Tunawezaje Kuwahubiria Watu wa Jamaa Zetu?
1 Linaweza kuwa jambo lenye kuleta shangwe kubwa kuingia katika ulimwengu mpya pamoja na wapendwa wetu, sote tukiwa na umoja katika ibada ya Yehova! Kwa kuwahubiria watu wa jamaa zetu, huenda wakajifunza jinsi ya kumwabudu Yehova na kupata tumaini la kuishi katika ulimwengu mpya. Hata hivyo, tunahitaji kuwa wenye utambuzi ili kufanya hivyo kwa njia yenye kuchochea. Mwangalizi mmoja wa mzunguko alisema hivi: “Wale wanaowahubiria watu wa jamaa zao pindi kwa pindi kuhusu mambo yanayochochea upendezi, hupata matokeo mazuri sana.” Tunawezaje kufanya hivyo?
2 Amsha Upendezi Wao: Fikiria kimbele jinsi unavyoweza kuamsha upendezi wa watu wa jamaa yako. (Met. 15:28) Wanahangaikia nini? Wanakabili magumu gani? Labda unaweza kuwaonyesha makala au kutaja andiko kuhusu jambo hususa linalowapendeza. Ikiwa hawaishi karibu, unaweza kufanya hivyo kwa kuwaandikia barua au kuwapigia simu. Bila kuwaeleza mambo mengi sana, panda mbegu za kweli, na kutumaini kwamba Yehova atazikuza.—1 Kor. 3:6.
3 Yesu alimwagiza hivi mtu fulani ambaye alikuwa amefukuza roho waovu wengi kutoka kwake: “Nenda nyumbani kwa watu wa jamaa yako, ukawaambie mambo yote ambayo Yehova amekufanyia na jinsi alivyokuonyesha rehema.” (Marko 5:19) Hebu wazia jinsi watu wa jamaa ya mtu huyo walivyovutiwa na jambo hilo! Ingawa huenda usipate matokeo mazuri kama hayo, yaelekea watu wa jamaa yako wanapendezwa na mambo ya kiroho ambayo wewe na watoto wako mnafanya. Kutaja hotuba fulani uliyotoa katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, kusanyiko ulilohudhuria, ziara ya Betheli, au tukio lingine muhimu kunaweza kufanya iwe rahisi kuzungumza nao mambo mengi zaidi kumhusu Yehova na tengenezo lake.
4 Uwe na Utambuzi: Unapowahubiria watu wa jamaa yako, epuka kuwaeleza mambo mengi kwa wakati mmoja. Akikumbuka wakati alipoanza kujifunza Biblia, ndugu mmoja alikiri hivi: “Wakati huo nilimweleza mama yangu mambo mengi sana kuhusu karibu kila jambo nililokuwa nimejifunza katika Biblia, na mara nyingi hilo lilisababisha mabishano, hasa pamoja na baba yangu.” Hata kama mtu wa jamaa yako anapendezwa na ujumbe wa Biblia, toa maelezo kwa njia ambayo ataachwa akiwa na tamaa ya kujua mengi zaidi. (Met. 25:7) Sikuzote onyesha heshima, fadhili, na subira sawa na unavyofanya unapowahubiria watu usiowajua.—Kol. 4:6.
5 Pindi moja, watu wa jamaa ya Yesu walifikiri kuwa amerukwa na akili. (Marko 3:21) Hata hivyo, baadaye, baadhi yao wakawa Wakristo. (Mdo. 1:14) Ikiwa jitihada zako za kwanza za kuwaeleza watu wa jamaa yako kuhusu ile kweli hazitafaulu, usife moyo. Hali na mtazamo wao unaweza kubadilika. Endelea kutafuta nafasi nyingine ya kuwaeleza jambo ambalo huenda likaamsha upendezi wao. Unaweza kupata shangwe ya kuwasaidia kutembea katika barabara iongozayo kwenye uzima wa milele.—Mt. 7:13, 14.
[Maswali ya Funzo]
1. Kwa nini tunahitaji kuwa wenye utambuzi tunapowahubiria watu wa jamaa zetu?
2. Kupendezwa kikweli na watu wa jamaa zetu kunawezaje kutusaidia kuamsha upendezi wao?
3. Upendezi ambao watu wa jamaa zetu wanaonyesha kwa mambo yetu ya kiroho unawezaje kufanya iwe rahisi kuwahubiria?
4. Ni mitego ipi tunayopaswa kuepuka tunapowahubiria watu wa jamaa zetu?
5. Tunahitaji kufanya nini ikiwa watu wa jamaa zetu hawaitikii tunapowahubiria?