Sehemu ya 6—Kuongoza Mafunzo ya Biblia Yenye Maendeleo
Mwanafunzi Anapouliza Swali
1 Baada ya kuanzisha funzo la Biblia na kuliongoza kwa muda, kwa kawaida ni vizuri kuzungumzia mafundisho ya Biblia kwa utaratibu, badala ya kuzungumzia mambo mengi tofauti-tofauti. Jambo hilo humsaidia mwanafunzi kuelewa mafundisho ya msingi kwa usahihi na kufanya maendeleo kiroho. (Kol. 1:9, 10) Hata hivyo, mara kwa mara wanafunzi huuliza maswali kuhusu mambo mbalimbali wakati wa funzo. Maswali hayo yashughulikiweje?
2 Uwe Mwenye Utambuzi: Maswali yanayohusiana na habari mnayojifunza yanaweza kujibiwa mara moja. Kama swali litazungumziwa baadaye katika kichapo mnachojifunza, huenda ikatosha tu kumweleza mwanafunzi jambo hilo. Hata hivyo, ikiwa swali halihusiani na habari mnayojifunza au linahitaji kufanyiwa utafiti ili kujibiwa ifaavyo, huenda ikafaa kulizungumzia jambo hilo baada ya funzo au wakati mwingine. Baadhi ya wahubiri huona kwamba kuandika swali hilo humhakikishia mwanafunzi kwamba swali lake halipuuzwi na huwasaidia wahubiri wasikengeuke kutoka katika habari wanayojifunza.
3 Mafundisho mengi ya Biblia huzungumziwa kifupi tu katika vichapo vyetu vya funzo. Namna gani ikiwa mwanafunzi ana tatizo la kukubali fundisho fulani au anashikilia sana imani fulani ya uwongo? Huenda ikafaa kutumia kichapo kingine kinachozungumzia kinaganaga yale ambayo Biblia inasema kuhusu jambo hilo. Ikiwa mwanafunzi hasadikishwi, basi liache jambo hilo hadi wakati mwingine na uendelee na funzo lenu la kawaida. (Yoh. 16:12) Anapoendelea kujifunza Biblia na kufanya maendeleo kiroho, huenda akaelewa fundisho hilo la Biblia.
4 Usitoe Maoni Yako: Ikiwa huna hakika kuhusu jibu la swali fulani, usishawishike kutoa maoni yako. (2 Tim. 2:15; 1 Pet. 4:11) Mweleze mwanafunzi kwamba utafanya utafiti kuhusu swali hilo na kumjibu baadaye. Hata unaweza kutumia nafasi hiyo kumwonyesha mwanafunzi jinsi ya kufanya utafiti. Mwonyeshe hatua kwa hatua jinsi anavyoweza kufanya utafiti kwa kutumia vifaa mbalimbali vilivyoandaliwa na tengenezo la Yehova. Kwa njia hiyo, hatimaye yeye mwenyewe ataweza kupata majibu kwa maswali yake.—Mdo. 17:11.