Kuvaa na Kujipamba kwa Kiasi
1 “Wanaume wote, hata wavulana wachanga, huvaa tai. Wote, wanawake kwa wasichana, matineja kwa wadogo, huvaa rinda au skati. Hakuna mtu anayevaa mavazi aina ya jinzi (jeans) au shati bila tai. Kila mtu hapa ni mwenye furaha.” Ndivyo lilivyosema gazeti moja. Lilikuwa likifafanua watu gani? Wanasiasa? Wanamichezo? Maonyesho ya roki? La hasha! Lilikuwa likifafanua akina ndugu na dada kwenye kusanyiko kubwa la wilaya mwaka uliopita.
2 Katika jiji lingine ambamo kusanyiko lilifanywa, mwandishi mmoja wa gazeti aliwafafanua Mashahidi hivi: “Wanaume wote ni safi na wanavaa suti na tai. Wanawake nao wamevaa kwa kiasi lakini maridadi.” Mlinzi mmoja alisema: “Nyinyi mna adabu, mna heshima, watu safi, na nadhifu. Mnavutia sana. Katika ulimwengu huu mchafu, mmeweza kuondolea mbali uchafu!” Hayo ni maelezo bora kama nini kutuhusu! Je, hatushukuru kwamba udugu wetu waweza kusemwa vema namna hiyo? Bila shaka, Mashahidi wote walichangia ripoti hiyo nzuri kwa mfano wao mzuri.
3 Tumejulikana ulimwenguni pote kwa kuwa sisi ni tofauti sana. (Mal. 3:18) Kwa nini? Kwa sababu twatii shauri la Kimaandiko la ‘kujiremba wenyewe katika mavazi yenye mpangilio mzuri, pamoja na kiasi na utimamu wa akili, katika njia inayofaa wale wanaodai kumstahi Mungu.’—1 Tim. 2:9, 10.
4 Mavazi na Mapambo Yako Yanaonyesha Wewe Ni Mtu wa Aina Gani? Mavazi tunayovaa na jinsi tunavyoyavaa huonyesha jinsi tulivyo—imani yetu , mitazamo yetu, na nia zetu. Mitindo tunayochagua huonyesha sisi ni nani na tunaamini nini. Hatupaswi kamwe kukubali mawazo na mwenendo uliopotoka unaopendwa sana na ulimwengu. Hangaikio letu si kama mtindo fulani ni wa karibuni zaidi bali kama unamfaa mtu anayedai kuwa mhudumu wa Mungu. (Rom. 12:2) Badala ya kujipamba kwa njia ambayo huonyesha roho ya kujitegemea au inayoonyesha maisha yasiyo na adili, twataka kuonyesha kwamba ‘twamtukuza Mungu.’—1 Pet. 2:12.
5 Nyakati nyingine, huenda mtu mpya, asiye na uzoefu, au aliye dhaifu kiroho akakubali kile ambacho ulimwengu huchochea katika mavazi na mapambo bila kufikiria kwanza jinsi watu watakavyofikiri kuhusu Yehova na tengenezo lake. Sisi sote twaweza kujichunguza wenyewe tuone kama tumeathiriwa na mawazo ya ulimwengu huu. Twaweza kumwendea ndugu au dada mkomavu mwenye kuheshimiwa tumwulize atoe maoni yenye unyofu kuhusu mtindo wetu wa mavazi na mapambo kisha tufikirie kwa uzito madokezo yake.
6 Wengine wanakubali kwamba wanapaswa kuwa waangalifu kuhusu jinsi wanavyovaa wanapohudhuria kusanyiko. Lakini wanashusha kiwango chao wakati wa shughuli za starehe baada ya programu ya siku kwisha. Dumisha kiwango cha juu kinachostahili kudumishwa na wahudumu Wakristo. (2 Kor. 6:3, 4) Mahali popote twendapo hadharani, beji za kusanyiko letu pamoja na mavazi na mapambo yetu hututambulisha kuwa Mashahidi wa Yehova. Kwa hiyo, mavazi yetu yapasa sikuzote kuwa yenye mpangilio mzuri na yenye kiasi, yakionyesha kwamba sisi “si sehemu ya ulimwengu.”—Yn. 15:19.
7 Acheni tufanye yote tuwezayo kwenye Kusanyiko la Wilaya la “Watangazaji wa Ufalme Wenye Bidii” la mwaka huu ili tuthibitishe kwamba sisi ni ‘watu watakatifu kwa Yehova Mungu wetu.’ Kwa kufanya hivyo, tutaongeza “sifa na jina, na heshima” kwa Yehova.—Kum. 26:19.
[Sanduku katika ukurasa wa 6]
Jinsi ya Kumtukuza Yehova:
■ Valia jinsi mhudumu wa Mungu anavyostahili kuvaa.
■ Epuka mitindo inayofuata roho ya ulimwengu.
■ Onyesha sifa ya kiasi, inayoonyesha utimamu wa akili.