Ratiba ya Familia—Funzo la Familia
1 Ukiwa mzazi Mkristo, zawadi bora zaidi unayoweza kuwapa watoto wako ni kuwasaidia kumpenda Yehova kama wewe unavyompenda. Nafasi muhimu ya kufanya hivyo hupatikana “unapoketi katika nyumba yako” kwa ajili ya funzo la Biblia la familia la kila juma. (Kum. 6:5-7) Iwe una mwenzi wa ndoa anayeamini, familia yenu imegawanyika kidini, au uwe mzazi asiye na mwenzi, unaweza kuwasaidia watoto wako kumkaribia Yehova kwa kuwa na funzo la familia linaloongozwa kwa ukawaida.
2 Kuanzisha Funzo la Familia: Kwanza mnapaswa kuwa na desturi ya kujifunza mkiwa familia. Ikiwa hujui ni wakati gani unaofaa kuwa na funzo hilo, kwa nini msizungumzie jambo hilo mkiwa familia? (Met. 15:22) Ikiwa una watoto wachanga, huenda ukapendelea kuwa na vipindi vifupi vya kujifunza mara kadhaa kila juma. Panga ratiba itakayofaa zaidi hali ya familia yako. Weka wakati hususa wa funzo hilo katika ratiba ya familia yenu, na mhakikishe kwamba mnaufuata.
3 Mnaweza kujifunza mambo gani? Familia fulani hutayarisha habari itakayozungumziwa katika Funzo la Kitabu la Kutaniko au Funzo la Mnara wa Mlinzi litakalofuata. Wengine hujifunza habari inayohusu vijana. Baba mmoja aliye na mwana mchanga na binti mchanga, asema: ‘Sisi huigiza masimulizi ya Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia na hilo hufanya watoto wetu waone funzo la familia kuwa jambo muhimu sana katika juma. Ufahamu na ueleweji tunaopata ni muhimu sana kuliko kusoma tu mafungu mengi.’
4 Jifunzeni Kila Juma: Funzo la familia linapaswa kufanywa kwa ukawaida na kutazamiwa kwa hamu na kila mmoja katika familia. Huenda mkabadili siku na saa ya funzo hilo ili kushughulikia mambo ya dharura. Pia, huenda kukawa na uhitaji wa kuzungumzia jambo tofauti. Lakini mabadiliko hayo hayapaswi kuvuruga ratiba ya funzo la familia kwa muda mrefu. Ikiwa kuna unahitaji wa kubadilisha wakati wa funzo, baba mmoja huandika ujumbe mfupi unaoonyesha wakati funzo litakapofanywa na kuuweka mahali ambapo wote katika familia wanaweza kuuona. Jitihada kama hizo za kuhakikisha kwamba funzo la familia linafanywa kwa ukawaida zinafaa sana. Unapoendelea kuwalea watoto wako “katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova,” utakuwa ukionyesha jinsi unavyowapenda na pia jinsi unavyompenda Baba yetu wa mbinguni.—Efe. 6:4.