Sanduku la Swali
◼ Ni mavazi gani yanayofaa tunapotembelea majengo yanayotumiwa kwa ajili ya utumishi wa Yehova?
Kuzunguka ulimwengu, Majumba ya Ufalme, Majumba ya Kusanyiko, makao ya Betheli, na ofisi za tawi ni majengo ya pekee yaliyowekwa wakfu kwa ajili ya utumishi wa Yehova. Hayo si majengo ya kifahari, lakini ni majengo safi, maridadi, na yenye kuheshimika. Yanatofautiana sana na majengo mengi katika mfumo wa Shetani. Wale wanaotembelea majengo yanayotumiwa kwa ajili ya utumishi wa Yehova wanapaswa kutambuliwa kuwa watu wa Yehova, watu wanaofanya mapenzi yake.
Tukiwa Wakristo, “tunajipendekeza kuwa wahudumu wa Mungu” katika kila njia, kutia ndani kuvalia na kujipamba kwa njia inayofaa na kwa mpangilio mzuri. (2 Kor. 6:3, 4) Pia, tunatazamiwa kujiendesha kwa njia inayofaa. Nyakati zote tunapaswa kuvalia na kujipamba kwa njia nadhifu na yenye kuheshimika kama inavyowastahili watumishi wa Yehova Mungu. Hilo linafaa hasa tunapotembelea makao makuu huko New York na pia ofisi za tawi ulimwenguni pote.
Kikizungumzia umuhimu wa kuvaa na kujipamba kwa njia inayofaa, kitabu Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova kinaeleza kuhusu usafi wa kimwili, kiasi katika mavazi, na kujipamba inavyofaa tunapohubiri na tunapohudhuria mikutano ya Kikristo. Kisha, kinasema hivi katika ukurasa wa 139, fungu la 1: “Kumbuka, jina Betheli linamaanisha ‘Nyumba ya Mungu.’ Kwa hiyo, tunapaswa kuvalia, kujipamba, na kujiendesha kama tunavyofanya tunapohudhuria mikutano ya ibada katika Jumba la Ufalme.” Kiwango hicho cha juu kinapaswa kuzingatiwa na wahubiri wa Ufalme wanaokuja kutembelea Betheli iwe wanatoka maeneo ya karibu au ya mbali. Kwa kufanya hivyo, wageni hao wataonyesha uthamini wao na heshima inayofaa.—Zab. 29:2.
Mavazi yetu yanapaswa kututambulisha kuwa watu “wanaodai kumheshimu Mungu.” (1 Tim. 2:10) Kuvaa na kujipamba kwa njia inayofaa kunawafanya watu wawe na maoni mazuri kuhusu ibada ya kweli ya Yehova. Hata hivyo, imeonekana kwamba wanapotembelea majengo yanayotumiwa kwa ajili ya utumishi wa Yehova, ndugu na dada wachache wanavaa mavazi ya kupita kiasi, ya kishaghalabaghala, na yasiyositiri. Mavazi kama hayo hayamfai Mkristo wakati wowote ule. Katika jambo hili na katika sehemu nyingine zote za maisha ya Kikristo, tunatamani kudumisha viwango vinavyotofautisha watu wa Mungu na ulimwengu, tukifanya mambo yote kwa utukufu wa Mungu.—Rom. 12:2; 1 Kor. 10:31.
Hivyo unapotembelea makao makuu na ofisi ya tawi katika Jimbo la New York au unapotembelea ofisi nyingine za tawi, iwe ulipanga kutembelea maeneo hayo au unayatembelea ukiwa katika safari za utalii, jiulize: ‘Je, nimevaa na kujipamba kwa kiasi, kwa njia nadhifu, na kwa heshima inavyostahili mahali ambapo ninataka kutembelea? Je, ni kwa njia itakayomletea Yehova heshima? Je, mavazi na mapambo yangu yatawakengeusha au kuwaudhi wengine?’ Nyakati zote na ‘tulipambe fundisho la Mwokozi wetu, Mungu, katika mambo yote,’ kupitia mavazi na mapambo yetu!—Tito 2:10.