Tosheleza Mahitaji Yako ya Kiroho
1 Kusanyiko letu la Wilaya linalokuja la “Watangazaji wa Ufalme Wenye Bidii” linatupatia fursa nzuri ya kutosheleza mahitaji yetu ya kiroho. Kama chakula cha kimwili chenye kujenga, programu hiyo itatulisha kiroho kwa “maneno ya imani.” (1 Tim. 4:6) Itatuwezesha kumkaribia Yehova zaidi. Na twaweza kutazamia kupata ushauri na kitia-moyo cha kutusaidia tukabiliane na majaribu maishani mwetu. Yehova anatuhakikishia hivi: “Nitakufundisha na kukuonyesha njia utakayoiendea; nitakushauri, jicho langu likikutazama.” (Zab. 32:8) Tuna pendeleo kama nini kuwa na mwongozo huu wenye upendo maishani mwetu! Fikiria hatua kadhaa zenye mafaa tunazoweza kuchukua ili tunufaike zaidi na programu ya kusanyiko.
2 Twahitaji Kutayarisha Moyo Wetu: Kila mmoja wetu ana daraka la kulinda moyo wake wa mfano. (Mit. 4:23) Hiyo inamaanisha tujidhibiti na kuwa wanyoofu kuhusu utu wetu. Wakati wa kusanyiko ni wakati wa kutafakari juu ya uhusiano wetu na Yehova, wakati wa ‘kuchungua ndani ya sheria kamilifu iliyo ya uhuru.’ Ili kutayarisha moyo wetu ‘upokee kupandwa kwa neno,’ twapaswa kumwomba sana Yehova atuchunguze, atuonyeshe ikiwa kuna “njia iletayo majuto” ndani yetu inayohitaji kurekebishwa na atuongoze kwenye “njia ya milele.”—Yak. 1:21, 25; Zab. 139:23, 24.
3 Sikiliza na Utafakari:Yesu alimpongeza Maria kwa kusikiliza maneno yake kwa makini, akisema: “Maria alichagua fungu jema, nalo halitaondolewa mbali naye.” (Luka 10:39, 42) Ikiwa tuna mtazamo kama huo, hatutaruhusu mambo madogo yatukengeushe fikira. Tutahakikisha kwamba tumeketi na kuwa makini wakati wa programu yote. Tutaepuka kuzungumza au kutembea isivyo lazima na kuwa waangalifu tusiwakengeushe wengine kwa simu za mkononi, peja, kamera, na video-kamera.
4 Tunaposikiliza hotuba, itafaa tuandike maandishi mafupi ya kutusaidia tuchanganue jinsi habari hiyo inavyoelezwa. Twapaswa kuunganisha yale tunayosikia na yale tunayojua tayari. Hiyo itatusaidia tuelewe na kukumbuka habari hiyo. Tunapopitia maandishi yetu, twahitaji kufikiria jinsi tutakavyotumia habari hiyo. Kila mmoja wetu anaweza kuuliza hivi: ‘Hiyo inahusuje uhusiano wangu na Yehova? Nahitaji kufanya marekebisho gani maishani mwangu? Naweza kutumiaje habari ninayojifunza ninaposhughulika na wengine? Naweza kuitumiaje katika huduma yangu?’ Zungumza na wengine mambo tuliyofurahia hasa. Kufanya mambo haya kutatusaidia ‘kuhifadhi ndani ya mioyo yetu’ maneno ya Yehova.—Mit. 4:20, 21.
5 Tutumie Yale Tunayojifunza: Baada ya kuhudhuria kusanyiko la wilaya, ndugu mmoja alisema hivi: “Programu hiyo ilikuwa ya pekee sana. Ilimchochea kila mtu achunguze hali ya moyo wake na wa familia yake, na kutoa msaada wenye upendo wa Kimaandiko kama inavyohitajiwa. Imenifanya niwe macho kuhusu wajibu wangu wa kusaidia zaidi kutanikoni.” Yaelekea kwamba wengi wetu tumewahi kuhisi hivyo. Lakini haitoshi tu kuhisi tumejengwa na kuburudishwa. Yesu alisema: “Ikiwa mwajua mambo haya, wenye furaha ni nyinyi ikiwa mwayafanya.” (Yn. 13:17) Lazima tujitahidi kutumia yale ambayo tumejifunza. (Flp. 4:9) Hiyo ndiyo njia pekee ya kutosheleza kikamili mahitaji yetu ya kiroho.
[Sanduku katika ukurasa wa 5]
Tafakari Yale Unayosikia:
■ Yanahusuje uhusiano wangu na Yehova?
■ Naweza kutumiaje yale ninayosikia ninaposhughulika na wengine?
■ Ninaweza kuyatumiaje katika maisha yangu na katika huduma yangu?