Tanguliza Uhudhuriaji wa Mikutano kwa Ukawaida
1 Familia za Kikristo hutanguliza uhudhuriaji wa mikutano kwa ukawaida. Lakini mahangaiko ya maisha ya leo yanaweza kufanya iwe vigumu. Je, kazi za nyumbani, za kimwili, au za shule zinaanza kuchukua wakati ambao umetengwa kwa ajili ya ibada ya Yehova? Kuwa na maoni ya Yehova kutatusaidia kutanguliza mambo yanayopaswa kutangulizwa.—1 Sam. 24:6; 26:11.
2 Mwanamume mmoja Mwisraeli alipuuza maoni ya Yehova kwa kukusanya kuni siku ya Sabato. Huenda alifikiri kwamba alifanya hivyo kwa ajili ya familia yake au kwamba ni jambo dogo tu. Hata hivyo, kupitia hukumu aliyotoa, Yehova alionyesha kwamba kufuatia shughuli za kimwili wakati ambao umetengwa kwa ajili ya ibada ni jambo zito.—Hes. 15:32-36.
3 Kukabiliana na Magumu: Kwa walio wengi, si rahisi kuizuia kazi ya kimwili isiingilie uhudhuriaji wa mikutano. Wengine wamekabiliana na ugumu huo kwa kuongea na mwajiri wao, kubadilishana zamu na wafanyakazi wenzao, kutafuta kazi nyingine inayofaa, au kurahisisha maisha yao. Bila shaka, dhabihu za namna hiyo zinazofanywa kwa ajili ya ibada ya kweli zinampendeza vema Yehova.—Ebr. 13:16.
4 Kazi ya shule pia inaweza kuleta magumu. Kijana mmoja alisema: “Mimi hufanya baadhi ya kazi yangu ya shule kabla ya mikutano, na kuifanya iliyobaki baada ya kurudi nyumbani.” Ikiwa siku za mikutano kazi ya shule haiwezi kumalizwa, wazazi wengine huwaambia walimu kwamba kuhudhuria mikutano ya Kikristo ni jambo la kutangulizwa katika familia yao.
5 Ni muhimu kupanga mambo vizuri na kushirikiana ili kumaliza kazi za nyumbani na kujitayarisha kuhudhuria mikutano kwa wakati mkiwa familia. (Met. 20:18) Hata watoto wadogo wanaweza kufundishwa kuvaa kwa wakati ili kuwa tayari kwenda kwenye mikutano. Wazazi wanaweza kuweka mfano kwa kuwaonyesha watoto wao kwamba mikutano ni muhimu.—Met. 20:7.
6 Kadiri mikazo ya mfumo huu wa mambo inavyoongezeka, ni muhimu tuhudhurie mikutano kwa ukawaida. Na tuendelee kuona mambo jinsi Yehova anavyoyaona na kutanguliza uhudhuriaji wa mikutano kwa ukawaida.—Ebr. 10:24, 25.