Tumia kwa Hekima Vichapo Vyetu Vinavyotegemea Biblia
1 “Nimekuwa nikisoma vichapo vyenu tangu mwaka wa 1965. Mimi huchunguza Biblia ninapovisoma, na kila jambo lililo katika vichapo vyenu linapatana na Biblia. Nimetamani kujua ukweli kumhusu Mungu na Yesu, na ninaweza kusema kwamba ninapata majibu ya kweli katika vichapo vyenu na kwenye Biblia.” Hivyo ndivyo mwanamume fulani alivyosema katika barua aliyoandikia makao makuu ya Mashahidi wa Yehova. Katika barua hiyohiyo, aliomba mtu wa kumfunza Biblia.
2 Kama mtu huyo mwenye uthamini, mamilioni ya watu ulimwenguni huthamini vichapo vya kujifunzia Biblia vinavyochapishwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mt. 24:45) Kila mwaka, vichapo vingi sana huchapishwa ili kuwasaidia watu wanyoofu ‘wapate ujuzi sahihi wa kweli.’ (1 Tim. 2:4) Tunawezaje kutumia kwa hekima vichapo vyetu vinavyotegemea Biblia?
3 Epuka Kuharibu Vichapo: Huenda baada ya muda tukakusanya vichapo vingi sana ambavyo hatutatumia. Tunaweza kufanya nini ili tusiharibu vichapo vyetu vyenye thamani? Tunahitaji kuwa watambuzi tunapochukua vichapo tutakavyotumia kwenye huduma. Badala ya kuchukua nakala nyingi za kichapo kilekile tutakachotumia shambani, tunaweza kuchukua nakala moja tu au mbili na kuchukua nakala nyingine baada ya kugawia watu nakala hizo. Hilo litazuia vichapo vingi visirundamane nyumbani mwetu. Vivyo hivyo, ikiwa tuna magazeti mengi ambayo hatujagawia watu, itafaa tupunguze idadi ya magazeti tunayoagiza.
4 Vichapo Vingi Akibani: Ikiwa kutaniko lina vichapo fulani vilivyorundamana, mratibu wa vitabu anaweza kuwasiliana na makutaniko yaliyo karibu ili kuona kama yanaweza kutumia vichapo hivyo. Wahubiri wanaweza kutoa vichapo vya zamani kwa washiriki wa familia wasioamini, wanafunzi wa Biblia, na wengine. Huenda wale ambao wameanza kushirikiana na kutaniko hivi karibuni wakataka kuwa na vichapo vya zamani kwa ajili ya maktaba zao.
5 Tungependa vichapo vyetu vitimize kusudi lake, yaani, kusaidia watu wanyoofu wajifunze mengi zaidi kuhusu makusudi mazuri ya Yehova. Sawa na Yesu ambaye hakuharibu chakula kilichobaki baada ya kulisha umati kimuujiza, tunapaswa kuweka mradi wa kutumia vizuri vichapo vyenye thamani vinavyotegemea Biblia. (Yoh. 6:11-13) Ujumbe unaookoa uhai ambao uko katika vichapo vyetu hautaweza kugusa mioyo ya watu wanaopenda uadilifu ikiwa utabaki kwenye rafu zetu au mikoba yetu. Kwa hiyo, tunapaswa kutumia busara tunapochukua vichapo vya kuhubiri na kuvitumia kwa hekima ili kuwanufaisha wengine.—Flp. 4:5.
[Maswali ya Funzo]
1, 2. Watu wengi wana maoni gani kuhusu vichapo vyetu, na hilo hutokeza swali gani?
3. Tunawezaje kuepuka kuharibu vichapo vyetu?
4. Kutaniko linaweza kufanya nini iwapo lina vichapo vingi akibani?
5. Tunawezaje kuonyesha kwamba tunathamini vichapo vyetu?