Jinsi Kweli Inavyotuweka Huru
1 Wakati fulani, Yesu aliwaambia hivi Wayahudi waliomwamini: “Mtajua kweli, na kweli itawaweka nyinyi huru.” (Yoh. 8:32) Alikuwa akizungumzia uhuru bora zaidi ya uhuru wa kawaida wa kiraia unaopatikana kwa wote—matajiri na maskini, wenye elimu na wasio na elimu. Uhuru ambao Yesu alifundisha ungewaweka watu huru kutokana na dhambi na kifo. Yesu alisema kwamba “kila mtendaji wa dhambi ni mtumwa wa dhambi.” (Yoh. 8:34) Tunatazamia kwa hamu wakati ambapo wanadamu wote watiifu ‘watawekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu na kuwa na uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.’—Rom. 8:21.
2 Kweli kumhusu Yesu na daraka lake katika kusudi la Mungu huleta uhuru huo. Kweli hiyo inatia ndani ujuzi kuhusu dhabihu ya fidia ambayo aliitoa kwa ajili yetu. (Rom. 3:24) Tukikubali na kutii kweli ya Biblia tunaweza kupata uhuru wa kiasi fulani hata sasa kutokana na hofu, kukata tamaa, na mazoea yote yenye kudhuru.
3 Uhuru Kutokana na Hofu na Kukata Tamaa: Hatupaswi kukata tamaa kwa sababu ya hali za ulimwengu kwani tunaelewa kwa nini kuna uovu na tunajua kwamba utaondolewa duniani hivi punde. (Zab. 37:10, 11; 2 Tim. 3:1; Ufu. 12:12) Isitoshe, kweli hutuweka huru kutokana na mafundisho ya uwongo kuhusu hali ya wafu. Tunajua kwamba wafu hawawezi kutudhuru, kwamba hawateseki katika mahali penye mateso ya milele, na kwamba Mungu hawaui watu ili aishi nao katika makao ya roho.—Mhu. 9:5; Mdo. 24:15.
4 Kweli hiyo iliwafariji wazazi fulani wakati mtoto wao alipokufa katika msiba wa barabarani. “Kuna pengo katika maisha yetu ambalo haliwezi kuzibwa hadi tutakapomwona mwana wetu tena katika ufufuo,” mama yake alisema. “Lakini twajua kwamba huzuni yetu ni ya muda tu.”
5 Uhuru Kutokana na Mazoea Yenye Kudhuru: Kweli ya Biblia inaweza kubadili njia ya mtu ya kufikiri na utu wake na hivyo kumfanya asipatwe na matatizo yanayoweza kuepukwa. (Efe. 4:20-24) Kuwa mwaminifu na kufanya kazi kwa bidii kunaweza kumsaidia mtu kuepuka umaskini. (Mit. 13:4) Mtu anapoonyesha upendo ambao unamchochea kujitolea, hilo humwezesha kuwa na uhusiano bora na wengine. (Kol. 3:13, 14) Kuheshimu mpango wa Kikristo wa ukichwa kunapunguza matatizo katika familia. (Efe. 5:33–6:1) Mtu anapoepuka ulevi, ukosefu wa adili katika ngono, kuvuta sigara, na dawa za kulevya anakuwa na afya nzuri.—Mit. 7:21-23; 23:29, 30; 2 Kor. 7:1.
6 Kijana mmoja alizoea kutumia dawa za kulevya kwa miaka tisa na alikuwa ameshindwa kukomesha zoea hilo. Siku moja alikutana na mhubiri aliyekuwa akitoa ushahidi barabarani. Alikubali vichapo, na mipango ikafanywa ili kumtembelea nyumbani kwake. Alianza kujifunza Biblia. Miezi miwili baadaye kijana huyo aliacha kutumia dawa za kulevya kabisa, na baada ya kujifunza kwa miezi minane akabatizwa. Ndugu yake na mke wa ndugu yake walipoona kwamba ameacha zoea hilo, walianza kujifunza Biblia.
7 Wasaidie Wengine Wapate Uhuru: Wale ambao wamefuata mafundisho ya uwongo tangu utotoni wanaweza kushindwa kuelewa uhuru unaoletwa na Neno la Mungu. Huenda mwalimu akahitaji kutumia ustadi wa kipekee na kujitayarisha vizuri ili kufikia mioyo yao. (2 Tim. 4:2, 5) Huu si wakati wa kupunguza bidii katika kazi yetu ya “kuwatangazia mateka uhuru wao.” (Isa. 61:1) Uhuru wa Kikristo una thamani kubwa. Kuupata kunamaanisha uhai wa milele.—1 Tim. 4:16.