Vipi Jamaa Zako?
1 Wengi wetu tuna jamaa kadhaa wasio katika kweli. Jinsi tunavyotamani wapendwa hao wajiunge nasi kwenye barabara iongozayo kwenye uhai! Kuhangaikia kwetu wakati ujao wao wa milele kwaweza kuwa kukubwa zaidi wanapokuwa ni washiriki wa nyumba yetu wenyewe. Ijapokuwa tumejaribu kwa miaka kadhaa kuwavuta wapendezwe na kweli, hatupaswi kuamua kwamba hali hiyo haina tumaini.
2 Yesu alipofanya kazi yake ya kuhubiri, “kwa kweli, ndugu zake walikuwa hawadhihirishi imani katika yeye.” (Yn. 7:5) Wakati mmoja, jamaa zake walifikiri alikuwa mwenye kichaa. (Mr. 3:21) Hata hivyo, Yesu hakukata tamaa nao. Baada ya muda fulani, ndugu zake waliikubali kweli. (Mdo. 1:14) Ndugu-nusu wake Yakobo alikuja kuwa nguzo katika kutaniko la Kikristo. (Gal. 1:18, 19; 2:9) Ikiwa ungetaka kuwa na shangwe ya kuona jamaa zako wakiikubali kweli, usiache kujaribu kuwafikia na habari njema za Ufalme.
3 Uwe Mwenye Kuburudisha, Si Mwenye Kulemeza: Yesu alipowahubiria wengine, wasikilizaji wake walihisi wameburudishwa, si kudhulumiwa. (Mt. 11:28, 29) Hakuwalemeza na mafundisho ambayo hawangeelewa. Ili kuwaburudisha jamaa zako na maji ya kweli, wape ya kiasi cha kikombe, si ya kiasi cha ndoo nzima! Mwangalizi wa mzunguko alisema: “Matokeo bora yanapatikana na wale wanaoamsha udadisi kwa jamaa zao kwa kuwahubiria viwango vilivyopimwa.” Kwa njia hii, hata wapinzani wanaweza kuanza kuuliza maswali na hatimaye kusitawisha kiu ya kweli.—1 Pet. 2:2; linganisha 1 Wakorintho 3:1, 2.
4 Wakristo wengi waliofunga ndoa wametolea ushahidi wenzi wao wasioamini kwa matokeo kwa kuwaachia fasihi ikiwa imefunguliwa mahali ilipo habari ambayo huenda ikawapendeza. Dada mmoja aliyefanya hivi pia aliongoza funzo la Biblia pamoja na watoto wake mume wake akisikiliza, akitoa maelezo ambayo yangemnufaisha. Nyakati nyingine alikuwa akimuuliza mume hivi: “Nilijifunza hivi na hivi katika funzo langu leo. Wewe waonaje?” Mume wake hatimaye aliikubali kweli.
5 Uwe Mwenye Staha, Si Asiye na Subira: Mtangazaji mmoja alieleza kwamba “hata watu wa ukoo wana haki ya kuwa na maoni yao wenyewe na kauli zao.” Kwa hiyo twapaswa kuonyesha staha wanaposema mawazo yao au wanapotuomba kihususa tusiongee nao kuhusu kweli. (Mhu. 3:7; 1 Pet. 3:15) Kwa kuwa wenye subira na wenye upendo na kwa kuwa wasikilizaji wazuri, twaweza kutafuta fursa zifaazo za kutoa ushahidi wenye busara. Subira kama hiyo yaweza kuthawabisha, kama ilivyoonekana katika kisa cha mume Mkristo ambaye alistahimili kwa subira kutendewa kwake vibaya na mke wake kwa miaka 20. Mara tu mke alipoanza kubadilika, huyo mume alisema: “Ninamshukuru Yehova kama nini kwamba alinisaidia kusitawisha ustahimilivu, kwa sababu sasa naweza kuona tokeo: Mke wangu ameanza kutembea katika kijia cha uhai!”
6 Vipi jamaa zako? Huenda ikawa kupitia mwenendo mzuri wa Kikristo na sala zako kwa niaba yao, “ukapata kuwavuta kwa Yehova.”—1 Pet. 3:1, 2, kielezi-chini.