehova.—Eze. 9:4.
5 Dada mmoja painia alisema: “Hakuna jambo lenye kuridhisha zaidi kuliko kusaidia watu kumjua Yehova na kweli yake.” Na tufanye yote tuwezayo ili tutie wengi moyo wakubali mafunzo ya Biblia. Kumtumikia Yehova na kujitolea kusaidia wengine wamtumikie, huleta furaha nyingi sana.—Mdo. 20:35.